Na Mapuli Kitina Misalaba
Katika Halmashauri ya Wilaya ya
Kishapu, vitendo vya ukatili wa kijinsia vinaendelea kuwa chanzo kikuu cha
mateso, vifo visivyo vya lazima, kukatishwa kwa ndoto za watoto wa kike, na
kuzorota kwa haki za binadamu. Takwimu zilizotolewa na Afisa Maendeleo ya Jamii
wa Halmashauri hiyo, Ibrahim Sakulia, zinaonesha picha halisi ya uhalisia wa
maisha ya wanawake na wasichana katika wilaya hiyo.
Kwa kipindi cha Januari hadi Machi
2024, jumla ya matukio 64 ya ubakaji na ulawiti yameripotiwa – wanawake wakiwa
61 na wanaume watatu. Idadi hiyo inazidi kuongezeka kwa kasi, kwani kati ya
Aprili hadi Juni pekee, matukio ya ubakaji na ndoa za utotoni kwa jinsi ya kike
yalifikia 203. Kuanzia Julai hadi Septemba, visa vya ukatili wa kingono
viliripotiwa 89 kwa wanawake na tukio moja kwa mwanaume, huku kuanzia Oktoba
hadi Desemba matukio yakiwa 157 kwa wanawake na mawili kwa wanaume.
Takwimu hizi zinaibua maswali mazito
kuhusu usalama wa wanawake na wasichana katika jamii, na ni dhahiri kuwa kuna
haja ya hatua za haraka na madhubuti ili kupunguza ukatili huu ambao umeonekana
kuota mizizi.
Takwimu za kitaifa za mwaka 2022
zinaonesha kuwa asilimia 85 ya wanawake walihudhuria kliniki wakati wa
kujifungua, huku asilimia 81 wakijifungulia katika vituo vya afya, na 65%
wakisaidiwa na wahudumu wa afya. Hata hivyo, bado changamoto kubwa ipo kwenye
uhuru wa kufanya maamuzi kuhusu afya ya uzazi.
Kati ya wanawake wenye umri wa miaka
15 hadi 49, ni asilimia 47 hadi 49.6 pekee waliofanya maamuzi ya kutumia njia
za uzazi wa mpango au kujali afya zao pasipo kuingiliwa. Hali hii inaashiria
kuwa bado wanaume wanashikilia maamuzi mengi kuhusu afya ya uzazi wa wenza wao,
jambo linalohitaji mjadala wa wazi katika familia na jamii.
Katika viwango vya ukatili kwa
mujibu wa viashiria vya kitaifa:
- Vipigo: 22.3%
- Ukatili wa kingono: 8.7%
- Ndoa za utotoni: 32.4%
- Maamuzi binafsi ya wanawake: 72%
Lakini katika mkoa wa Shinyanga,
hali ni mbaya zaidi:
- Vipigo: 34.2%
- Ukatili wa kingono: 17.8%
- Ndoa za utotoni: 45.9%
- Maamuzi binafsi ya wanawake: 77%
Takwimu hizi zinaonesha kuwa
Shinyanga inahitaji juhudi za makusudi kukabiliana na hali hiyo kupitia elimu
endelevu, mabadiliko ya kifikra na ushirikiano wa karibu kati ya viongozi,
wazazi na vijana.
Kaimu Mratibu wa Huduma za Mama na
Mtoto katika Hospitali ya Wilaya ya Kishapu, Hilda Ebunka, anaeleza kuwa hali
ya mimba za utotoni imeanza kupungua kutokana na juhudi mbalimbali za utoaji wa
elimu kwa jamii. Lakini bado anasisitiza kuwa jamii inapaswa kuendelea
kushirikiana ili kulinda watoto wa kike dhidi ya ndoa za utotoni na vitendo vya
unyanyasaji.
Afisa Ustawi wa Jamii, Paul
Lupolaso, anabainisha kuwa ndoa za utotoni ni moja ya changamoto zinazokwamisha
maendeleo ya watoto wa kike, huku akihimiza wazazi kuwapa watoto wao nafasi ya
kufikia ndoto zao kwa kupitia elimu.
Naye Mkuu wa Dawati la Jinsia na Watoto
Wilaya ya Kishapu, Inspekta Rose Mbwambo, anasisitiza kuwa jamii inapaswa
kushirikiana kwa karibu na vyombo vya dola kwa kutoa taarifa za ukatili mapema
ili hatua zichukuliwe kwa mujibu wa sheria. Anasema dawati hilo limekuwa
kimbilio kwa wahanga wa ukatili wa kijinsia na limechangia kuwapa faraja na
msaada wa kisheria wahanga wengi.
Wananchi kutoka kata za Idukilo,
Mwamalasa, Ukenyenge na Mwamashele, wanaomba elimu iendelee kutolewa ambapo
walisema wananchi wengi hawana uelewa jambo ambalo linasababisha matukio hayo
ya ukatili kuendelea katika Wilaya ya Kishapu.
Shija Mongo wa kata ya Mwamashele
anasema: “Tulikuwa tunaona haya kuzungumzia masuala ya ndoa za utotoni,
lakini sasa tumeelewa kuwa ukimya wetu ni hatari kwa watoto wetu. Tumejifunza
kuwa majadiliano ni silaha ya mabadiliko.”
Antony Francis kutoka Ukenyenge
anaongeza: “Makundi rika ni njia nzuri ya kutengeneza sauti moja katika
familia na jamii. Tunahitaji kuendelea kujifunza na kushirikiana kwa ajili ya
kizazi bora.”
Ukatili wa kijinsia hauwezi kukomeshwa kwa sheria pekee. Unahitaji mabadiliko ya kifikra, ushirikiano wa jamii nzima, na nafasi ya mazungumzo ya wazi kati ya vijana na wazee kupitia midahalo ya makundi rika.
Post a Comment