" UKOSEFU WA ELIMU YA USALAMA UNAVYOHATARISHA MAISHI YA WACHIMBAJI WADOGO WA MADINI SHINYANGA

UKOSEFU WA ELIMU YA USALAMA UNAVYOHATARISHA MAISHI YA WACHIMBAJI WADOGO WA MADINI SHINYANGA


Na Mapuli Kitina Misalaba

Sekta ya uchimbaji mdogo wa dhahabu katika Mkoa wa Shinyanga imeendelea kuwa tegemeo muhimu la uchumi wa wananchi wengi, hususan katika migodi ya Mwakitolyo na Nyandolwa ambapo kupitia migodi hiyo, mamia ya wakazi wamepata ajira za moja kwa moja na zisizo za moja kwa moja, biashara ndogondogo zimeimarika, na familia nyingi zimeanza kushuhudia mabadiliko ya kiuchumi.

Hata hivyo, nyuma ya mchango huo wa kiuchumi kuna hatari kubwa inayowakabili wachimbaji, inayochangiwa kwa kiasi kikubwa na ukosefu wa elimu ya haki za msingi za mfanyakazi, kanuni za usalama kazini, pamoja na uwajibikaji hafifu wa waajiri na mamlaka husika.

Uchunguzi uliofanywa na Misalaba Media unaonesha kuwa idadi kubwa ya wachimbaji wadogo na vibarua wa migodini hawana uelewa wa kutosha kuhusu haki zao pindi ajali zinapotokea na kwamba wengi hawajui taratibu za fidia, bima, msaada wa dharura, wala namna ya kushirikiana na inspekta wa migodi katika masuala ya usalama.

Katika kipindi cha mwaka 2022 hadi 2025, migodi ya Nyandolwa na Mwakitolyo mkoani Shinyanga imerekodi jumla ya watu 72 waliokumbwa na ajali kubwa migodini. Kati yao, watu 36 wamethibitishwa kufariki dunia, mmoja (1) hajapatikana, na 11 wamejeruhiwa, huku 27 wakinusurika katika matukio hayo.

Katika mgodi wa Nyandolwa uliopo kata ya Mwenge kwenye leseni ya kikundi cha Wachapakazi Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga, ajali ya mwaka 2022 ilihusisha watu 30, ambapo watu sita (6) walifariki dunia sawa na asilimia 20 ya waathirika wote, huku watu 24 wakinusurika.

Hata hivyo, ajali ya Agosti 11, 2025 katika mgodi huo wa Nyandolwa ilihusisha watu 25, ambapo 21 walifariki dunia, watatu (3) waliokolewa wakiwa hai na mmoja hajapatikana, ikiwa ni kiwango cha vifo cha takribani asilimia 84 na kwamba Desemba 2025 kuliripotiwa kifo cha mtu mmoja (1) katika ajali nyingine.

Katika mgodi wa Mwakitolyo, Mei 17, 2025 watu 17 waliathirika katika ajali Mwakitolyo namba 2, ambapo watu sita (6) walifariki dunia na 11 kujeruhiwa, sawa na kiwango cha vifo cha asilimia 35. Tukio lingine mwishoni mwa mwaka 2025 katika Kitalu namba 15 lilisababisha vifo vya watu wawili (2) ambao miili yao haikupatikana.

Katika ajali hiyo, Samwel Makenzi Chembanya, kijana mchimbaji mdogo, alipoteza maisha baada ya kuangukiwa na kifusi. Familia yake ilieleza kuwa haikuwa na uelewa wa masuala ya fidia wala msaada wa dharura, hali iliyowaacha katika changamoto kubwa za kiuchumi na kijamii.

Mchimbaji mdogo Kulwa Mpelwa alisema kuwa licha ya kufanya kazi mgodini kwa muda mrefu, hajawahi kupatiwa mafunzo rasmi ya usalama kazini, hali inayomfanya kufanya kazi bila uelewa wa nini cha kufanya endapo atapata ajali au jeraha akiwa kazini.

Mchimbaji Bwana Mpiga Mhamal alisema baadhi ya duara hazifungwi nguzo ipasavyo, huku wengine wakivamia duara bila kufuata taratibu ili kupata dhahabu kwa haraka huku Kandya Ndutu akidai kuwa ukaguzi wa inspekta haufanyiki mara kwa mara, na wakati mwingine taarifa za hatari hazifiki kwa wamiliki wa migodi kwa wakati.

Kwa upande wake, Boniface Misong’oni, alieleza kuwa hata elimu ya haki za mfanyakazi haijawahi kuwafikia wachimbaji wengi, jambo linalowaacha katika hatari kubwa wanapopatwa na ajali.

Akizungumza na Misalaba Media, Mwenyekiti wa Kijiji cha Mwakitolyo namba 2, Bwana Chongo Lutenganija, alieleza kuwa kumekuwepo na ajali nyingine ambazo haziripotiwi rasmi kwa mamlaka husika, licha ya kusababisha vifo vya wachimbaji mmoja mmoja au wawili, hali inayozuia hatua za kudumu kuchukuliwa.

Alishauri kuwa ukaguzi wa mara kwa mara katika maduara unapaswa kuwa wa lazima, huku hatua za haraka zikichukuliwa pale hatari zinapobainika ili kuzuia ajali kabla hazijatokea.

Kwa upande wa Nyandolwa, Mwenyekiti wa Kijiji cha Mwongozi, Bwana Mange Didas, alisema ajali migodini zimekuwa mzigo mkubwa kwa jamii, hasa kwa familia zinazopoteza wapendwa wao bila fidia ya haraka wala msaada wa kisaikolojia na kwamba alipendekeza elimu ya mara kwa mara kuhusu usalama kazini pamoja na haki zao itolewe kwa vitendo.

Kwa upande wa wafanyakazi wa pembezoni, akina mama wanaobonda mawe ya dhahabu walisema nao wanakabiliwa na hatari kubwa kutokana na ukosefu wa elimu ya usalama na mazingira machafu ya kazi.

Christina alisema hafanyi kazi kwa kutumia mafunzo rasmi ya usalama, bali hutegemea uzoefu wa muda mrefu na mbinu za jadi kujilinda. Stella, anayefanya kazi ya kuponda mawe naye alisema ajali ndogondogo zimekuwa zikimuathiri kiafya na kiuchumi kutokana na kukosekana kwa elimu ya usalama kazini.

Mkazi wa Mwakitolyo, Esther Jackson, alisema ajali migodini huathiri moja kwa moja biashara ndogondogo na ustawi wa familia nyingi huku  Mchungaji Paul James akisema vifo na majeraha migodini huacha maumivu makubwa ya kijamii na kiuchumi pale msaada wa dharura na fidia unapokosekana.

Inspekta wa migodi Samson Jelemiah alisema changamoto kubwa ni kupuuzwa kwa maelekezo ya usalama wanayotoa kwa wamiliki wa migodi. Dotto Seleman alisema baadhi ya inspekta hukumbana na vitisho wanapotekeleza majukumu yao.

Clement Samson alisema mafunzo ya mara kwa mara kwa inspekta bado hayatoshi, huku Mussa Bilia akieleza kuwa bila ulinzi wa kisheria, inspekta hushindwa kusimamia usalama ipasavyo.

Mjiolojia kutoka Ofisi ya Afisa Madini Mkoa wa Shinyanga, James Kibiti Muiko, alisema Tume ya Madini ina jukumu la kusimamia shughuli zote za uchimbaji ikiwemo masuala ya usalama, lakini tofauti ya uchimbaji mdogo na wa kati husababisha changamoto kubwa zaidi katika migodi midogo.

Migodi ya Mwakitolyo na Nyandolwa imeendelea kuwa mhimili wa uchumi wa Mkoa wa Shinyanga, lakini ajali za mara kwa mara zinaonesha gharama kubwa ya maendeleo hayo kwa maisha ya wachimbaji.

Wachimbaji wagodo walipendekeza elimu ya mara kwa mara kuhusu haki zao na kanuni za usalama itolewe, vifaa vya kujikinga vitolewe kwa kila mfanyakazi, ukaguzi wa mara kwa mara ufanyike na upatikanaji wa fidia na bima uboreshwe.

Mdau wa shughuli za uchimbaji madini kutoka kata ya Salawe, Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga, Hosea Marco, alitoa wito kwa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) kuongeza uwepo wake katika maeneo ya migodi kwa kutoa elimu na kufanya ufuatiliaji wa karibu, hatua itakayosaidia kupunguza vitendo vya rushwa na kuimarisha usalama kwa wachimbaji wadogo.

Diwani wa Kata ya Mwenge Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga, Mhe. Raphael Maharage alisema ili kupunguza ajali katika migodi ya wachimbaji wadogo ni muhimu kwa inspekta wa migodi kufanya ukaguzi wa mara kwa mara na kuchukua hatua kwa duara zinazobainika na dosari.

Katibu wa Wanawake Wachimbaji Taifa, kupitia Shirikisho la Vyama vya Wachimbaji Wadogo wa Madini Tanzania (FEMATA), Evelyne Cleophace Nzinza alisisitiza kuwa inspekta wanapaswa kufanya kazi kwa uadilifu na kuweka mbele usalama wa wachimbaji ikiwemo kuchukua hatua stahiki pale hatari inapobainika.

Mrakibu Msaidizi wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Mkoa wa Shinyanga, ambaye pia ni Kaimu Kamanda wa jeshi hilo mkoani humo, Thomas Majuto, alisema jeshi hilo linashauri uchimbaji ufanyike kwa mtindo wa mteremko wa nyuzi 30 hadi 45 (horizontal angle), kwani njia hiyo hurahisisha utengenezaji wa njia za pembeni kwa ajili ya kufikia eneo la tukio wakati wa ajali, tofauti na mtindo wa kuchimba wima moja kwa moja chini ambao huongeza hatari na kuathiri upatikanaji wa njia za uokoaji.

Amezikumbusha mamlaka za kisekta kuwasikiliza na kuwasimamia kwa karibu wachimbaji wadogo, akieleza kuwa mara nyingi hutanguliza tamaa ya kufikia madini bila kuzingatia usalama wa maisha yao, na wakati mwingine hulazimisha kuingia maeneo yasiyo salama, jambo linaloweza kusababisha ajali.

Majuto ametoa wito kwa wachimbaji kutambua kuwa usalama huanza kabla ya shughuli za uchimbaji kuanza, na kusisitiza kuwa mamlaka za usalama, ikiwemo OSHA, zinapaswa kuendelea kufanya ziara za mara kwa mara migodini kwa ajili ya kutoa elimu na miongozo ya kitaalamu itakayosaidia kupunguza ajali na madhara.

Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Kimadini Shinyanga, Mhandisi Noel Baraka, alisema kwa mujibu wa kanuni za usalama, umbali kati ya duara na duara haupaswi kupungua mita kumi ambapo Ofisi ya Madini itaendelea kusimamia Kanuni za Usalama na Utunzaji wa Mazingira Mahali pa Kazi za mwaka 2010, ambazo zinataka umbali huo uzingatiwe.

Mhandisi Baraka alisema iwapo itabainika kuwa maduara yapo karibu kuliko inavyotakiwa, hatua za kusimamisha leseni ya eneo husika zitachukuliwa huku akieleza kuwa ukaguzi unaendelea katika maeneo mengine ili kuzuia ajali kama iliyotokea Nyandolwa.

Akitoa wito kwa wachimbaji wadogo, alisema wanapaswa kufuata sheria na kanuni za usalama bila shuruti, kuzingatia upangaji sahihi wa maduara kwa mujibu wa maelekezo ya maafisa wa madini, na kutumia baruti kwa kufuata taratibu. Pia aliwataka kutoa taarifa mapema pindi wanapobaini dalili za hatari ili hatua stahiki zichukuliwe kabla ya kutokea kwa majanga makubwa.

MWISHO

 


 

Post a Comment

Previous Post Next Post