" MWANAUME ADAIWA KUMUUA MKE WAKE NA KUMZIKA KWENYE SHIMO LA CHOO SALAWE SHINYANGA

MWANAUME ADAIWA KUMUUA MKE WAKE NA KUMZIKA KWENYE SHIMO LA CHOO SALAWE SHINYANGA


Na Mapuli Kitina Misalaba

Mwanaume mmoja anayefahamika kwa jina la Chima Majiyanguhi Samamba ambaye anakadiliwa kuwa na umri wa Miaka 52, mkazi wa Songambale Kata ya Salawe Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga, anadaiwa kumpiga mke wake hadi kusababisha kifo kisha kumzika kwenye shimo la choo lililopo pembezoni mwa nyumba yake.

Taarifa za tukio hilo zilianza kusambaa jana jioni baada ya wananchi kutoa taarifa kwa uongozi wa Kijiji ambapo Mwenyekiti wa Kijiji cha Songambele, Bwana Lazaro Enock, akizungumza na Misalaba Media leo Oktoba 8, 2025 amethibitisha kupokea taarifa hizo na kueleza kuwa leo ni siku ya 12 tangu mauaji hayo kufanyika.

Amesema kuwa baada ya kupata taarifa hizo, alichukua hatua za haraka kutoa taarifa kwa viongozi mbalimbali wa serikali pamoja na jeshi la polisi. Kwa mujibu wa Enock, awali jeshi la sungusungu lilimhoji mtuhumiwa ambapo alikanusha kufanya mauaji, lakini baada ya kufikishwa kituo cha polisi alikiri kuwa alimuua mke wake.

“Baada ya mahojiano, polisi walishirikiana na wananchi kufukua mwili wa marehemu, na uchunguzi wa kitabibu umefanyika kabla ya kukabidhi mwili kwa familia kwa ajili ya mazishi,” amesema Enock.

Kwa upande wake, Mtendaji wa Kijiji cha Songambele, Bi Evalina Isack, amekiri kupokea taariza hizo na kwamba leo ameshiriki hatua zote za kufukua mwili huo huku akiwashukuru wananchi kwa kutoa ushirikiano na kutoficha taarifa za tukio hilo.

Ameitaka jamii kuacha kujichukulia sheria mkononi na badala yake kutumia viongozi wa serikali, dini na vyombo vya sheria kutatua migogoro.

“Tunawaomba wananchi kuwa na subira pale wanapokuwa na migogoro. Serikali na vyombo husika vipo kwa ajili ya kutoa suluhisho, siyo kuchukua sheria mikononi,” amesema Evalina.

Mwili wa marehemu, aliyezaliwa mwaka 1978 ambaye hadi sasa angekuwa na miaka 47, umekabidhiwa kwa familia kwa ajili ya mazishi ambayo yanatarajiwa kufanyika leo katika eneo la Ntobo, Halmashauri ya Msalala, Wilaya ya Kahama, mkoani Shinyanga, hata hivyo majina yake bado hayajafahamika rasmi.

Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga, ACP Kennedy Mgani, amesema jeshi la polisi linaendelea na uchunguzi wa tukio hilo, na kwamba taarifa kamili zitatolewa baada ya uchunguzi kukamilika.

 

Post a Comment

Previous Post Next Post