
Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM–TAMISEMI) anayeshughulikia Elimu, Mhe. Reuben Kwagilwa.
OWM-TAMISEMI,Dar es salaam
Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu – Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OWM–TAMISEMI) anayeshughulikia Elimu, Mhe. Reuben Kwagilwa, amemuagiza Mkuu wa Wilaya ya Ilala kuwakamata na kuwahoji Mkandarasi pamoja na Mhandisi Mshauri wa mradi wa ujenzi wa Barabara ya Kitunda–Kivule–Msongola, kufuatia ucheleweshaji usioridhisha wa utekelezaji wa mradi huo.
Agizo hilo limetolewa baada ya Mhe. Kwagilwa kufanya ziara ya ukaguzi wa maendeleo ya ujenzi wa barabara hiyo, unaotekelezwa kwa gharama ya Shilingi bilioni 30.37 na Kampuni ya Jiangxi Geo Engineering Co. Ltd, huku Mhandisi Mshauri wa mradi akiwa ni Mhandisi Consultancy Ltd. Hadi sasa, kiasi cha Shilingi bilioni 4 tayari kimeshalipwa kwa mkandarasi huyo.
Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mhe. Kwagilwa amesema Serikali haitavumilia uzembe wala kutotekelezwa kwa mikataba kwa wakati, akisisitiza kuwa mradi huo ni muhimu kwa ustawi wa wananchi na maendeleo ya Jiji la Dar es Salaam.
“Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI, ninakuelekeza Mkuu wa Wilaya ya Ilala kuhakikisha hawa wahusika wanakamatwa na kuhojiwa mara moja. Wanapaswa kutoa mpango wa utekelezaji wa mradi huu. Hakutakuwa na nyongeza ya muda hata kwa sekunde moja; mwezi wa nne mradi huu lazima uwe umekabidhiwa,” amesema Mhe. Kwagilwa.
Mradi huo unahusisha ujenzi wa barabara ya Kitunda–Kivule–Msongola yenye urefu wa kilomita 9.95 pamoja na barabara ya Kivule–Majohe Junction yenye urefu wa kilomita 2.79, hivyo kufikia jumla ya kilomita 12.74. Utekelezaji wake unafanyika chini ya Mpango wa Maendeleo ya Jiji la Dar es Salaam Awamu ya Pili (DMDP II).
Hadi sasa, utekelezaji wa mradi umefikia asilimia 33 tangu ulipoanza mwezi Januari 2025, huku mkataba ukitarajia kukamilika mwezi Aprili 2026. Pamoja na matarajio makubwa ya mradi huo kuleta unafuu wa usafiri na kuchochea shughuli za kiuchumi kwa wakazi wa maeneo ya Kitunda, Kivule na Msongola, kasi ya utekelezaji imeonekana kutoridhisha na kwenda kinyume na matarajio ya Serikali na wananchi.
Serikali imeeleza kuwa itaendelea kuchukua hatua kali za kisheria na kiutawala kwa wakandarasi na wasimamizi wa miradi wanaokiuka masharti ya mikataba au kuchelewesha utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

🥃🍶 TUMIA VINYWAJI BORA VYA EAST AFRICAN SPIRITS – BEI RAFIKI, LADHA SAFI BILA HARUFU MBAYA
Wasiliana nasi:
📍 East African Spirits (T) Ltd
📞 +255 767 650 806 | +255 652 096 254
Post a Comment