Jeshi la Polisi Mkoa wa Shinyanga limewakamata
watuhumiwa wawili, Kisaka Elinihaki (22) na Makoye James, kwa tuhuma za
kusambaza taarifa za uongo kuhusu kupoteza sehemu zao za siri, jambo
lililosababisha taharuki kubwa kwa wananchi katika Wilaya ya Kahama.
Taarifa hiyo imetolewa leo, Aprili 7, 2026, na Kamanda
wa Polisi Mkoa wa Shinyanga, ACP Janeth Magomi, alipokuwa akizungumza na
waandishi wa habari ofisini kwake.
Kwa mujibu wa Kamanda Magomi, tukio la kwanza
lilitokea Aprili 4, 2026 katika Soko Kuu lililopo eneo la Stendi Kuu ya Mabasi,
Kata ya Kahama Mjini. Katika tukio hilo, Kisaka Elinihaki, mkazi wa Majengo,
alidai kupoteza sehemu zake za siri kimiujiza baada ya kuguswa bega la kushoto
na dereva aitwaye Joseph Godfrey (36), mkazi wa Shunu.
Amesema madai hayo ya uongo yalisababisha taharuki
kubwa miongoni mwa wananchi waliokuwepo eneo hilo, ambapo baadhi yao walichukua
sheria mkononi na kuanza kumshambulia Joseph Godfrey wakimtuhumu kuhusika na
tukio hilo.
Hata hivyo, Jeshi la Polisi lilifika kwa wakati na
kufanikiwa kumwokoa mtuhumiwa huyo pamoja na kumchukua Kisaka kwa ajili ya
uchunguzi zaidi.
Aidha, tukio la pili lilitokea Aprili 6, 2026 katika
eneo la machimbo ya dhahabu Mwime, wilayani Kahama, ambapo kijana aitwaye
Makoye James alitoa taarifa ya uongo akidai kupoteza sehemu zake za siri baada
ya kushikwa na abiria mwenzake alipokuwa akisafiri kwa pikipiki.
Kamanda Magomi ameeleza kuwa tukio hilo pia lilizua
taharuki na kusababisha mkusanyiko wa wananchi wenye hasira waliokuwa wakitaka
kumshambulia mtu aliyekuwa akituhumiwa, kabla ya polisi kufika na kudhibiti
hali hiyo.
Ameongeza kuwa uchunguzi wa kitabibu uliofanyika
katika Hospitali ya Wilaya ya Kahama ulithibitisha kuwa mhusika hakuwa na
tatizo lolote, hivyo kuthibitisha kuwa taarifa aliyotoa ilikuwa ya uongo.
Mtuhumiwa huyo naye amekamatwa na hatua za kisheria zinaendelea kuchukuliwa
dhidi yake.
Kamanda Magomi ameonya kuwa vitendo vya kusambaza
taarifa za uongo vina madhara makubwa kwa jamii, ikiwa ni pamoja na kusababisha
uvunjifu wa amani, kuwadhuru watu wasio na hatia na hata kuhatarisha maisha.
Ametoa wito kwa wananchi kuacha tabia ya kuzua taarifa
zisizo na ukweli na badala yake kushirikiana na vyombo vya dola katika
kudumisha amani na usalama.
Jeshi la Polisi Mkoa wa Shinyanga limeeleza kuwa
halitasita kuchukua hatua kali za kisheria dhidi ya mtu yeyote atakayebainika
kusambaza taarifa za uongo zinazoweza kuhatarisha usalama wa jamii.
SHY TALENT FILMS - CONTENT YA MWISHO DRAMA
🥃🍶 TUMIA VINYWAJI BORA VYA KAMPUNI YA EAST AFRICAN SPIRITS – BEI RAFIKI, LADHA SAFI BILA HARUFU MBAYA
Wasiliana nasi:
📍 East African Spirits (T) Ltd
📞 +255 767 650 806 | +255 652 096 254

Post a Comment