Baadhi ya wakazi wa Manispaa ya Shinyanga
waliopoteza makazi yao kufuatia mafuriko ya mvua kubwa iliyoambatana na upepo
mkali mwaka 2024, wameishukuru Compassion Tanzania kwa msaada wa kuwajengea
nyumba mpya kupitia ushirikiano na makanisa saba ya kipentekoste na kiinjili
yaliyoko katika manispaa hiyo.
Wakazi hao, ambao
walikumbwa na athari za moja kwa moja za maafa hayo ya asili, wameeleza kuwa
walijikuta wakikosa mahali pa kuishi, wakilala chini ya turubai huku
wakikabiliwa na changamoto za chakula, usalama na afya.
Hali hiyo iliwaweka katika mazingira ya unyonge kwa
kipindi kirefu hadi pale walipopata msaada kutoka kwa shirika hilo la kimataifa
linalotoa huduma za maendeleo ya mtoto na familia maskini.
Kwa mujibu wa taarifa
rasmi iliyotolewa na viongozi wa Compassion Tanzania, jumla ya nyumba 29
zimejengwa katika kata saba za Manispaa ya Shinyanga, zikiwemo Kolandoto,
Kitangili, Ndala, Masekelo na nyingine, kwa gharama ya shilingi 183,900,292.
Nyumba hizo zimejengwa
kupitia vituo vya huduma kwa mtoto na kijana (Child and Youth Development
Centers) vilivyo chini ya usimamizi wa makanisa saba ambayo ni EAGT Ndala, KKKT
Mjini, Anglican Ndala, Anglikan Mjini, AICT Kitangili, AICT Kolandoto na TAG
Moleka.
Mwenyekiti wa Compassion Tanzania, Lemi Dumbi, amesema mradi huo ni sehemu ya
dhamira ya shirika hilo katika kuimarisha ustawi wa watoto na familia maskini
nchini kwa kuwapatia si tu huduma za afya, elimu na lishe, bali pia mazingira
salama ya kuishi.
“Tunatambua kuwa maendeleo ya mtoto hayawezi
kufikiwa pasipo familia yake kuwa katika mazingira salama. Ndiyo maana tuliona
ni muhimu kuingilia kati kwa vitendo baada ya maafa yale ya mwaka jana,”
amesema Dumbi.
Naye mwenyekiti wa
Klasta ya Shinyanga, Steven Simion,
amesema kazi ya ujenzi wa nyumba hizo ilifanyika kwa hatua na usimamizi wa
karibu wa makanisa yenye vituo vya watoto, huku jamii ikihusishwa katika
utekelezaji ili kuhakikisha uendelevu.
Amesema shirika hilo
limejikita katika kutoa huduma kwa watoto maskini wenye mazingira magumu na
kwamba wanashirikiana na makanisa kama njia ya kuunganisha huduma za kiroho,
kijamii na kimwili kwa mtoto na familia yake.
Katika hafla ya kukabidhi nyumba hizo kwa wanufaika,
mgeni rasmi Said Kitinga, ambaye
alimwakilisha Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga, alilipongeza shirika la Compassion
kwa kazi hiyo ya kijamii na kusema serikali itaendelea kushirikiana na
mashirika yasiyo ya kiserikali yenye nia njema ya kusaidia jamii.
“Tunatambua mchango
mkubwa wa mashirika ya kidini katika kusaidia serikali kutimiza wajibu wake kwa
jamii. Tunapenda kuona zaidi mashirika kama Compassion yakisaidia wananchi wetu
kwa vitendo kama hivi,” amesema Kitinya.
Ameongeza kuwa serikali
ya awamu ya sita imekuwa mstari wa mbele kushirikiana na wadau wote wa
maendeleo na kwamba juhudi za mashirika kama haya zinachangia kufanikisha
malengo ya maendeleo endelevu.
Wakati wa tukio hilo, Askofu wa Kanisa la AICT
Dayosisi ya Shinyanga, Zakayo Bugota,
amewataka viongozi wa dini kuendelea kuwaombea viongozi wa serikali na taifa
kwa ujumla, hasa kuelekea uchaguzi mkuu ujao.
“Tunaliombea taifa letu
liendelee kuwa la amani na mshikamano. Tunatambua kuwa kazi hii ya kujenga
nyumba ni sehemu ya huduma kwa jamii, lakini pia ni njia ya kuonyesha upendo wa
Kristo kwa vitendo,” amesema Askofu Bugota.
Ameongeza kuwa makanisa
yataendelea kushirikiana na serikali katika nyanja mbalimbali, ikiwa ni pamoja
na huduma za kijamii, maadili na malezi bora ya watoto.
Baadhi ya familia zilizonufaika na nyumba hizo
zimesema msaada huo umewarejeshea heshima na matumaini baada ya kipindi kirefu
cha kuhangaika bila makazi maalum.
Wengine wamesema nyumba
hizo zimewawezesha kurudi katika maisha ya kawaida, watoto wao sasa wanapata
muda wa kusoma vizuri na familia zimerudishiwa heshima katika jamii.
Mradi wa ujenzi wa nyumba 29 kwa waathirika wa
mafuriko katika Manispaa ya Shinyanga ni mfano hai wa ushirikiano kati ya
mashirika ya kidini, jamii na serikali katika kusaidia watu walioko katika
mazingira magumu.
Aidha, unatoa somo kuwa
majanga ya asili yanapotokea, kunahitajika mshikamano wa kweli na hatua za
haraka kuwanusuru wahanga badala ya kuachwa kwa muda mrefu bila msaada.
Kwa mujibu wa
Compassion Tanzania, miradi kama hiyo itaendelea kutekelezwa kadri ya uhitaji
na uwezo wa kifedha wa shirika hilo, huku vipaumbele vikiwa kwa watoto, familia
na maeneo yenye changamoto kubwa za kiuchumi na kijamii.

Post a Comment