
Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) imeendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu haki na wajibu wao katika sekta za nishati na maji, sambamba na kuhamasisha uwekezaji wa vituo vya mafuta vijijini ili kuongeza upatikanaji wa huduma salama na kukomesha biashara holela ya mafuta.
Hatua hiyo ni sehemu ya mafanikio ya ushiriki wa EWURA katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika Viwanja vya Chinangali, jijini Dodoma, ambapo maelfu ya wananchi wamefika katika banda la mamlaka hiyo kupata elimu na ufafanuzi kuhusu huduma mbalimbali zinazodhibitiwa na EWURA.
Akizungumza katika maonesho hayo, Kaimu Meneja wa Mawasiliano na Uhusiano wa EWURA, Wilfred Mwakalosi, amesema kwa siku nane mfululizo mamlaka hiyo imekuwa ikitoa elimu kwa wananchi kuhusu sekta za mafuta, umeme, gesi asilia na maji, pamoja na kupokea na kushughulikia maswali na changamoto mbalimbali zinazowakabili watumiaji wa huduma hizo.
Amesema wananchi wengi walitumia fursa hiyo kupata ufahamu kuhusu namna ya kuwasilisha malalamiko wanapokumbana na changamoto za huduma, huku mada ya uwekezaji katika vituo vya mafuta vijijini ikiwa miongoni mwa masuala yaliyoibua maswali mengi zaidi.
“Wananchi wengi walitaka kufahamu taratibu na fursa zilizopo za kuanzisha vituo vya kisasa vya mafuta vijijini ili kuondokana na biashara ya mafuta inayofanyika kwa kutumia chupa, ndoo na magaloni, ambayo mara nyingi huhatarisha usalama wa watu na mali,” amesema Mwakalosi.
Ameeleza kuwa Serikali kupitia EWURA imeweka mazingira rafiki ya uwekezaji kwa kupunguza kwa kiasi kikubwa gharama za vibali na leseni kwa wawekezaji wa vituo vya mafuta vijijini.
Kwa mujibu wa EWURA, ada ya kibali cha ujenzi wa kituo cha mafuta katika maeneo ya vijijini imepunguzwa kutoka Shilingi 500,000 zinazotozwa maeneo ya mijini hadi Shilingi 50,000, huku ada ya leseni ikishushwa kutoka Shilingi milioni moja hadi Shilingi 100,000.
Mbali na punguzo hilo, EWURA imepunguza baadhi ya masharti ya uwekezaji kwa kuruhusu matumizi ya nyaraka za uthibitisho wa umiliki wa ardhi zinazotolewa na serikali za vijiji badala ya hati kamili za ardhi zinazohitajika katika maeneo ya mijini.
Hatua hiyo inalenga kuvutia wawekezaji wengi zaidi katika maeneo ya vijijini na kuongeza upatikanaji wa mafuta kwa njia salama, nafuu na inayozingatia viwango vya usalama.
Katika maonesho hayo, wananchi pia walipata ufafanuzi kuhusu namna EWURA inavyosimamia ukokotoaji wa bei za mafuta, viwango vya huduma za maji na umeme, pamoja na taratibu za kuwasilisha malalamiko pale wanaporidhika au kutoridhika na huduma zinazotolewa na watoa huduma.
Aidha, Mwakalosi amewahimiza wananchi kusoma na kuelewa mikataba ya huduma kwa wateja inayotolewa na taasisi za maji, umeme na nishati, akieleza kuwa mikataba hiyo inaainisha kwa uwazi haki, wajibu na viwango vya huduma vinavyopaswa kutolewa kwa mteja.
Amesisitiza kuwa wananchi wenye uelewa wa mikataba hiyo wanakuwa na uwezo mkubwa wa kudai huduma bora, kufuatilia utekelezaji wa haki zao na hata kudai fidia pale ambapo watoa huduma watashindwa kutekeleza viwango walivyoahidi.
Vilevile, EWURA imewahakikishia wananchi kuwa nchi inaendelea kuwa na hali nzuri ya upatikanaji wa umeme, gesi na maji kutokana na uwekezaji mkubwa unaoendelea kufanywa na Serikali katika sekta hizo.
Mwakalosi ametaja ongezeko la uzalishaji wa umeme kupitia Bwawa la Mwalimu Nyerere kuwa miongoni mwa hatua zilizochangia kuimarika kwa huduma za nishati nchini, huku EWURA ikiendelea kusimamia upatikanaji endelevu wa huduma za maji na nishati kwa manufaa ya wananchi wa sasa na vizazi vijavyo.
Post a Comment