" KAMANDA MAGOMI ASISITIZA WELEDI KWA SUNGUSUNGU SHINYANGA, SEMINA YAFANYIKA KATA YA NDALA

KAMANDA MAGOMI ASISITIZA WELEDI KWA SUNGUSUNGU SHINYANGA, SEMINA YAFANYIKA KATA YA NDALA

Na Elisha Petro, Misalaba Blog

Kamanda wa jeshi la Polisi Mkoa wa Shinyanga kamishna msaidizi wa Polisi Janeth Magomi amelitaka jeshi la jadi Sungusungu kuendelea kutekeleza majukumu yake kwa weledi kwa kuzingatia sheria na taratibu za Nchi.

Ameyasema hayo  wakati akizungumza  na  jeshi la jadi sungusungu wa kata ya Ndala kwenye semina elekezi juu ya utendaji kazi, ambayo imeandaliwa na Diwani wa kata ya Ndala Mhe.  Zamda Shabani ambapo pamoja na mambo mengine  amewakumbusha Sungusungu kutojichukulia sheria mkononi katika utekelezaji wa majukumu yao.

Kamanda Magomi amesema serikali inatambua juhudi za sungusungu katika kukabiliana na uhalifu na wahalifu lakini amesisitiza kuzingatiwa kwa  uzalendo na weledi pamoja na kuendelea kushirikiana na  jeshi la polisi ktk jitihada za kuimarisha ulinzi na usalama kwa wananchi.

“Kiukweli mnafanyakazi nzuri  katika kukahikisha maeneo yetu, mali na watu wetu wote wanakuwa salama hii ni faida ambayo sisi jeshi la Polisi tunaitambua na kuithamini  sana niendelee  kuwataka mfanyekazi hii huku mkitanguliza uzalendo”.

“Niwaase wapiganaji na makamanda wangu wa sungusungu tufanyekazi yetu kwa weledi wa hali ya juu na kwa kuzingatia sheria za Nchi na nawaahidi ushirikiano wa dhati lakini pia ofisi zetu ziko wazi muda wote pale ambapo unatendewa ndiyo sivyo sema sisi tutachukua hatua”.amesema kamanda Magomi.

Aidha kamanda Magomi ametumia nafasi hiyo kuiomba jamii hasa wazazi na walezi kuendelea kushirikiana na serikali katika kutokomeza mmomonyoko wa maadili na kuimarisha ulinzi na usalama.

Kwa upande wake Diwani wa kata ya Ndala Mhe. Zamda Shabani amewasihi jeshi la sungusungu kata hiyo kuendelea kushirikiana katika juhudi za kuimarisha usalama kwa wananchi.

“Tuendelee kudumisha upendo, tuendelee kushirikiana kwa pamoja, tuendelee kusheshimiana kwa nafasi zetu ili safari yetu iwe njema pamoja na kwamba tunahamasisha masuala ya maendeleo hatuwezi kupata maendeleo bila kuwa na usalama lakini niseme makamanda hawa wanatusaidia sana kata ya Ndala niombe tu tuendelee kushirikiana huku tukimtanguliza mwenyezi Mungu”.amesema Mhe. Zamda

Akisoma risala iliyoandaliwa na jeshi la Sungusungu kata ya Ndala katibu wa jeshi hilo Bwana Raymond Misana ameelezea mafanikio mbalimbali yaliyofikiwa na kuahidi kuendelea kushirikiana na jeshi la polisi katika utekelezaji wa majukumu.

“Sungusungu kata ya Ndala pamoja na matukio madogomadogo kwenye mitaa yetu tumefanikiwa kuzuia matukio makubwa yaliyokuwa yakijirudia kama vile wizi wa mifugo, kuvunja na kuiba, upolaji wa simu za mikononi na mikoba ya akina mama kwa kutumia bodaboda na matukio mengine’

“Kwa kiasi kikubwa uhalifu mdogomdogo unaotokea kwa sasa unachangiwa na uzembe wa watu wanaotendewa uhalifu huo ama kwa kutoweka taa za ulinzi kwenye nyumba zao au kwa kutofunga milango na mageti nyakati za usiku pia tunaahidi kuendelea kupokea na kufanyika kazi maelekezo yako kutoka jeshi la Polisi”

Semina hiyo imefanyika katika soko la Ndala  na kuhudhuriwa na viongozi mbalimbali wa kata pamoja na jeshi la polisi  ambapo mgeni rasmi alikuwa kamanda wa jeshi la polisi Mkoa wa Shinyanga ACP Janeth Magomi.

Kamanda wa jeshi la Polisi Mkoa wa Shinyanga ACP Janeth Magomi  akisoma hotuba kwenye semina iliyoandaliwa na Diwani wa kata ya Ndala Mhe.  Zamda Shabani.

Diwani wa kata ya Ndala     Mhe. Zamda Shabani akiomba ushirikiano kwa jeshi la sungusungu kata hiyo.

Diwani wa kata ya Ndala     Mhe. Zamda Shabani akizungumza kwenye semina hiyo

Katibu wa jeshi hilo Bwana Raymond akisoma risala iliyoandaliwa na jeshi la Sungusungu kata ya Ndala.

Post a Comment

Previous Post Next Post