Na
Mapuli Kitina Misalaba, Shinyanga
Licha ya kuwepo kwa sheria, kanuni na
mifumo ya usimamizi wa sekta ya madini nchini, simulizi kutoka migodi ya
wachimbaji wadogo mkoani Shinyanga zinaonyesha taswira tofauti—usalama bado ni
kitendawili kisichopata majibu.
Katikati ya hali hiyo, sauti ya mtaalamu
wa jiolojia, James Kibiti Muiko, inajitokeza ikiweka wazi kuwa tatizo si
ukosefu wa sheria bali utekelezaji wake. Kibiti kwa mtazamo wake, changamoto si
ukosefu wa sheria bali ni pengo kati ya sheria na utekelezaji wake. Ni pengo
linalogharimu maisha.
“Hatua za awali za utoaji leseni hufuata
taratibu zote, lakini matatizo huanza mara uchimbaji unapoanza na usimamizi
kuwa dhaifu,” anasema Kibiti ambaye ni Mjiolojia kutoka Ofisi ya Ofisa Madini
Mkazi, Shinyanga
Ripoti ya Tume ya Madini nchini (TMC) ya
mwaka 2023/24 inaonyesha kuwa
kutokufuatwa sheria za madini ni changamoto kubwa kiasi cha kuilazimisha tume
hiyo kutoa notisi za ukiukwaji na hata kufuta leseni za wahusika mara kwa mara.
Sheria zinazotazamwa kusimamia usalama
wa wachimbaji wadogo ni ile ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi ya mwaka 2003
(OSHA) na Sheria ya Madini ya mwaka 2010, lakini bado kuna udhaifu katika
kusimamia na kulinda usalama wa wachimbaji hao.
Ingawa sheria hizi zimekusudiwa kuweka
misingi ya usalama kazini na katika shughuli za uchimbaji, uhalisia unaonyesha
kuwa hazijitoshelezi kukidhi mazingira halisi ya uchimbaji mdogo (ASM), ambao
kwa kiasi kikubwa ni sekta isiyo rasmi, yenye rasilimali chache, na
inayofanyika nje ya mifumo madhubuti ya kisheria.
Kwa ujumla, udhaifu wa sheria hizi mbili
unatokana na kutolingana na hali halisi ya uchimbaji mdogo, ukosefu wa masharti
mahsusi ya usalama, utegemezi wa kanuni zisizo wazi, pamoja na changamoto za
utekelezaji.
Matokeo yake wachimbaji wadogo nchini
Tanzania wanaendelea kufanya kazi katika mazingira hatarishi, wakikosa ulinzi
madhubuti wa kisheria licha ya uwepo wa sheria hizo.
Mwenendo
wa ajali
Takwimu zinaonysha kuwa katika kipindi
cha miaka mitatu kuanzia 2022 hadi 2025, watu 72 waliathirika na ajali migodini
katika maeneo ya Nyandolwa na Mwakitolyo; kati yao 36 walifariki dunia. Ajali
ya Agosti 11, 2025 pekee iligharimu maisha ya watu 21 kati ya 25
waliohusika—siku ambayo kwa wengi ilibadili “miduara” kuwa makaburi ya wazi.
Kwa mujibu wa Kibiti, moja ya vyanzo
vikuu vya ajali ni “miduara”—mashimo ya uchimbaji chini ya ardhi. “Mara nyingi
huchimbwa pasipo utaalam, hali inayosababisha mtikisiko na maporomoko ya
ghafla,” anaeleza. Tofauti na migodi mikubwa, wachimbaji wadogo huchimba kwa
ukaribu mkubwa, jambo linaloongeza hatari ya miundombinu kuingiliana chini kwa
chini bila udhibiti.
Hatari hii huongezeka zaidi kutokana na
uwepo wa kundi linalojulikana kama “manyani”—watu wanaoingia kwenye miduara
iliyofungwa kwa ukarabati wakisaka mabaki ya madini. Ni taswira ya kukata
tamaa; uchumi wa kuungaunga unaowasukuma watu kwenye hatari iliyo wazi.
Hata hivyo ripoti ya TMC ya 2023/24
inabainisha kutokuwepo kwa takwimu za kina kuhusu ajali, huku kukiwa hakuna
idadi rasmi ya vifo, majeruhi, wala aina za ajali. Kwa wataalamu, hili ni pengo
linalodhoofisha uwezo wa kupanga sera za usalama.
Hali hiyo inathibitshwa na baadhi ya
viongozi wa vijiji ambao wanakiri kuwepo kwa utamaduni wa kufumbia macho ajali.
Mwenyekiti wa Kijiji cha Nyandolwa, Mange Didas, anasema, “Vifo vya mtu mmoja
au wawili mara nyingi haviripotiwi.” Hali hii inaficha ukubwa wa tatizo na
kuchelewesha hatua.
Sababu za ajali
Taarifa ya Tume ya Madini nchini (TMC) kwa
mwaka unaoishia Juni 30, 2024 unabainisha kuwa miongoni mwa visababishi vya
ajali katika migodi ya wachimbaji wadogo wa madini ni kuporomoka kwa migodi,
ukosefu wa miundombinu salama ya uchimbaji, matumizi ya zana duni au za
kienyeji, pamoja na kukosekana kwa mifumo ya uingizaji hewa.
“Teknolojia
nayo ni changamoto. Wachimbaji wengi bado wanatumia mbinu za jadi na vifaa
visivyo salama—hali inayoongeza uwezekano wa ajali,” inasomeka sehemu ya ripoti
hiyo ya mwaka unaoishia Juni 30, 2024.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo, katika migodi
mingi ya wachimbaji wadogo hakuna vifaa kinga (kama chepeo/helmeti na buti),
wala mfumo thabiti wa ukaguzi wa mara kwa mara. Hali hii inaacha wachimbaji
wakifanya kazi katika mazingira yasiyo na ulinzi.
Hali hii inathibitishwa na baadhi ya
wachimbaji wadogo wa madini katika migodi ya Nyandolwa na Mwakitolyo Halmashauri
ya Wilaya ya Shinyanga, ambao mbali na kutokuwa na vifaa vya usalama, pia
wamekuwa wakiingia migodini bila kupata mafunzo stahiki.
Miongoni mwao ni Boniface Misong’oni
ambaye anasema vifaa vya kujikinga vinapotolewa, hakuna mwongozo wa matumizi
yake. “Unapewa vifaa, lakini hakuna anayekuonyesha jinsi ya kuvitumia
ipasavyo,” anasema.
Hata hivyo Clement Samson anasema baadhi ya wachimbaji huwa hawazingatii a matumizi ya vifaa vya kujikinga, hali inayoongeza hatari.
Naye Mpiga Mhamal anaeleza kuwa
wanapokuja wachimbaji wapya mara nyingi huulizwa iwapo ana uzoefu na akijibu
ndiyo, huruhusiwa kuanza kazi mara moja. “Ukosefu wa mafunzo ya awali
unasababisha wachimbaji kufanya kazi kwa tahadhari ndogo,” anasisitiza.
Kwa upande wa wanawake, hali si tofauti.
Christina Shija na Stella Jemes wanaojihusisha na ubondaji wa mawe ya
dhahabu, wanasema wanategemea mbinu za jadi kujilinda. “Hatupati mafunzo rasmi
ya usalama,” wanasisitiza, wakieleza kuwa ajali ndogondogo huathiri afya zao na
kipato cha familia.
Mwingine ni Kulwa Mpelwa ambaye anasema: “Naingia ndani ya duara nikitegemea
nilichojifunza kwa wenzangu.” Kauli hii inaonyesha pengo kubwa la mafunzo rasmi
ya usalama kwa wachimbaji.
Kandya Ndutu yeye anaongeza kwa kusema,
“Elimu ya usalama haipatikani, tunajifunza kwa majaribio na makosa.”
Udhaifu wa Sheria ya OSHA
Sheria ya OSHA ya mwaka 2003
inazungumzia mazingira rasmi ya kazi yenye muundo wa mwajiri na mwajiriwa. Hali
hii haipo katika uchimbaji mdogo ambapo wachimbaji wengi hujiajiri au kufanya
kazi katika vikundi visivyo rasmi.
Kutokana na hilo, vifungu muhimu vya
sheria vinavyohusu wajibu wa mwajiri, usimamizi wa usalama, na uwajibikaji
vinashindwa kutekelezwa kwa vitendo. Pia sheria inalazimisha usajili rasmi na
ukaguzi wa mara kwa mara, jambo ambalo wachimbaji wadogo wengi hawawezi
kulimudu kutokana na gharama na urasimu, hali inayowasukuma kufanya kazi nje ya
mfumo wa kisheria.
Kadhalika matakwa yanayowekwa na sheria
hiyo kama matumizi ya mitambo iliyothibitishwa, uwepo wa wataalamu wa afya
kazini, na ukaguzi maalum ni kama mfupa mgumu kutafunwa kwa kundi hili la
wachimbaji wadogo, hivyo kuifanya sheria ionekane kuwa ya kinadharia zaidi
kuliko ya vitendo, hasa katika muktadha wa ASM.
Hata pale ambapo sheria inatoa masharti
muhimu ya usalama kama vile matumizi ya vifaa kinga, huduma ya kwanza, na
udhibiti wa hatari, utekelezaji wake unakuwa hafifu kutokana na ukosefu wa
ufuatiliaji na hofu ya wachimbaji kuripoti ajali kwa kuhofia adhabu.
Ukaguzi wa usalama
Uchunguzi wa Misalaba Media pia ulibaini
udhaifu wa ukaguzi wa usalama katika migodi, kabla ya kutumia.
Mwenyekiti wa Kijiji cha Nyandolwa,
Mange Didas, anasema, ukaguzi wa mara kwa mara haupo. “Wakaguzi wanapaswa
kufanya kazi mara kwa mara, lakini wengi hawalipwi au hawafanyi kazi ipasavyo.”
Naye Nuhi Shomi, Mwenyekiti wa Kijiji
cha Mwakitolyo, anaeleza kuwa maofisa wa madini hufika mara chache na wakati
mwingine hawashuki kabisa kwenye miduara. “Usimamizi unakuwa wa juu juu,”
anasema.
Hata hivyo wakaguzi wa migodi nao
wanajitetea, wakisema nao hawawezeshwi kufanya kazi zao ipasavyo nakwamba mafunzo
wanayopata hayatoshi.
“Tunapatiwa mafunzo mara moja kwa mwaka,
hayatoshelezi,” anasema mmoja wa wakaguzi Samson Jelemiah huku mwezake Dotto
Seleman akiongeza kuwa hata taarifa wanazotoa huwa hazifanyiwi kazi kwa wakati.
Hata hivyo Sheria ya Madini ya mwaka
2010, licha ya leseni za uchimbaji mdogo (PML), haijaweka masharti ya moja kwa
moja yanayolenga usalama wa wachimbaji hao. Badala yake, inatoa marejeo ya
jumla tu kwa kanuni nyingine zisizobainishwa wazi, hali inayosababisha ukosefu
wa mwongozo thabiti wa usalama.
Aidha, sheria haielezi wazi wajibu wa
wachimbaji au mamlaka husika katika kuhakikisha mazingira salama ya kazi, wala
haiweki masharti ya lazima kuhusu mafunzo ya usalama, matumizi ya vifaa kinga,
au utaratibu wa kuripoti ajali. Upungufu huo unaacha pengo la kisheria
linalowaacha wachimbaji wadogo katika hatari bila ulinzi wa kutosha.
Hata nafasi ya Mkaguzi Mkuu wa Migodi,
ingawa ipo kisheria, haijapewa mamlaka ya moja kwa moja ya kusimamia na
kutekeleza masuala ya usalama kwa wachimbaji wadogo, hivyo kuwapo umuhimu wa
sheria hiyo kurejewa.
Mwisho
SHY TALENT FILMS - CONTENT YA MWISHO DRAMA
🥃🍶 TUMIA VINYWAJI BORA VYA KAMPUNI YA EAST AFRICAN SPIRITS – BEI RAFIKI, LADHA SAFI BILA HARUFU MBAYA
Wasiliana nasi:
📍 East African Spirits (T) Ltd
📞 +255 767 650 806 | +255 652 096 254


Post a Comment