" CHADEMA JIMBO LA SHINYANGA MJINI YALALAMIKIA CHANGAMOTO KWENYE UANDIKISHAJI WA WAPIGA KURA

CHADEMA JIMBO LA SHINYANGA MJINI YALALAMIKIA CHANGAMOTO KWENYE UANDIKISHAJI WA WAPIGA KURA

Na Mapuli Kitina Misalaba

Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) jimbo la Shinyanga mjini kimeeleza hofu yake juu ya changamoto zinazojitokeza katika zoezi la uandikishaji wa wapiga kura, kikidai kuwa baadhi ya mawakala wake wananyimwa takwimu sahihi na wasimamizi wa vituo vya kujiandikisha.

Madai haya yameibua mjadala mzito kuhusu ufanisi na uwazi wa zoezi hili muhimu katika maandalizi ya uchaguzi wa serikali za mitaa unaotarajiwa kufanyika baadaye mwaka huu.

Kwa mujibu wa Mwenyekiti wa CHADEMA jimbo la Shinyanga mjini, Bwana Hamis Ngunila, pamoja na Katibu wa jimbo hilo, Bwana Sebastian Polepole, matatizo haya yamejitokeza katika vituo kadhaa vya uandikishaji vilivyopo ndani ya jimbo hilo.

Wakiwa wanazungumza na Misalaba Media, viongozi hao wameeleza kuwa mawakala wa chama hicho wamekuwa wakinyimwa taarifa muhimu zinazohusiana na idadi ya wananchi wanaojitokeza kujiandikisha na kuboresha taarifa zao.

Bwana Ngunila ameongeza kuwa bila kuwa na takwimu sahihi na zinazolingana, itakuwa vigumu kuhakikisha uwazi na usawa katika uchaguzi ujao wa serikali za mitaa.

Bwana Polepole naye ameongeza kwa kusema, "Tunakabiliana na hali ambapo mawakala wetu wanakosa ushirikiano kutoka kwa wasimamizi wa vituo, hii inazua wasiwasi mkubwa juu ya uwazi wa zoezi hili na kuleta mashaka juu ya matokeo ya mwisho."

CHADEMA imemwomba msimamizi mkuu wa zoezi hilo jimbo la Shinyanga mjini kuchukua hatua za haraka na kuhakikisha kuwa mawakala wa vituo vya uandikishaji wanatoa ushirikiano kwa mawakala wa vyama vyote, ikiwemo CHADEMA, ili kuhakikisha takwimu zinazopatikana ni sahihi na zinafanana ili kuepuka mkanganyiko wowote na kuhakikisha kuwa kila kura inahesabika kwa haki.

Mbali na kutoa wito kwa wasimamizi wa vituo vya uandikishaji, CHADEMA pia imewaomba wananchi wa Shinyanga kujitokeza kwa wingi kushiriki katika zoezi hili la uandikishaji.

Bwana Hamis Ngunila, amesisitiza umuhimu wa wananchi kuhakikisha wanajiandikisha na kuboresha taarifa zao, ili wawe na sifa za kupiga kura katika uchaguzi wa serikali za mitaa.

"Hii ni haki yenu ya kikatiba. Ni muhimu kuhakikisha mnashiriki katika mchakato huu kwahiyo tunawaomba mjitokeza kwa wingi kwenye vituo”. amesema Ngunila

Bwana Ngunila pia amehitimisha kwa kusema kuwa chama hicho kitaendelea kufuatilia kwa karibu zoezi hili na kuhakikisha kuwa haki inatendeka.

"Hatutakubali udanganyifu au ukiukwaji wowote wa haki za wapiga kura, tutaendelea kusimamia maslahi ya wananchi na kuhakikisha kuwa kila mwananchi anapata fursa ya kushiriki kikamilifu katika uchaguzi ujao," amesema Ngunila.

Hali hii inakuja wakati ambapo maandalizi ya uchaguzi wa serikali za mitaa yakiendelea kwa kasi, huku vyama vya siasa vikijipanga kujiimarisha na kuhakikisha kuwa wapiga kura wao wanakuwa na sifa stahiki za kushiriki katika uchaguzi huo.

Changamoto zinazodaiwa kujitokeza sasa zinaweza kuwa na athari kubwa kwenye mchakato wa uchaguzi, na hivyo ni muhimu kwa mamlaka husika kuchukua hatua za haraka kurekebisha hali hiyo.

Kwa mujibu wa ratiba iliyotolewa na Tume ya Uchaguzi, mchakato wa kuchukua fomu za kugombea utafanyika kuanzia tarehe 01 Novemba 2024, na utafuatiwa na kampeni za uchaguzi ambazo zitaanza tarehe 20 hadi 26 Novemba 2024.

 Siku ya kupiga kura imepangwa kuwa tarehe 27 Novemba 2024, ambapo wananchi watajitokeza kuchagua viongozi wao katika uchaguzi wa serikali za mitaa.

Katika mwendelezo wa ufuatiliaji wa zoezi hili, Misalaba Media itaendelea kukuletea habari za kina na za kipekee kuhusu maendeleo ya uandikishaji wapiga kura na matukio mengine muhimu yanayoendelea jimboni Shinyanga.

 

Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) jimbo la Shinyanga mjini, Bwana Hamis Ngunila, akielezea sheria na kanuni za uchaguzi leo Agosti 22,2024.

 Katibu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) jimbo la Shinyanga mjini Bwana Sebastian Polepole, akizungumza leo Agosti 22,2024.


Post a Comment

Previous Post Next Post