Amani ni msingi wa ustawi wa taifa lolote. Bila amani,
haki nyingine zote za msingi hupoteza maana yake. Hii ndiyo taswira
inayojitokeza wazi kupitia ripoti ya uchunguzi kuhusu matukio ya uvunjifu wa
amani yaliyotokea wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025 nchini
Tanzania. Ripoti hiyo inaweka bayana tofauti kati ya maandamano ya amani
yanayotambuliwa kisheria na vitendo vya ghasia vilivyoshuhudiwa siku hiyo.
Kisheria, haki ya kuandamana ipo na inalindwa na
Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977, hususan kupitia Ibara
ya 18 na 20. Hata hivyo, haki hiyo ina mipaka yake, ikiwemo sharti la
maandamano kuwa ya amani pamoja na kutoa taarifa (notisi) kwa mamlaka husika,
kwa mujibu wa Sheria ya Jeshi la Polisi na Huduma Saidizi. Kwa mujibu wa ripoti
hiyo, matukio ya Oktoba 29 hayakuzingatia masharti hayo, jambo lililoondoa
uhalali wake kisheria.
Zaidi ya hapo, haki ya kushiriki uchaguzi kama mpiga
kura au mgombea ni haki ya kikatiba inayolindwa na Ibara ya 5. Hivyo basi,
kufanya vurugu siku ya uchaguzi kulikuwa ni kuvunja haki za wananchi wengine
waliotaka kushiriki katika mchakato huo wa kidemokrasia kwa amani. Badala ya
kuwa jukwaa la kutoa maoni kwa njia halali, matukio hayo yaligeuka kuwa kikwazo
kwa haki za wengine.
Mwenyekiti wa Tume ya Rais ya Kuchunguza Matukio ya
Uvunjifu wa Amani wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba, 2025, Jaji Mkuu
Mstaafu Mhe. Mohamed Chande Othman wakati akisoma Muhtasari wa Ripoti ya Tume
hiyo, Ikulu Jijini Dar es Salaam, tarehe 23, Aprili, 2026 amesema washiriki wa
matukio hayo hawakuwa waandamanaji wa amani, bali walihusika katika vitendo vya
ghasia huku wakiwa wamebeba silaha mbalimbali zikiwemo mawe, nondo, mapanga,
visu, pamoja na vifaa hatarishi kama vilipuzi na bunduki. Hali hii ni kinyume
kabisa na sheria za kitaifa na mikataba ya kimataifa inayoruhusu maandamano ya
amani yasiyo na silaha wala vitendo vya taharuki.
Kwa mujibu wa viwango vya kimataifa, ikiwemo Mkataba
wa Kimataifa wa Haki za Kiraia na Kisiasa wa mwaka 1966 na Mkataba wa Afrika wa
Haki za Watu na Binadamu wa mwaka 1981, maandamano yanapaswa kuwa ya amani,
yasiyohatarisha maisha ya watu wala kusababisha uharibifu wa mali. Ripoti
inaonyesha kuwa matukio ya Oktoba 29 yalikiuka misingi hiyo kwa kusababisha
hofu, uharibifu wa mali za umma na binafsi pamoja na kuhatarisha usalama wa
wananchi.
Uchunguzi zaidi umebaini kuwa matukio hayo hayakuwa ya
bahati mbaya, bali yalipangwa, kuratibiwa na hata kufadhiliwa. Waratibu
walitumia mbinu mbalimbali kuwashawishi watu kushiriki, wakiwalenga zaidi
vijana, waendesha bodaboda, watoto wanaoishi katika mazingira magumu na
wajasiriamali wadogo. Wengine walipewa fedha kidogo kuanzia shilingi elfu 10
hadi elfu 50 au kuahidiwa ajira na maisha bora, jambo lililosababisha baadhi
yao kushiriki bila kuelewa madhumuni halisi ya matukio hayo.
Aidha, ilibainika kuwa wahusika wakuu hawakuwepo
katika maeneo ya matukio, huku waliokamatwa wengi wakiwa ni wananchi wa kawaida
waliovutwa au kushawishiwa kushiriki. Mbinu zilizotumika zilijumuisha kuweka
vizuizi barabarani, kuchoma moto mali, kutumia pikipiki kusambaza vurugu na
kuanzisha matukio katika maeneo mengi kwa wakati mmoja ili kuvuruga mifumo ya
usalama.
Matokeo ya ghasia hizo yalikuwa makubwa na ya
kusikitisha. Tume ilibaini kuwa jumla ya watu 518 walipoteza maisha, wengi wao
wakiwa raia wa kawaida. Vifo vingi vilitokana na majeraha makubwa, ikiwemo
kupigwa risasi, kupoteza damu nyingi na kujeruhiwa sehemu mbalimbali za mwili.
Hali hii imeacha maumivu makubwa kwa familia na jamii, huku pia ikipunguza
nguvu kazi ya taifa.
Mbali na vifo, ripoti pia inaonyesha uwepo wa madai ya
ukiukwaji wa haki za binadamu, ikiwemo matumizi ya nguvu kupita kiasi katika
baadhi ya maeneo ambayo hayakuwa na vurugu. Haya ni masuala nyeti yanayohitaji
uchunguzi wa kina ili kuhakikisha haki inatendeka kwa pande zote.
Katika enzi ya teknolojia, ripoti pia imebaini kuwa
baadhi ya picha na video zilizosambazwa mitandaoni zilikuwa si za kweli, bali
zilitengenezwa au kuhaririwa kwa kutumia teknolojia ya akiliunde (AI) ili
kupotosha umma. Hali hii inaonyesha umuhimu wa wananchi kuwa makini na taarifa
wanazopokea na kuzisambaza.
Kwa ujumla, hitimisho la Tume ni wazi kuwa matukio ya
Oktoba 29, 2025 hayakuwa maandamano ya amani, bali yalikuwa ghasia zilizokiuka
sheria za kitaifa na viwango vya kimataifa. Hivyo, hayapaswi kulindwa chini ya
haki ya maandamano ya amani.
Somo kubwa linalopatikana ni kwamba amani ni jukumu la
kila mmoja. Wananchi wanapaswa kuwa waangalifu dhidi ya ushawishi unaoweza
kuwapelekea kushiriki vitendo vya vurugu, huku wakilinda haki zao kwa njia
halali na za kisheria. Vilevile, kuna umuhimu wa kuendelea kuimarisha mifumo ya
haki, uwajibikaji na elimu kwa umma ili kuepuka kurudia matukio kama haya.
Mwisho, wito wa maridhiano, umoja na mshikamano ni muhimu zaidi sasa kuliko wakati mwingine wowote. Taifa linahitaji kujifunza kutoka yaliyopita na kusonga mbele kwa pamoja, likilinda amani kama tunu kuu ya maendeleo na ustawi wa kizazi cha sasa na kijacho.





SHY TALENT FILMS - CONTENT YA MWISHO DRAMA
🥃🍶 TUMIA VINYWAJI BORA VYA KAMPUNI YA EAST AFRICAN SPIRITS – BEI RAFIKI, LADHA SAFI BILA HARUFU MBAYA
Wasiliana nasi:
📍 East African Spirits (T) Ltd
📞 +255 767 650 806 | +255 652 096 254






Post a Comment