" COMMUNITY DEVELOPMENT YATWAA UBINGWA WA INTERCLASS CSGM SHINYANGA, YAICHAPA FINANCE 4-0 MBELE YA MGENI RASMI SAMWEL JACKSON

COMMUNITY DEVELOPMENT YATWAA UBINGWA WA INTERCLASS CSGM SHINYANGA, YAICHAPA FINANCE 4-0 MBELE YA MGENI RASMI SAMWEL JACKSON



Timu ya Community Development imeibuka bingwa wa mashindano ya Interclass katika Chuo cha Serikali za Mitaa (CSGM) Kampasi ya Shinyanga baada ya kuichapa Finance mabao 4-0 katika mchezo wa fainali uliochezwa kwa ushindani mkubwa.

Fainali hiyo ilihudhuriwa na mgeni rasmi Samwel Jackson, Katibu wa Mbunge wa Jimbo la Shinyanga Mjini, ambaye aliwapongeza wanafunzi kwa kujitokeza kushiriki michezo na kudumisha umoja, ushirikiano na nidhamu kupitia mashindano hayo.

Akizungumza katika hafla ya kufunga mashindano hayo, Samwel Jackson alisema michezo ni nyenzo muhimu ya kujenga afya, kuibua vipaji na kuwaunganisha vijana, huku akiwataka wanafunzi kuendelea kutumia michezo kama sehemu ya kujenga mahusiano mema na kujiandaa kwa majukumu ya maendeleo ya jamii.

Katika mchezo huo wa fainali, Community Development ilionyesha ubora mkubwa uwanjani kwa kutawala mchezo na kufanikiwa kuibuka na ushindi mnono wa mabao manne bila majibu dhidi ya Finance, matokeo yaliyoiwezesha kutwaa ubingwa wa mashindano hayo ya Interclass.

Mashindano hayo yaliyoandaliwa kwa ushirikiano wa Wizara ya Habari na Wizara ya Michezo ndani ya chuo hicho yalihusisha michezo mbalimbali ikiwemo mpira wa miguu, netiboli na riadha, yakilenga kukuza vipaji na kuimarisha mshikamano miongoni mwa wanafunzi.

Katika hayo Mshindi wa mpira wa miguu alipokea zawadi ya mbuzi mmoja, huku washindi wa michezo mingine na watu binafsi waliofanya vizuri wakitunukiwa zawadi mbalimbali.

Wanafunzi na wadau waliohudhuria fainali hiyo walieleza kufurahishwa na kiwango cha ushindani kilichoonyeshwa na timu zote, huku wakiipongeza Community Development kwa kuonyesha kiwango bora na kustahili ubingwa huo.

Matokeo ya Fainali

Community Development 4-0 Finance

mgeni rasmi Samwel Jackson, Katibu wa Mbunge wa Jimbo la Shinyanga Mjini akizungumza.

Mwenyekiti wa mtaa wa Miti mirefu Nassor Mokhe.













 

Post a Comment

Previous Post Next Post