" KAMATI YA BUNGE YA UTAWALA NA SERIKALI ZA MITAA (USEMI) YAIPONGEZA MANISPAA YA SHINYANGA KWA UTEKELEZAJI MZURI WA MIRADI

KAMATI YA BUNGE YA UTAWALA NA SERIKALI ZA MITAA (USEMI) YAIPONGEZA MANISPAA YA SHINYANGA KWA UTEKELEZAJI MZURI WA MIRADI

Kamati ya kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa (USEMI) imeridhishwa na utekelezaji unaoendelea wa miradi mbalimbali ya maendeleo katika Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga kwa kutumia fedha za mapato ya ndani kwa lengo la kutatua changamoto za wananchi.

Kamati hiyo leo imetembelea na kukagua miradi mbalimbali ikiwemo ujenzi wa soko kuu la kisasa la Mkoa wa Shinyanga pamoja na shule ya wasichana Butengwa iliyopo kata ya Ndembezi ambapo Mwenyekiti wa kamati hiyo Mhe. Daniel Londo amepongeza uongozi wa Halmashauri hiyo kwa matumizi sahihi ya fedha za mapato ya ndani.

Mhe. Longo amesema Halmashauri hiyo imefanya ubunifu ambao utakuwa chachu kwa maendeleo ya wananchi na Taifa kwa ujumla na kwamba ameziomba Halmashauri zingine Nchini kuiga mfano kutoka katika Manispaa hiyo.

“Nipongeze sana watumishi wa Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga kwa uzalendo mkubwa, weledi lakini kutanguliza mbele maslahi makubwa ya Taifa tunapenda mtumike kama rejea kwa watumishi wengine Tanzania miradi hii ambayo mmeitekeleza katika Halmashauri hii ya Manispaa ya Shinyanga kama ingetekelezwa katika kila Manispaa ya Nchi hii naamini kabisa safari yetu kuelekea kwenye mafanikio ingekuwa fupi na muda mchache zaidi kuliko tunaoenda nao”

“Nikupongeze Mkurugenzi wa Manispaa ya Shinyanga na timu yao uzalendo ambao unauonesha kamati imeuona rai yetu tunaomba sana uendelee kuwa mzalendo kwa Nchi yao”amesema Mhe. Longo

“Lakini kitendo cha wafanyabishara kuukubali mradi wa soko kamati hii inauzoefu wa kupokea malalamiko katika miradi ambayo inawahusisha wamachinga, wauzamitumba na wafanyabishara ndogo ndogo katika safari zetu tumekuwa tukipokea malalamiko lakini hali hiyo imekuwa tofauti sana kwa hapa Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga kwakweli tunawapongeza sana”.amesema Mhe. Longo

Kwa upande wake Naibu waziri ofisi ya Rais Tamisemi Deo Ndejembi wakati kamati hiyo ikitembelea na kukagua ujenzi wa soko kuu la kisasa la Mkoa wa Shinyanga, amesema Manispaa hiyo imefanya utekelezaji wenye tija ambao utawanufaisha wafanyabishara wakubwa kwa wadogo.

“Naipongeza Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga kwa kuja na mradi huu wa ubunifu lakini mradi ambao unatatua pia kero za wafanyabiashara wadogo wadogo lakini pia Halmashauri hii kwa kutenga fedha wamefanya jambo kubwa sana na nijambo la kuigwa na Halmashauri zingine ambazo kwenye mapato ya ndani zinauwezo wa kutekeleza miradi mikubwa kama hii”.amesema Naibu Waziri Ndejembi

Awali akizungumza Mkurugenzi wa Manispaa ya Shinyanga Dkt. Jomaary Satura amesema ujenzi wa soko kuu la kisasa la Mkoa wa Shinyanga unatekelezwa kwa kutumia fedha za mapato ya ndani ambao utagharimu kiasi cha shilingi Bilion 1.8.

Mkurugenzi Dkt. Satura amesema ujenzi wa soko kuu la kisasa la Mkoa wa Shinyanga ghorofa moja itakuwa na vyumba 106 na kwamba mradi huo utawanufaisha wafanyabishara, wananchi pamoja na Halmashauri katika ukusanyaji wa mapato ya ndani.

Baadhi ya wabunge akiwemo mbunge wa viti maalum Mkoa wa Shinyanga kupitia chama cha Demokrasia na Maendeleo CHADEMA Mheshimiwa Salome Makamba wameipongeza Halmashauri kwa ubunifu huo wa miradi ya maendeleo ambayo  itawanufaisha wananchi hasa wa Manispaa ya Shinyanga.

Wabunge hao pia wamesisitiza kuharakishwa kwa miradi hiyo ambapo wamesema endapo miradi itakamilika kwa wakati itamaliza kero za wananchi ambao wengi wanatarajia kunufaika.

Kamati ya kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa (USEMI)) leo Machi 17, 2023 imefanya ziara ya kutembelea na kukagua miradi mbalimbali katika Manispaa ya Shinyanga ambapo imetembelea na kukagua mradi  wa ujenzi wa soko kuu la kisasa la Mkoa wa Shinyanga, ujenzi wa soko la mitunga lililopo kata ya Ngokolo, ujenzi wa majengo ya huduma katika kwenye kituo cha afya Kambarage pamoja na ujenzi wa shule ya wasichana Butengwa kata ya Ndembezi na kwamba miradi hiyo ipo katika Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga.Kamati ya kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa (USEMI) ikiwa katika mradi wa ujenzi wa soko kuu la kisasa la Mkoa wa Shinyanga ambapo mradi huo unatekelezwa kwa mapato ya Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga.

Post a Comment

Previous Post Next Post