" TAASISI YA NASIMAMA NA MAMA YAAHIDI KUSIMAMIA HAKI NA MAADILI SHINYANGA, RC MACHA AIPONGEZA

TAASISI YA NASIMAMA NA MAMA YAAHIDI KUSIMAMIA HAKI NA MAADILI SHINYANGA, RC MACHA AIPONGEZA


Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mhe. Anamringi Macha.

Na Mapuli Kitina Misalaba

Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mhe. Anamringi Macha, ameipongeza taasisi ya “Nasimama na Mama” kwa malengo yake ya kusaidia wananchi hususan wanawake, vijana na makundi yenye uhitaji katika jamii kwa kusimamia haki, kuhamasisha maendeleo na kudhibiti vitendo vya ukatili.

RC Macha ametoa pongezi hizo wakati wa hafla ya viongozi wa taasisi hiyo kujitambulisha ofisini kwake, ambapo amesema taasisi hiyo imeonyesha dira nzuri ya kuunga mkono juhudi za serikali katika kulinda utu, kukuza maadili na kuchochea maendeleo ya kiuchumi kwa wananchi.

“Nawapongeza kwa kazi mnayofanya ya kusimamia haki za wanawake, watoto, wanaume na watu wasio na sauti. Ni vyema mkahakikisha kuwa taasisi hii inakuwa msaada wa kweli kwa jamii kwa kutekeleza majukumu yenu kwa weledi na kwa kuzingatia sheria za nchi,” amesema RC Macha.

Aidha, amehimiza taasisi hiyo kuendelea kutoa elimu kwa vijana kuhusu umuhimu wa kujiepusha na makundi hatarishi na badala yake wajikite kwenye shughuli halali zitakazowawezesha kiuchumi na kimaadili.

Aidha, RC Macha amehimiza taasisi hiyo pia kushiriki kikamilifu katika kuhamasisha jamii kuhusu umuhimu wa kushiriki kikamilifu kwenye shughuli za maendeleo, ikiwemo uchaguzi unaotarajiwa kufanyika mwaka huu.

Akizungumza kwa niaba ya Katibu wa taasisi hiyo Mkoa wa Shinyanga, Katibu wa Kanda ya Serengeti (Shinyanga, Simiyu na Mara), Renatus Mzenmo amesema taasisi hiyo itaendelea kutekeleza majukumu yake kwa kufuata sheria, taratibu na kanuni za nchi.

“Tunaahidi kutekeleza maelekezo ya Mkuu wa Mkoa kwa vitendo. Tutasimama na mama, kijana, au mtu yeyote ambaye hana sauti katika jamii kwa ajili ya haki, usawa na maendeleo,” amesema Mzenmo.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Taasisi ya Nasimama na Mama Mkoa wa Shinyanga, Zamda Shaban, amesema taasisi hiyo ni mwamvuli wa kuisaidia jamii hasa wale wanaonyimwa haki, kufanyiwa ukatili au kutelekezwa.

Ameongeza kuwa pia wanajihusisha na sekta ya ujasiriamali na wanahamasisha vijana na wanawake kuchangamkia fursa za kiuchumi na kijamii.

Taasisi ya “Nasimama na Mama Popote Nilipo” imeanzishwa hivi karibuni kwa lengo la kuwa sauti ya wanyonge, kusimamia haki, na kuchochea maendeleo jumuishi kwa wanawake, vijana na makundi mengine.

Taasisi ya “Nasimama na Mama Popote Nilipo” imeanzishwa kwa lengo la kuwainua watu waliokosa sauti katika jamii, kulinda haki za binadamu, na kuhimiza maendeleo jumuishi kwa ushirikiano na serikali na wadau wa maendeleo.

Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mhe. Anamringi Macha, akiipongeza Taasisi ya Nasimama na Mama Mkoa wa Shinyanga leo Aprili 30, 2025.
Mwenyekiti wa Taasisi ya Nasimama na Mama kanda ya Serengeti, Oscar Kaijage akizungumza. 

Katibu wa Kanda ya Serengeti (Shinyanga, Simiyu na Mara), Renatus Mzenmo akizungumza kwa niaba ya katibu wa Taasisi hiyo Mkoa wa Shinyanga.






Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mhe. Anamringi Macha (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya viongozi wa Taasisi ya Nasimama na Mama Mkoa wa Shinyanga leo Aprili 30, 2025.


Post a Comment

Previous Post Next Post