" KASHISHI FC YAANDIKA HISTORIA KWA KUMUONDOA BINGWA MTETEZI SANGU FC KATIKA NIACHEKONA CUP 2026 WENGI HAWAAMINI

KASHISHI FC YAANDIKA HISTORIA KWA KUMUONDOA BINGWA MTETEZI SANGU FC KATIKA NIACHEKONA CUP 2026 WENGI HAWAAMINI

Na Mapuli Kitina Misalaba

Bingwa mtetezi wa NIACHEKONA CUP 2024, Sangu FC kutoka Wilaya ya Kwimba, Mkoa wa Mwanza, ameaga rasmi mashindano ya NIACHEKONA CUP 2026 baada ya kufungwa kwa mikwaju ya penati na Kashishi FC katika mchezo uliochezwa leo Juni 12, 2026 kwenye Uwanja wa Mwabenda, Kata ya Solwa.

Mchezo huo uliokuwa ukisubiriwa kwa hamu kubwa na mashabiki wengi ulimalizika kwa sare ya bila kufungana ndani ya dakika 90 za kawaida, huku Sangu FC ikishindwa kutumia vyema nafasi ilizozipata ili kutafuta bao la ushindi.

Kutokana na matokeo hayo, mshindi alitafutwa kwa mikwaju ya penati ambapo Kashishi FC ilifanikiwa kupata penati nne dhidi ya tatu za Sangu FC na hivyo kuandika historia ya kumuondoa bingwa mtetezi wa mashindano hayo.

Ushindi huo wa Kashishi FC umeibua mshangao kwa mashabiki wengi wa soka, kwani timu hiyo ilirejeshwa kwenye mashindano kupitia nafasi ya Best Rooza, huku wengi wakiamini kuwa Sangu FC ilikuwa na nafasi kubwa ya kutetea ubingwa wake wa mwaka 2024.

Akizungumza baada ya mchezo huo, kocha wa Sangu FC kwa niaba ya timu yake amekubali matokeo hayo na kuushukuru uongozi wa mashindano kwa nafasi waliyopewa kushiriki. Aidha, amemuomba mwandaaji wa mashindano hayo kuendelea kuwapa fursa ya kushiriki katika matoleo yajayo ya NIACHEKONA CUP.

Kwa upande wao, viongozi wa Kashishi FC wameushukuru uongozi wa mashindano pamoja na Kamati ya Mashindano kwa kuwaamini na kuwarudisha kwenye mashindano kupitia nafasi ya Best Rooza. Wamesema ushindi dhidi ya bingwa mtetezi ni ishara kuwa wana uwezo wa kufanya vizuri zaidi na sasa wanaamini wanaweza kufika mbali na hata kutwaa ubingwa wa mwaka huu.

Kwa matokeo hayo, Sangu FC imehitimisha safari yake katika NIACHEKONA CUP 2026 huku Kashishi FC ikitinga hatua ya robo fainali pamoja na timu nyingine zilizofuzu. Mchezo huo pia umehitimisha rasmi hatua ya timu 12 bora na kufungua pazia la hatua ya robo fainali inayotarajiwa kuwa na ushindani mkubwa zaidi.

Akizungumza kwa niaba ya Kamati ya Mashindano, Makamu Mwenyekiti wa NIACHEKONA CUP, Samwel Stephen, ametangaza ratiba ya mchezo wa kesho ambapo Songambele Mhangu FC kutoka Kata ya Salawe Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga itamenyana na Ufukunyungu FC kutoka Kata ya Ngokolo Manispaa ya Shinyanga katika pambano la robo fainali linalotarajiwa kuvutia mashabiki wengi.

Samwel Stephen amewahimiza wananchi, wadau wa michezo na mashabiki kuendelea kujitokeza kwa wingi katika Uwanja wa Mwabenda ili kushuhudia michezo mbalimbali inayoendelea kuibua vipaji vya vijana na kuimarisha mshikamano wa jamii.

Mashindano ya NIACHEKONA CUP 2026 yameandaliwa na Bwana Paul Daud Augustino maarufu MC NIACHEKONA kwa ufadhili wa Shirika la Lushu Foundation, yakiwa na lengo la kuibua vipaji vya vijana, kukuza michezo, kuimarisha amani na mshikamano wa jamii.

Kwa mawasiliano ya shughuli mbalimbali za michezo, matangazo na ushereheshaji wa matukio, wasiliana na MC NIACHEKONA kupitia namba 0757 267 738.

Kikosi cha Sangu FC.

 

Post a Comment

Previous Post Next Post