" KATIBU WA JUMUIYA YA WAZAZI CCM MPANDA AUNGANA NA WANAWAKE KUADHIMISHA SIKU YA WANAWAKE DUNIANI

KATIBU WA JUMUIYA YA WAZAZI CCM MPANDA AUNGANA NA WANAWAKE KUADHIMISHA SIKU YA WANAWAKE DUNIANI

Katibu wa Jumuiya ya Wazazi CCM Wilaya ya Mpanda, Ndugu Jimotoli Jilala Maduka, ameungana na wanawake wa Manispaa ya Mpanda Mkoa wa Katavi katika maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani yaliyofanyika kwa shangwe na matukio mbalimbali ya kijamii.

Katika maadhimisho hayo, wanawake wa Manispaa ya Mpanda walifanya maandamano yaliyopita katika baadhi ya barabara za manispaa hiyo kabla ya kukusanyika katika viwanja vya Ukumbi wa Manispaa ambako kulifanyika kongamano pamoja na michezo mbalimbali ya burudani.

Miongoni mwa michezo iliyochezwa ni pamoja na kuvuta kamba, kukimbiza kuku, kula mayai kwa kutumia kijiko, kunywa soda kwa dakika moja pamoja na michezo mingine iliyolenga kuimarisha mshikamano, furaha na ushirikiano miongoni mwa wanawake.

Akizungumza katika maadhimisho hayo, Ndugu Jimotoli Jilala Maduka amewapongeza wanawake kwa juhudi zao katika kujiletea maendeleo pamoja na mchango wao mkubwa katika familia na jamii kwa ujumla. Amesema wanawake ni nguzo muhimu ya maendeleo hivyo ni muhimu kuendelea kuwapa nafasi na kuwawezesha ili waweze kufikia malengo yao ya kiuchumi na kijamii.

Mgeni rasmi katika tukio hilo, akimwakilisha Mkuu wa Wilaya ya Mpanda, Katibu Tawala wa Wilaya hiyo Fidesiana Mwanakulya amesema serikali inaendelea kuweka mikakati mbalimbali ya kuwawezesha wanawake kiuchumi ikiwemo kuwapatia mikopo yenye masharti nafuu kupitia halmashauri.

Amesema kupitia mpango wa mikopo ya asilimia 10 inayotolewa na halmashauri kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu, wanawake wengi tayari wamenufaika na kuweza kuanzisha na kuendeleza shughuli mbalimbali za kiuchumi zinazowasaidia kuboresha maisha yao na ya familia zao.

Maadhimisho hayo yamekuwa fursa muhimu kwa wanawake kukutana, kubadilishana uzoefu na kuhamasishana kuhusu umuhimu wa umoja, mshikamano na kufanya kazi kwa bidii ili kuendelea kuleta maendeleo katika jamii.



  

  • Wasiliana nasi:
    📍 East African Spirits (T) Ltd
    📞 +255 767 650 806 | +255 652 096 254

Post a Comment

Previous Post Next Post