" USAFIRISHAJI HARAMU WA BINADAMU WAENDELEA KUWA TISHIO HASA KWA WASICHANA

USAFIRISHAJI HARAMU WA BINADAMU WAENDELEA KUWA TISHIO HASA KWA WASICHANA

Usafirishaji haramu wa binadamu umeendelea kuwa changamoto kubwa nchini, huku wasichana kutoka maeneo ya vijijini wakiwa miongoni mwa waathirika wakuu kutokana na ahadi za ajira, elimu na maisha bora ambazo baadaye huishia kuwaingiza katika mazingira ya unyonyaji na unyanyasaji.

Akizungumza kwa niaba ya katibu Tawala wa Mkoa wa Shinyanga ambaye pia ni Afisa Maendeleo ya Jamii Mkoa, Rehema Edson, wakati akifungua semina ya mafunzo kuhusu usafirishaji haramu wa binadamu na uhamiaji salama kwa maafisa mbalimbali wa serikali.

Mafunzo hayo yamefanyika kupitia mradi wa EmPoWedeD II unaotekelezwa na mashirika ya CVM na APA kwa ushirikiano na CHODAWU pamoja na Wote Sawa, kwa ufadhili wa Italian Agency for Development Cooperation.

Rehema amesema watoto wengi, hususan wasichana balehe ambao walipaswa kuwa shuleni, wamekuwa wakidanganywa kwa ahadi za ajira na kusafirishwa kwenda kufanya kazi za nyumbani katika makazi binafsi, ambako hukumbana na mazingira magumu ya kazi na ukiukwaji wa haki zao.

Ameeleza kuwa baadhi ya changamoto wanazokutana nazo ni kufanya kazi kwa saa nyingi bila mapumziko, kulipwa mishahara midogo au kutolipwa kabisa, kunyimwa haki ya kupata elimu, pamoja na kukumbana na unyanyasaji wa kimwili, kisaikolojia na unyonyaji wa kiuchumi.

Kwa mujibu wa Rehema, changamoto hiyo ni ngumu zaidi kubainika kwa kuwa kazi nyingi hufanyika ndani ya nyumba binafsi, hali inayowafanya waathirika kutotambulika kwa urahisi.

Aidha, amesema bado kuna watoto wanaoajiriwa katika shughuli za kilimo, ufugaji, uchimbaji mdogo wa madini, biashara zisizo rasmi na uuzaji wa bidhaa mitaani.

Ameongeza kuwa wahalifu wanaojihusisha na usafirishaji haramu wa binadamu wamebadili mbinu zao, ambapo mbali na kutumia madalali wa kawaida, sasa wanatumia teknolojia, mitandao ya kijamii, matangazo ya ajira za uongo pamoja na mifumo isiyo rasmi ya uajiri ili kuwavuta waathirika.

Kwa upande wake, mwezeshaji kutoka Shirika la CVM, Mwajuma Ally, amesema mradi wa EmPoWedeD II umeanza awamu ya pili baada ya mafanikio yaliyopatikana katika utekelezaji wa awamu ya kwanza.

Amesema mradi huo utatekelezwa kwa kipindi cha miaka mitatu kuanzia mwaka 2026, ukiweka mkazo katika kuwawezesha wasichana wanaofanya kazi za nyumbani kupata mafunzo ya stadi kupitia vyuo mbalimbali, pamoja na kuhakikisha wanapatiwa mikataba ya ajira na waajiri wao ili kulinda haki zao.

Naye mwezeshaji wa semina hiyo kutoka Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, Providence Simbila, amesema usafirishaji haramu wa binadamu ni kosa la jinai kwa mujibu wa sheria za Tanzania na kwamba vitendo hivyo vina viashiria vinavyoweza kutambuliwa mapema.

Amevitaja baadhi ya viashiria hivyo kuwa ni matumizi ya ahadi za uongo kuhusu mishahara mikubwa au ajira nzuri, udanganyifu unaolenga kuwashawishi waathirika kukubali kusafirishwa, pamoja na vitisho au shinikizo vinavyolenga kuwanufaisha wahusika wa uhalifu huo.

Washiriki wa semina hiyo wamehimizwa kuendelea kutoa elimu kwa jamii, kuimarisha ushirikiano kati ya taasisi mbalimbali na kuwahamasisha wananchi kutoa taarifa mapema kuhusu viashiria vya usafirishaji haramu wa binadamu ili kulinda haki na usalama wa makundi yaliyo katika mazingira hatarishi, hususan wanawake na watoto.

Afisa Maendeleo ya Jamii Mkoa, Rehema Edson.mwezeshaji kutoka Shirika la CVM, Mwajuma Ally





 

Post a Comment

Previous Post Next Post