
Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam
KLABU ya Yanga SC imetangaza kuingia mkataba na kampuni ya kiteknolojia ya BlackBird kutoka Rotterdam, Uholanzi, kwa ajili ya matumizi ya teknolojia ya Artificial Intelligence (AI) katika ukusanyaji wa taarifa za wachezaji wake.
Akizungumza leo Septemba 11, 2025 jijini Dar Es Salaam Rais wa Yanga, Eng. Hersi Said, amesema kuwa klabu hiyo imeandika historia kwa kuwa ya kwanza barani Afrika kuingia kwenye ushirikiano huo wa kiteknolojia.
“Leo tumeingia mkataba na kampuni ya BlackBird kutoka Rotterdam, Uholanzi. Mkataba huu ni kwa ajili ya teknolojia ya Artificial Intelligence (AI), mfumo ambao utatusaidia kukusanya taarifa za wachezaji wetu. Klabu ya Yanga ndio ya kwanza Afrika kuingia kwenye mkataba huu,” amesema Eng. Hersi.
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa BlackBird, Thim van der Weijden, amesema kuwa wamefurahishwa kushirikiana na Yanga, wakieleza kuwa klabu hiyo imeonyesha mwelekeo wa kisasa na mabadiliko ya kweli katika uendeshaji wake.
“Tunayofuraha kubwa sana kuwa mshirika wa kiteknolojia na klabu ya Yanga. Tumeichagua Yanga kwa sababu ni klabu kubwa sana Afrika na tumetiwa moyo na mchakato wao wa mabadiliko. Mfumo huu umetupatia fursa ya kufanya kazi na moja ya klabu inayokwenda sambamba na kasi ya teknolojia,” amesema Thim.
Ushirikiano huu unatarajiwa kuiwezesha Yanga kusimamia kwa ufanisi zaidi rekodi na takwimu za wachezaji, hatua ambayo wadau wa soka wanaona kuwa ni mapinduzi makubwa katika tasnia ya michezo barani Afrika.
Post a Comment