" SERIKALI INACHUNGUZA TUKIO LA UKATILI DHIDI YA MTOTO - WAZIRI DKT. GWAJIMA

SERIKALI INACHUNGUZA TUKIO LA UKATILI DHIDI YA MTOTO - WAZIRI DKT. GWAJIMA



Na. Meleka Kulwa

Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Dkt. Dorothy Gwajima, amesema Serikali kuanza kuchukua hatua kufuatia taarifa za tukio la ukatili dhidi ya mtoto linalodaiwa kutokea eneo la Kinyerezi, Zimbili Mtipesa au karibu na Msikiti wa Mzee Uranga, Manispaa ya Ilala, Dar es Salaam.

Amesema Maafisa Ustawi wa Jamii wameshaanza kushughulikia suala hilo sambamba na vyombo vya dola, huku viongozi wa Mkoa wa Dar es Salaam na Manispaa ya Ilala wakishiriki kikamilifu katika ufuatiliaji wa kina wa tukio hilo.

Dkt. Gwajima ametoa wito kwa jamii kuwa na utulivu wakati Serikali ikiendelea kukusanya na kuandaa taarifa kamili kwa ajili ya umma. Aidha, ametoa ombi maalum la kumtafuta mama mzazi wa mtoto aliyekatiliwa, akimtaka awasiliane naye haraka kupitia namba ya simu 0765 345777.

Amehakikishia wananchi kuwa kila anayehusika na ukatili dhidi ya watoto atachukuliwa hatua kali za kisheria kwa mujibu wa Sheria ya Mtoto, huku akiendelea kuthamini mchango wa wananchi wanaotoa taarifa za vitendo vya ukatili.

Kupitia ukurasa wake wa Instagram, January 11,2025, Dkt. Gwajima amewashukuru wananchi waliotoa taarifa za tukio hilo akiwemo Yericko Nyerere, Jemedarisaid na wengine, akibainisha kuwa taarifa hizo tayari zilipelekwa Kituo cha Polisi na taratibu za kisheria zinaendelea kuchukuliwa.

Katika ujumbe wake, Waziri Gwajima amesisitiza kuwa ukatili dhidi ya watoto ni jambo lisilokubalika na kwamba Serikali, kwa kushirikiana na jamii, imejipanga kukomesha vitendo hivyo.

“Ukatili kwa watoto tutaukomesha wenyewe jamii kwa ushirikiano wetu, kwa kutoa taarifa mapema na kwa kuyaibua matukio ya ukatili sambamba na kuelimishana kuacha fikra za kikatili,” amesema.





Post a Comment

Previous Post Next Post