" TANESCO YAIMARISHA USHIRIKIANO NA MADIWANI KISHAPU, YAWASILISHA MIRADI MIKUBWA YA UMEME NA NISHATI SAFI

TANESCO YAIMARISHA USHIRIKIANO NA MADIWANI KISHAPU, YAWASILISHA MIRADI MIKUBWA YA UMEME NA NISHATI SAFI

 

Kishapu, Shinyanga

Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) leo limekutana na Baraza la Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu, ambapo limewasilisha taarifa ya utekelezaji wa miradi mikubwa ya kimkakati ya umeme na nishati safi, inayolenga kuimarisha upatikanaji wa umeme wa uhakika, kuimarisha Gridi ya Taifa na kuchochea maendeleo ya kiuchumi kwa wananchi wa Kishapu na Mkoa wa Shinyanga kwa ujumla.

Katika kikao hicho, TANESCO ilieleza kuwa inaendelea kutekeleza miradi ya kimkakati katika maeneo mbalimbali ya nchi, ikiwemo Mkoa wa Shinyanga, ikiwa ni sehemu ya jitihada za Serikali kuhakikisha umeme wa uhakika kwa maendeleo ya wananchi.

Mradi Mkubwa wa Umeme wa Jua Ngunga Wakaribia Kukamilika

Moja ya miradi mikubwa iliyowasilishwa ni mradi wa kuzalisha umeme kwa kutumia nishati ya jua unaotekelezwa katika eneo la Ngunga, Wilaya ya Kishapu, wenye uwezo wa kuzalisha Megawati 150.

Mradi huu unatekelezwa kwa awamu mbili, ambapo awamu ya kwanza ya Megawati 50 ilianza Desemba 2023 na unatarajiwa kukamilika Machi 2026 kwa gharama ya Shilingi Bilioni 323. Hadi sasa, mradi umefikia asilimia 92.6 ya utekelezaji, na hatua za mwisho zinaendelea ili kuanza kuingiza umeme kwenye Gridi ya Taifa.

TANESCO ilieleza kuwa mradi huu utakuwa na mchango mkubwa katika kuongeza uzalishaji wa umeme, kuimarisha Gridi ya Taifa na kuhakikisha Kanda ya Ziwa inapata umeme wa uhakika zaidi.

Upanuzi wa Kituo cha Ibadakuli Kuleta Umeme wa Uhakika

TANESCO pia ilieleza kuhusu mradi wa upanuzi wa Kituo cha Umeme cha Ibadakuli, ambacho kwa sasa kina uwezo wa Megawati 296.

Kupitia mradi huu, transfoma mpya zinafungwa ili kuongeza uwezo wa kituo na kuimarisha usambazaji wa umeme. Mradi huu unatekelezwa kwa gharama ya Dola za Kimarekani Milioni 46.7, na umefikia asilimia 46.8 ya utekelezaji. Unatarajiwa kukamilika Desemba 2026.

Mradi huu utasaidia kuondoa changamoto za kukatika kwa umeme na kufungua fursa mpya za uwekezaji na shughuli za kiuchumi katika Kishapu na maeneo ya jirani.

Vitongoji 15 Kishapu Vyanufaika na Umeme

Katika hatua nyingine, TANESCO ilieleza kuwa mradi wa kufikisha umeme katika vitongoji 15 vya Jimbo la Kishapu tayari umeleta matokeo chanya.

Mkandarasi amekamilisha ujenzi wa miundombinu, ambapo:

Wateja 176 tayari wameunganishwa na umeme

Mradi umetumia zaidi ya Shilingi Bilioni 11.118

Baadhi ya vitongoji vilivyonufaika ni Buganika (Idukilo), Itilima, Nzanza, Igalukilo pamoja na vitongoji vingine, jumla vikiwa 15.

Shinyanga Yapata Vitongoji 581 Kupata Umeme

Habari njema zaidi ni kuwa Mkoa wa Shinyanga umepata mradi mwingine mkubwa wa kufikisha umeme katika vitongoji 581 ndani ya majimbo mbalimbali.

Mgawanyo wa vitongoji hivyo ni kama ifuatavyo:

Shinyanga Mjini – 20, Itwangi – 63, Solwa – 49, Msalala – 96, Kahama – 61, Ushetu – 136, Kishapu – 154

Mradi huu tayari mkandarasi amesaini mkataba na utatekelezwa kwa gharama ya Shilingi Bilioni 60, huku TANESCO ikisisitiza kuwa viongozi wa maeneo husika watashirikishwa kikamilifu katika utekelezaji.

Madiwani Wakumbushwa Kulinda Miundombinu ya Umeme

Meneja wa Wilaya ya Kishapu, Mhandisi Hussein Mbulu, aliwakumbusha madiwani na wananchi kwa ujumla kuwa miundombinu ya TANESCO ni mali ya umma, hivyo inapaswa kulindwa.

Alisisitiza umuhimu wa kulinda transfoma na nyaya za shaba, na kutoa wito kwa wananchi kutoa taarifa mara moja pale vitendo vya uharibifu vinapotokea.

Nishati Safi ya Kupikia Yapewa Kipaumbele

Afisa Uhusiano na Huduma kwa Wateja TANESCO, Emma Nyaki, alitumia kikao hicho kutoa elimu juu ya Agenda ya Kitaifa ya Nishati Safi ya Kupikia, akisisitiza umuhimu wa kuachana na nishati chafu na kuhamia kwenye matumizi ya majiko janja.

Alieleza kuwa majiko hayo yanaokoa muda, ni salama, na ni nafuu, ambapo mtu anaweza kupika wali au ugali kwa chini ya unit 350, huku yakisaidia kulinda afya na mazingira.

Madiwani walionesha kuridhishwa na elimu hiyo na kukubali kuwa mabalozi wa nishati safi ya kupikia katika Jimbo la Kishapu.

Mhandisi mwandamizi wa TANESCO Mkoa wa Shinyanga Anthony Tarimo, akizungumza.

Meneja wa TANESCO Wilaya ya Kishapu, Mhandisi Hussein Mbulu, akizungumza.Afisa Uhusiano na Huduma kwa Wateja TANESCO, Emma Nyaki, akizungumza.





 

  • Wasiliana nasi:
    📍 East African Spirits (T) Ltd
    📞 +255 767 650 806 | +255 652 096 254

 

Post a Comment

Previous Post Next Post