Na Mapuli Kitina Misalaba
Katika
kijiji cha Bushola na Lyandu, kilichopo kata ya Mwamalili, Manispaa ya Shinyanga, maji
yamekuwa kama lulu
isiyoonekana ambapo wakazi
wa vijiji hivi wamekuwa wakikabiliwa na hali ngumu ya upatikanaji wa maji safi
na salama, hali inayowalazimu kutumia maji ya bwawa la asili linalotumiwa pia
na mifugo kama Ng’ombe na Mbuzi, jambo ambalo linahatarisha afya zao kwa
kiwango kikubwa.
MISALABA MEDIA
ilifika katika eneo
hilo na kushuhudia wanawake
na watoto wakichota maji kutoka kwenye bwawa hilo huku likitumika na wanyama hao
na kwamba wakazi hawa,
maji ya bwawa siyo chaguo mbali ni suluhisho la dharura kutokana na ukosefu wa
huduma bora ya majisafi.
“Hili
bwawa tunalitumia sisi binadamu na wanyama. Hakuna kisima wala bomba la maji
hapa. Watoto wanaugua minyoo, kuhara na wengine ngozi zinapauka. Tumechoka,”
alisema Evaline Luzwilo mkazi
wa Lyandu.
Wenyeviti
wa vijiji na watendaji waliozungumza na MISALABA
MEDIA walithibitisha kuwepo kwa tatizo hilo kwa muda mrefu, huku
wakisema kuwa jitihada mbalimbali zimekuwa zikifanyika, lakini bado hakuna
hatua madhubuti zilizochukuliwa.
Wakazi wa maeneo hayo wameomba Serikali iangalie uwezekano wa kuwapatia
huduma ya maji kutoka Ziwa Viktoria,
kama njia ya kudumu ya kuwahakikishia maji safi. Wanadai kwamba hakuna sababu
ya wao kuendelea kutumia maji yasiyo salama ilhali ziwa hilo kubwa liko karibu
na mkoa wa Shinyanga.
“Tunaomba
Serikali ituangalie sisi wa vijijini. Tumevumilia vya kutosha. Kama bomba
linaweza kufikishwa Shinyanga mjini na Kishapu, kwa nini lisitufikie Bushola na
Lyandu?” alihoji Lazaro Masele, mkazi wa Bushola.
Kwa wakazi wa Bushola
na Lyandu, maji ya bwawa si tu hitaji – ni jambo la kulazimika. Katika hali ya
kushangaza na kusikitisha, familia nyingi zinabeba madumu wakati
wakielekea kwenye bwawa moja tu linalopatikana maeneo ya jirani. Katika bwawa hilo
inaelezwa kuwa wenda
wanyama kama Fisi wanatumia hasa nyakati za usiku kwa kuwa huonekana katika
maeneo hayo.
“Tunaogopa
lakini tunaishi kwa mazoea. Hakuna maji ya bomba hapa. Tunasumbuliwa na
magonjwa kila wakati, Watoto wanapata minyoo, kuhara, na hata magonjwa ya ngozi
kwa sababu ya haya maji,” anasema Anastazia Shiku , mkazi wa Bushola.
Diwani wa kata ya Mwamalili, Mhe. James Matinde, hakusita kueleza ukweli ambapo alisema changamoto
ya maji imekuwa sugu na juhudi nyingi zimekuwa zikifanyika kwa nyakati tofauti,
lakini majibu rasmi ya utekelezaji wa mradi wa maji hayajawahi kutolewa kwa
ukamilifu.
“Hili
ni tatizo linaloendelea. Tumeshawasiliana na mamlaka husika, hasa SHUWASA,
lakini mpaka sasa hatujapewa tarehe halisi ya kuanza kwa mradi wa kuwapatia
wananchi maji ya uhakika. Wananchi wamechoka. Tunahitaji msaada wa haraka,”
alisema Mhe. Matinde.
Baada ya malalamiko
kuendelea kuongezeka, Mamlaka ya
Majisafi na Usafi wa Mazingira Shinyanga (SHUWASA) imeeleza kuwa
inatambua changamoto hiyo na inafanya kila jitihada kuhakikisha maji kutoka Ziwa Viktoria yanawafikia wakazi wa Bushola na Lyandu.
Kwa
mujibu wa Mhandisi Uswege Musa,
ambaye ni Kaimu Mkurugenzi wa Usambazaji Maji SHUWASA, tayari kuna mpango wa
kuunganisha bomba kubwa linalosafirisha maji kuelekea wilaya ya Kishapu ili
liweze kutawanya tawi kuelekea Bushola.
“Changamoto
ipo. Kisima cha maji marefu kilichopo Mwagala kina maji yenye chumvi, na
wananchi hawataki kuyatumia. Ndiyo maana sasa tunalenga kutumia mfumo wa maji
kutoka Ziwa Viktoria. Mpango huu ni wa muda mfupi, lakini kuna pia mradi mkubwa
wa muda mrefu,” alisema Mhandisi huyo.
SHUWASA kwa
kushirikiana na Shirika la Maendeleo la
Ufaransa (AFD) na Serikali ya Tanzania, imeandaa mradi wa kuboresha huduma ya maji kwa wakazi wa Manispaa ya Shinyanga.
Mradi
huo unatarajiwa kugharimu mabilioni ya fedha na utahusisha:Kubadilisha mabomba chakavu yenye urefu wa
kilomita 9, Kufunga mabomba mapya ya maji yenye urefu wa zaidi
ya kilomita 35, Kufikia vijiji vya pembezoni kama Bushola, Lyandu,
Iselamagazi, Mwagala na vingine
Kwa sasa, SHUWASA
imemaliza hatua ya kupata mshauri mtaalamu wa mradi, na kinachosubiriwa ni
mkandarasi ambaye ataanza utekelezaji.
“Tunaomba
wananchi waendelee kuwa wavumilivu. Serikali yao kupitia SHUWASA ipo makini na
tunahakikisha hili linashughulikiwa kwa haraka,” aliongeza Mhandisi Uswege.
Licha ya matumaini hayo
mapya, bado wananchi hawana imani ya haraka. Wengi wanasema wamekuwa wakisikia
ahadi kwa muda mrefu bila matokeo ya wazi. Hata hivyo SHUWASA haijataja terehe
ya kuanza utatuzi wa changamoto hiyo ya maji ambapo wananchi wanaendelea kutoa wito kwa viongozi wa serikali, mashirika ya
maendeleo na mashirika ya haki za binadamu kufika kuona hali halisi.
“Hii
siyo maisha ya binadamu. Tunaomba viongozi wasikae ofisini wakisoma ripoti,
wafike hapa waone tunavyoteseka,” alisema Mzee Charles
Dotto, mkazi wa Bushola.
Katika dunia ya sasa
ambapo lengo namba sita la Malengo ya
Maendeleo Endelevu (SDG 6) linataka “Upatikanaji wa maji safi na huduma
za kujisafi kwa wote ifikapo 2030,” ni aibu kuona wakazi wa maeneo ya mijini
kama Shinyanga bado wakitegemea maji ya mabwawa ya wanyama.
Mwenyekiti wa kijiji cha Bushola Edward Machiya
Lyokala anatoa wito kwa serikali, mashirika yasiyo ya
kiserikali, viongozi wa dini na mashirika ya kiraia kushirikiana kuhakikisha
maji safi yanapatikana kwa wakazi wa Bushola na Lyandu haraka iwezekanavyo.
Wakati hayo yakiendelea
Shinyanga, Waziri wa Maji Jumaa Aweso
amewasilisha bungeni makadirio ya
Mapato na Matumizi ya Wizara ya Maji kwa mwaka wa fedha 2025/2026,
ambapo ametaja vipaumbele saba ambavyo serikali inatarajia kuvitekeleza ili
kuboresha huduma ya maji nchini.
Miongoni
mwa vipaumbele hivyo ni: Kuzuia upotevu wa maji, Kusimamia rasilimali
za maji, Kuendeleza rasilimali maji, Kuboresha ubora wa huduma ya maji safi na majitaka,
Kusambaza maji
mijini na vijijini, Kudhibiti upotevu wa maji, Kujenga uwezo wa
kitaasisi wa wizara
Hata hivyo, bado
haijabainika moja kwa moja kama vijiji vya Bushola na Lyandu ni miongoni mwa
maeneo yatakayopata kipaumbele kupitia bajeti hiyo mpya.
Ni wazi kuwa changamoto
ya maji kwa wakazi wa Bushola na Lyandu si jambo la kisiasa, bali ni suala la
maisha ya kila siku. Wito umetolewa
kwa Wizara ya Maji,
SHUWASA, na viongozi wa Mkoa wa Shinyanga kuhakikisha wanashughulikia kwa
dharura hali hii ya hatari. Maji
ni uhai na hakuna maendeleo
bila afya.
MWISHO
Baadhi ya wakazi wa kata ya Mwamalili changamoto ya maji.
Majibu ya SHUWASA
Post a Comment