" TAASISI YA JOSEPH MUHUNDA NYERERE FOUNDATION YAPANDA MITI HOSPITALI YA RUFAA YA MKOA WA SHINYANGA KUADHIMISHA SIKU YA MUUNGANO

TAASISI YA JOSEPH MUHUNDA NYERERE FOUNDATION YAPANDA MITI HOSPITALI YA RUFAA YA MKOA WA SHINYANGA KUADHIMISHA SIKU YA MUUNGANO

Na Mapuli Kitina Misalaba

Katika kuadhimisha Siku ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, Taasisi ya Joseph Muhunda Nyerere Foundation leo Aprili 26, 2026 imeendesha zoezi la upandaji miti katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga, ikiwa ni sehemu ya kuhamasisha utunzaji wa mazingira na kuenzi umoja wa kitaifa.

Akizungumza wakati wa tukio hilo, Mkurugenzi wa Taasisi hiyo, Joseph Muhunda Nyerere, amesema kuwa maadhimisho ya Muungano yanapaswa kwenda sambamba na vitendo vinavyogusa maisha ya wananchi, ikiwemo kulinda mazingira kwa manufaa ya kizazi cha sasa na kijacho.

Ameeleza kuwa upandaji miti ni njia mojawapo ya kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi na kuboresha afya ya jamii.

Kwa upande wake, Mratibu wa Taasisi hiyo katika Manispaa ya Shinyanga, Mwalimu Leonard Mapolu, amesema taasisi hiyo imekuwa mstari wa mbele katika kuendesha kampeni za mazingira, hususan upandaji miti, na kwamba wataendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kuhakikisha mji wa Shinyanga unakuwa wa kijani na salama kiafya.

Naye Mratibu mwingine wa Taasisi hiyo, Abdalah Sube, amesisitiza umuhimu wa jamii kushiriki kikamilifu katika uhifadhi wa mazingira, akibainisha kuwa juhudi za pamoja ndizo zitakazosaidia kufikia malengo ya maendeleo endelevu.

Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga, Dkt. Luzila John, ameishukuru taasisi hiyo kwa kuchagua hospitali hiyo kama eneo la zoezi hilo, akieleza kuwa miti hiyo itasaidia kuboresha mazingira ya hospitali na kutoa hewa safi kwa wagonjwa na watumishi wa afya. Dkt. Luzila pia alishiriki kikamilifu katika zoezi la upandaji miti.

Aidha, Mwenyekiti wa Baraza la Wazee la Manispaa ya Shinyanga, ambaye alikuwa miongoni mwa mashuhuda wa Muungano, alitoa simulizi ya kihistoria akieleza kuwa wakati Muungano unapatikana alikuwa na umri wa takribani miaka 10 ambapo amesema amani iliyojengwa tangu wakati huo imekuwa nguzo muhimu ya kuudumisha Muungano na maendeleo ya Taifa.

Taasisi ya Joseph Muhunda Nyerere Foundation imeendelea kujikita katika masuala ya uhifadhi wa mazingira nchini, ikiwa ni pamoja na kushiriki shughuli mbalimbali za kijamii.

Zoezi la upandaji miti limekuwa ni miongoni mwa vipaumbele vyake, hasa katika Manispaa ya Shinyanga, likilenga kuongeza uelewa na kuwahamasisha wananchi kushiriki katika utunzaji wa mazingira.




 SHY TALENT FILMS - CONTENT YA MWISHO DRAMA

🥃🍶 TUMIA VINYWAJI BORA VYA KAMPUNI YA EAST AFRICAN SPIRITS – BEI RAFIKI, LADHA SAFI BILA HARUFU MBAYA

  • Wasiliana nasi:
    📍 East African Spirits (T) Ltd
    📞 +255 767 650 806 | +255 652 096 254

Post a Comment

Previous Post Next Post