Mganga Mkuu wa Manispaa ya Shinyanga, Dkt. Elisha Robert, akitoa elimu kuhusu umuhimu wa chanjo ya polio kwa wadau na kuwahimiza wazazi kuhakikisha watoto wanapatiwa chanjo kwa wakati.
Serikali kupitia Wizara ya Afya inatarajia kuendesha
zoezi la utoaji wa chanjo ya matone ya polio kuanzia Mei 7 hadi 10, 2026,
likilenga watoto wote walio chini ya umri wa miaka 10. Hii ni awamu ya pili ya
kampeni hiyo ya kitaifa, baada ya awamu ya kwanza kufanyika Machi mwaka huu.
Katika kujiandaa na utekelezaji wa zoezi hilo,
serikali imeendesha mafunzo maalum kwa wadau mbalimbali wenye ushawishi katika
jamii, yakiwemo viongozi wa kimila, dini na makundi ya kijamii, kwa lengo la
kujenga uelewa wa pamoja na kuhakikisha ujumbe sahihi unawafikia wananchi.
Akizungumza wakati wa mafunzo hayo yaliyofanyika Mei
4, 2026, Mratibu wa Chanjo Manispaa ya Shinyanga, Ramadhani Maneno, alisema
lengo kuu ni kuhakikisha jamii inaelewa umuhimu wa chanjo hiyo na kushiriki
kikamilifu katika kampeni hiyo inayotekelezwa katika mikoa saba ikiwemo
Shinyanga, Geita, Mara, Singida, Simiyu, Kagera na Tabora.
Alisema katika Manispaa ya Shinyanga pekee, jumla ya
watoto 71,966 wanatarajiwa kupatiwa chanjo hiyo katika awamu ya pili, ikiwa ni
jitihada za kuimarisha kinga dhidi ya ugonjwa wa polio ambao unaweza
kusababisha kupooza kwa ghafla na ulemavu wa kudumu kwa watoto.
“Tumekamilisha maandalizi ya kutosha kuhakikisha
hakuna mtoto anayekosa chanjo. Tumeunda jumla ya timu 91, ambapo timu 83
zitafanya kazi ya kuwafikia watoto nyumba kwa nyumba, na timu 8 zitahudumu
katika maeneo ya mikusanyiko kama masoko na vituo vya huduma za jamii,” alisema
Maneno.
Kwa upande wake, mwakilishi kutoka Ofisi ya Waziri
Mkuu (TAMISEMI) Idara ya Afya, Linda Chatila, alisema kampeni hiyo siyo mpya
bali ni mwendelezo wa juhudi za muda mrefu za serikali kudhibiti ugonjwa huo.
Alifafanua kuwa uamuzi wa kuendesha kampeni maalum umetokana na kubainika kwa
vimelea vya polio katika maji taka jijini Mwanza, hali iliyozua tahadhari ya
kitaifa.
“Polio haina tiba, lakini inazuilika kwa chanjo. Ni
wajibu wa kila mzazi kuhakikisha mtoto wake anapata chanjo kwa wakati ili
kumkinga dhidi ya hatari ya kupooza,” alisema Chatila.
Aliongeza kuwa chanjo hiyo ni salama na imeidhinishwa
na taasisi za kitaifa na kimataifa ikiwemo Shirika la Afya Duniani (WHO) pamoja
na Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA). Alitoa rai kwa wazazi kupuuza taarifa
potofu zinazosambazwa kuhusu chanjo hiyo na badala yake kufuata maelekezo ya
wataalamu wa afya.
Akizungumza katika mafunzo hayo, Mganga Mkuu wa
Manispaa ya Shinyanga, Dkt. Elisha Robert, alisema zoezi la chanjo ya polio ni
muhimu katika kulinda afya za watoto na kuzuia madhara makubwa yanayoweza
kusababishwa na ugonjwa huo.
Alieleza kuwa
polio ni ugonjwa hatari unaoweza kusababisha ulemavu wa kudumu kwa mtoto ndani
ya muda mfupi, hivyo ni lazima jamii ichukue hatua za kinga mapema.
Dkt. Robert aliwahimiza wazazi na walezi kuhakikisha
watoto wote walio chini ya umri wa miaka kumi wanapatiwa chanjo hiyo bila
kukosa, akisisitiza kuwa chanjo ni salama, haina madhara na ndiyo njia bora ya
kuzuia ugonjwa huo.
Aidha, alitoa wito kwa wadau na viongozi wa jamii
kuendelea kutoa elimu sahihi kwa wananchi ili kuondoa hofu na imani potofu
zinazoweza kuathiri mafanikio ya zoezi hilo.
Wadau mbalimbali waliohudhuria mafunzo hayo wameeleza
kuunga mkono jitihada hizo za serikali. Kamanda Mkuu wa Sungusungu Mkoa wa
Shinyanga, John Kadama, alisema watashirikiana kikamilifu kuhakikisha zoezi
hilo linafanyika kwa ufanisi hadi kufikia kila mtoto anayelengwa.
Naye Mwenyekiti wa Baraza la Ushauri la Wazee Manispaa
ya Shinyanga, Stephano Tano, aliwataka wazazi na walezi kutumia fursa hiyo
kuhakikisha watoto wao wanapatiwa chanjo, akibainisha kuwa ni njia muhimu ya
kuzuia ulemavu na vifo vinavyoweza kuepukika.
Serikali imeendelea kusisitiza kuwa mafanikio ya kampeni hiyo yanategemea ushirikiano wa wadau wote, hasa wazazi na walezi, katika kuhakikisha watoto wote walio chini ya miaka 10 wanapatiwa chanjo kwa wakati, ili kulinda afya ya kizazi cha sasa na kijacho.
Mratibu wa Chanjo Manispaa ya Shinyanga, Ramadhani Manen. akielezea zoezi hilo. 
Mratibu wa Chanjo Manispaa ya Shinyanga, Ramadhani Maneno akielezea. 
Linda ChaMwakilishi kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu TAMISEMI idara ya afya, Linda Chatila.
Mganga Mkuu wa Manispaa ya Shinyanga, Dkt. Elisha Robert, akitoa elimu kuhusu umuhimu wa chanjo ya polio kwa wadau na kuwahimiza wazazi kuhakikisha watoto wanapatiwa chanjo kwa wakati.
Mganga Mkuu wa Manispaa ya Shinyanga, Dkt. Elisha Robert, akitoa elimu kuhusu umuhimu wa chanjo ya polio kwa wadau na kuwasisitiza wazazi kuhakikisha watoto wanapatiwa chanjo kwa wakati.

Kamanda Mkuu wa Sungusungu Mkoa wa Shinyanga, John Kadama.
Washiriki wa mafunzo.
Washiriki wa mafunzo.
SHY TALENT FILMS - CONTENT YA MWISHO DRAMA
🥃🍶 TUMIA VINYWAJI BORA VYA KAMPUNI YA EAST AFRICAN SPIRITS – BEI RAFIKI, LADHA SAFI BILA HARUFU MBAYA
Wasiliana nasi:
📍 East African Spirits (T) Ltd











Post a Comment