" WAZAZI NA WALEZI WATAKIWA KUIMARISHA MALEZI YA WATOTO KULINDA MAADILI YA JAMII

WAZAZI NA WALEZI WATAKIWA KUIMARISHA MALEZI YA WATOTO KULINDA MAADILI YA JAMII

Na Edington Mukiza Ezron, Misalaba Media

Baadhi ya wananchi katika Manispaa ya Shinyanga wamewataka wazazi na walezi kuzingatia malezi bora kwa watoto wao kwa kuwajenga katika misingi ya maadili ya Kitanzania ili kulinda heshima ya jamii na taifa kwa ujumla.

Wakizungumza na Misalaba Media leo Mei 5, 2026, wananchi hao wamesema baadhi ya wazazi wamekuwa wakilegeza usimamizi wa watoto wao, hali inayochangia kuporomoka kwa maadili miongoni mwa vijana.

Mzee Aley Juma amesema mmomonyoko wa maadili kwa vijana unachangiwa na baadhi ya wazazi kufanya vitendo visivyofaa mbele ya watoto wao, jambo linalowafanya watoto kuiga tabia hizo wanazoziona katika mazingira yao ya nyumbani.

Aidha, wananchi hao wameeleza kuwa ukosefu wa mbinu madhubuti za kukemea vitendo visivyofaa katika jamii umechangia vijana wengi kuendelea kufanya mambo yanayokiuka maadili ya Kitanzania.

Pia wamebainisha kuwa baadhi ya filamu, picha na maudhui kutoka tamaduni za kigeni, ikiwemo mavazi yasiyoendana na maadili ya jamii, vimekuwa na athari kwa watoto na vijana, hasa kutokana na matumizi ya simu na mitandao ya kijamii katika umri mdogo.

Wameongeza kuwa tamaa ya mali na maisha ya kifahari imewafanya baadhi ya watoto na vijana kujiingiza katika vitendo visivyofaa kimaadili ikiwemo ukahaba, hali inayohitaji juhudi za pamoja kutoka kwa wazazi, jamii na serikali.

Hata hivyo, wananchi hao wameiomba serikali kuweka mikakati madhubuti ya kulinda maadili ya taifa pamoja na kuchukua hatua kali dhidi ya watu wanaojihusisha na vitendo vinavyokiuka maadili ya jamii.

 

Post a Comment

Previous Post Next Post