" MHE. ZAMDA SHABAN ATOA TAARIFA YA UTEKELEZAJI WA ILANI YA CCM 2020-2025 KATA YA NDALA

MHE. ZAMDA SHABAN ATOA TAARIFA YA UTEKELEZAJI WA ILANI YA CCM 2020-2025 KATA YA NDALA

Diwani wa Kata ya Ndala ambaye pia ni Naibu Meya wa Manispaa ya Shinyanga, Mhe. Zamda Shaban Mwebea akizungumza mbele ya wajumbe wa mkutano mkuu wa CCM kata ya Ndala.

Na Mapuli Kitina Misalaba

Diwani wa Kata ya Ndala ambaye pia ni Naibu Meya wa Manispaa ya Shinyanga, Mhe. Zamda Shaban Mwebea, amewasilisha taarifa ya utekelezaji wa Ilani ya CCM kwa kipindi cha mwaka 2020 hadi 2025 katika kikao maalum na Wajumbe wa Mkutano Mkuu wa CCM Kata ya Ndala. Ambapo katika utangulizi wake, amesema:

“Najiona mtu mwenye faraja, na mtu mwenye upendo wa dhati kwa wananchi wenzangu wa Ndala. Aidha narudisha shukrani kwa Mungu kwa hii miaka mitano hadi nafikia kusoma utekelezaji wa hii ilani, na upendo wenu na maombi yenu ni faraja kwangu iliyonipa nguvu kusonga mbele na kupambania maendeleo ya wana Ndala.”

Kata ya Ndala ni miongoni mwa kata 17 katika Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga, ikiwa na mitaa mitano: Banduka, Mapinduzi, Mwabundu, Mlepa, na Ndala. Kwa mujibu wa sensa ya mwaka 2022, ina jumla ya wakazi 13,323; wanaume 6,359 na wanawake 6,964. Mtaa wa Mlepa unaongoza kwa idadi kubwa ya watu huku Mapinduzi ukiwa na idadi ndogo zaidi.

Ilani ya Uchaguzi ya CCM 2020-2025 ina kurasa 303, sura 10, na maneno 104,082. Kata ya Ndala imekuwa sehemu muhimu ya utekelezaji wa ilani hiyo kwa vitendo.

 ULINZI NA USALAMA

Kwa mujibu wa Ibara ya 105 (e) na (f) ukurasa wa 157 wa ilani ya CCM, kata ya Ndala imeunda Kamati za Ulinzi na Usalama katika ngazi ya kata na mitaa yote mitano. Taarifa zote za kiusalama zimekuwa zikiwasilishwa na kufanyiwa kazi kwa wakati. Kwa zile zinazohitaji maamuzi ya juu zaidi, zimekuwa zikiwasilishwa kwa mamlaka husika.

Zamda ameeleza kuwa kata hiyo imefanikiwa kuimarisha ulinzi shirikishi kwa kuunganisha mitaa yote, kuviwezesha vikundi vya sungusungu kwa vifaa vya usiku, na kupokea askari Polisi Kata aliye mratibu wa shughuli zote za kiusalama. Polisi Kata huyo pia amekuwa mstari wa mbele katika kuhamasisha uzalendo, uadilifu, na Polisi Jamii hasa kwa vijana na wanafunzi.

HUDUMA ZA JAMII (MAJI, UMEME, MAWASILIANO)

Kama ilivyoelezwa katika Sura ya 3 Ibara ya 77 ukurasa wa 124 wa ilani ya CCM, kata ya Ndala imepiga hatua kubwa katika kuhakikisha huduma bora kwa wananchi wake.

Umeme

Mhe. Zamda amesema Mitaa yote mitano ya Ndala imefikiwa na huduma ya umeme. Miradi iliyotekelezwa ni pamoja na:

·         Ufungaji wa Transfoma mtaa wa Mapinduzi.

·         Ufungaji wa Transfoma na nguzo mtaa wa Mlepa.

·         Usambazaji wa nguzo na uunganishaji wa nyaya maeneo ya Ndala hasa eneo la Visiwani.

Miundombinu ya Barabara, Makalavati na Madaraja

Kwa kipindi cha 2020-2025, jumla ya kilomita 5 za barabara zimechongwa katika mitaa ya Mwabundu, Mlepa na Ndala kwa ufadhili wa Manispaa. Miradi mikubwa ni pamoja na:

·         Ujenzi wa makalavati na mitaro mbalimbali.

·         Ujenzi wa Daraja linalounganisha Ndala na Kambarage kwa gharama ya Tshs 103,252,840.

Jumla ya miradi ya barabara, makalavati na madaraja imegharimu Tshs 440,725,740.

Mawasiliano

Amesema kata ya Ndala ina huduma nzuri ya mawasiliano ya simu na intaneti katika mitaa yote mitano. Hii imesaidia kuongeza kasi ya maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

 Elimu

Kwa mujibu wa Sura ya 3 Ibara ya 79 ya ilani ya CCM, kata ya Ndala diwani huyo amesema imepata mafanikio makubwa katika sekta ya elimu.

·         Idadi ya wanafunzi imeongezeka kwa 100% tangu 2021 hadi 2025 katika Shule ya Msingi Msufini na Ndala Sekondari.

·         Ufaulu umeongezeka hadi 98% mwaka 2024 katika Ndala Sekondari.

·         Motisha kwa walimu na wanafunzi imeendelea kutolewa; walimu walipewa zawadi zenye thamani ya TShs 180,000/=, wanafunzi walizawadiwa sabuni, madaftari na kalamu.

Miradi ya miundombinu ya elimu:

·         Ukamilishaji wa chumba cha maabara ya sayansi: Tshs 30,000,000/= (2021).

·         Ujenzi wa vyumba vya madarasa, matundu ya vyoo, madawati, viti na meza: Tshs 276,120,000/=.

Mhe. Zamda Shaban amewashukuru wananchi wote wa kata ya Ndala kwa ushirikiano, upendo na maombi yao ambayo yamewezesha mafanikio hayo huku akiahidi kuendelea kuwa kiongozi mwaminifu na mtumishi wa watu hadi mwisho wa kipindi chake cha uongozi.

“Ndala ni yetu sote, maendeleo yake yanatuhusu sote. Naendelea kuwahakikishia kuwa tutaendelea kushirikiana na kuhakikisha ilani ya CCM inaendelea kutekelezwa kwa vitendo.”

 


Post a Comment

Previous Post Next Post