" MAADHIMISHO YA MIAKA 47, CCM WILAYA YA SHINYANGA MJINI YAFANYIKA KOLANDOTO MWENYEKITI AHIMIZA UCHAGUZI SERIKALI ZA MITAA 2024

MAADHIMISHO YA MIAKA 47, CCM WILAYA YA SHINYANGA MJINI YAFANYIKA KOLANDOTO MWENYEKITI AHIMIZA UCHAGUZI SERIKALI ZA MITAA 2024

Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Shinyanga mjini Mhe. Anord Makombe akizungumza kwenye maadhimisho ya Miaka 47 ya chama hicho, ambayo yamefanyika katika eneo la shule ya sekondari Kolandoto Manispaa ya Shinyanga.

Na Mapuli Kitina Misalaba

Chama Cha Mapinduzi CCM Wilaya ya Shinyanga mjini leo Februari 2,2024 kimeadhimisha Miaka 47 ya kuzaliwa kwa Chama hicho  ambapo Shughuli hiyo imefanyika sanjari na zoezi la kupanda miti, kutolewa elimu ya madarasa ya itikadi kwa wanachama na viongozi wa ngazi za matawi na baadaye Mkutano wa hadhara.

Maadhimisho hayo yamefanyika katika viwanja vya Shule ya Sekondari Kolandoto  Manispaa ya Shinyanga ambapo Chama hicho kimepanda miti zaidi ya Mia tano kama sehemu ya kuunga mkono kampeni ya upandaji miti Nchini.

Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi CCM Wlaya ya Shinyanga Mjini  Mhe. Anord Makombe akizungumza baada ya zoezi la upandaji miti amehimiza uongozi wa shule hiyo kutunza miti yote iliyopandwa leo ili iweze kustawi vizuri ambapo hatua hiyo itasaidia kufikia melengo yaliyokusudiwa katika kupambana na mabadiliko ya tabia nchi.

Mwenyekiti huyo wakati akizungumza kwenye mkutano wa hadhara, amesema kuelekea uchaguzi wa Serikali za Mitaa Chama hicho kitachagua safu ya viongozi bora  wenye uwezo, sifa, utashi na maono, ambao wanakubalika    kwa wananchi.

Pamoja na mambo mengine amesisitiza mchakato wa kuwapata wenyeviti wa serikali za Mitaa,vijiji na vitongoji pamoja na wajumbe wao ufanyike kwa kuzingatia maslahi ya wananchi.

“Tutakapochagua viongozi wabovu tutakapochagua viongozi kwa sababu tu amekuja amekuletea Sukari amekuletea Chumvi amekuletea Kitenge lakini unajua kabisa mtu huyu uwezo wake ni mdogo tutakwenda pasipo,  kwahiyo tunachokitaka ninyi wenyewe mkafanye tathimini kwanza mtuletee watu ambao mnajua kwamba wanakubalika kwa wananchi”.amesema Mwenyekiti Makombe

Aidha Mwenyekiti  Makombe amewakumbusha wazazi na walezi kuhusu umuhimu wa kupeleka watoto shule kwa kuwa serikali imeweka mazingira wezeshi ya watoto kujifunzia.

“Ndugu zangu na wazazi wenzangu niwaombe itakuwa ni aibu tunavyoona shule zimejengwa vizuri na shule za msingi zipo halafu bado watoto hawaendi shule ni jambo la aibu mno utakuwa ni mtu wa ajabu mno kushindwa kumpeleka mtoto shule wakati elimu ni bure kuanzia chekechea mpaka kidato cha sita ni bure kabisa sasa shida ni nini niwaombe kila mtu awe kiongozi kwa jirani yake ukiona mtoto haendi shule mripoti haraka sana jirani yako usimuonee aibu tunataka Taifa la watu wenye weledi haiwezekani mtu anakaa nyumbani hajui kusoma na kuandika yaani hajui Dunia inakwendaje ni muhimu kila mtu kupata elimu hasa kizazi cha sasa”.amesema Makombe

Kwa upande wake Mstahiki Meya wa Manispaa ya Shinyanga Mhe. Elias Ramadhan Masumbuko wakati akizungumza kwenye maadhimisho hayo naye amewakumbusha wazazi kuendelea kusimamia jukumu la malezi na makuzi bora ya watoto,huku akisisitiza watoto kupelekwa shule hasa waliochaguliwa kuingia kidato cha kwanza.

Wakati huo huo amewakumbusha wakazi wa Manispaa ya Shinyanga kuendelea kuchukua tahadhari ya kujikinga na ugonjwa wa kipindupindu ikiwemo kuzingatia usafi katika maisha ya kila siku.

Maadhimisho hayo ya Miaka 47 ya kuzaliwa kwa CCM, katika Wilaya ya Shinyanga mjini yamehudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Chama hicho wakiwemo madiwani wa kutoka kwenye kata zote 17 za Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga.  

Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Shinyanga mjini Mhe. Anord Makombe akizungumza kwenye maadhimisho ya miaka 47 ya CCM ambayo yamefanyika katika kata ya Kolandoto.

Mstahiki meya wa Manispaa ya Shinyanga Mhe. Elias Ramadhan Masumbuko akizungumza kwenye maadhimisho hayo leo Februari 2,2024.Diwani wa kata ya Kambarage Mhe. Hassan Mwendapole akizungumza kwenye maadhimisho hayo.Diwani wa kata ya Kolandoto Mhe. Mussa Andrew akizungumza kwenye maadhimisho hayo.Diwani wa kata ya Ibadakuli Mhe. Msabila Malale akizungumza kwenye maadhimisho hayo.
Awali zoezi la upandaji miti likiendelea katika eneo la shule ya sekondari Kolandoto Manispaa ya Shinyanga.









Post a Comment

Previous Post Next Post