" SERIKALI YAIPONGEZA TAASISI YA FLAVIANA MATATA KWA KUKABIDHI MRADI WA WASH KATIKA SHULE YA SEKONDARI SALAWE MKOANI SHINYANGA

SERIKALI YAIPONGEZA TAASISI YA FLAVIANA MATATA KWA KUKABIDHI MRADI WA WASH KATIKA SHULE YA SEKONDARI SALAWE MKOANI SHINYANGA

Na Daniel Sibu, Misalaba Media

Taasisi ya Flaviana Matata imekabidhi  mradi wa uboreshaji wa miundombinu ya maji, afya na usafi wa mazingira (WASH) katika Shule ya Sekondari Salawe, mkoani Shinyanga, unaolenga kuboresha mazingira ya kujifunzia kwa wanafunzi, hususan wasichana.

Makabidhiano ya mradi huo yamefanyika Julai 23, 2025 yakiongozwa na mgeni rasmi, Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga, Wakili Julius Mtatiro na kwamba mradi huo umetekelezwa na Taasisi ya Flaviana Matata kwa ufadhili wa shirika la kimataifa la Diamonds Do Good.

Meneja Miradi kutoka Taasisi ya Flaviana Matata, Lineth Masala amesema kupitia mradi huo, shule imenufaika na ujenzi wa matundu 12 ya vyoo vya kisasa, sehemu ya kunawia mikono, chumba maalumu kwa wanafunzi wenye ulemavu, chumba cha wasichana kujisitiri wakati wa hedhi pamoja na sehemu ya kuchomea taka, ikiwemo taulo za kike zilizotumika.

Lineth Masala, amesema taasisi hiyo imekuwa mstari wa mbele kusaidia watoto wa kike kupitia miradi ya elimu, huku lengo likiwa ni kuhakikisha mazingira ya shule yanakuwa salama, safi na yenye staha kwa kila mtoto.

Akizungumza wakati wa hafla ya makabidhiano, Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga, Wakili Julius Mtatiro amesema mradi huo umeonyesha ushirikiano mzuri kati ya taasisi binafsi na serikali katika kuleta maendeleo kwenye sekta ya elimu, huku akisisitiza umuhimu wa kuweka mazingira bora kwa wanafunzi wa kike.

Baadhi ya wanafunzi wa Shule ya Sekondari Salawe akiwemo Maryciana Juma wameeleza furaha yao kwa kupatiwa miundombinu rafiki, hususan chumba cha kujisitiri wakati wa hedhi, wakisema hatua hiyo itawasaidia kuhifadhi utu na kuongeza mahudhurio shuleni.

Kwa mujibu wa uongozi wa shule hiyo, zaidi ya wanafunzi 665 watanufaika moja kwa moja na mradi huo, hatua inayotarajiwa kusaidia kuongeza ufaulu na kuboresha afya ya wanafunzi.Picha ya pamoja.


Post a Comment

Previous Post Next Post