" MAADHIMISHO YA SIKU YA FAMILIA NA MTOTO WA AFRIKA: WAZAZI WATAKIWA KUJENGA MALEZI BORA KWA TAIFA IMARA

MAADHIMISHO YA SIKU YA FAMILIA NA MTOTO WA AFRIKA: WAZAZI WATAKIWA KUJENGA MALEZI BORA KWA TAIFA IMARA

Kauli Mbiu: "Mtoto ni Mlezi, Msingi wa Familia Bora kwa Taifa Imara."

Kanisa lenye Kituo cha Huduma ya Maendeleo ya Mtoto (CDSP) kwa kushirikiana na Shirika la Compassion Tanzania, Klasta ya Shinyanga, limeadhimisha Siku ya Familia na Mtoto wa Afrika kwa lengo la kuhamasisha jamii kuwekeza katika malezi bora ya watoto, kulinda haki zao na kujenga familia imara zitakazozalisha taifa lenye maadili mema.

Maadhimisho hayo yaliwakutanisha viongozi wa dini na serikali, wazazi, walezi, watoto, vijana pamoja na wadau mbalimbali wa maendeleo ili kujadili nafasi ya familia katika malezi ya mtoto wa Afrika.

Ibada ya Ufunguzi

Shughuli ilianza kwa ibada iliyoongozwa na Mchungaji Papias Sendegeya, ambaye alifungua kwa Neno la Mungu na kuwahimiza watoto kuwa jasiri, wachapakazi na wenye malengo makubwa maishani.

Katika ujumbe wake, mchungaji aliwataka watoto kutokata tamaa mbele ya changamoto bali wajitume katika elimu, waishi kwa maadili mema na kumtumaini Mungu ili waweze kufanikisha ndoto zao na kuwa viongozi wa kesho.

Aidha, aliwakumbusha wazazi kuwa jukumu la kulea watoto si la kuwapatia mahitaji ya msingi pekee, bali pia kuwaongoza kiroho, kimaadili na kijamii.

Afisa Ustawi wa Jamii Atoa Elimu ya Malezi Bora

Mtoa mada mkuu alikuwa Afisa Ustawi wa Jamii wa Manispaa ya Shinyanga, Bi. Elizabeth Mweo, ambaye alianza kwa kuwauliza wazazi swali lililowafanya wengi kutafakari:

"Mtoto wako jamii inamchukulia kuwa ni mtoto wa aina gani? Mtoto wako anajulikana kwa lipi katika jamii?"

Alieleza kuwa tabia na mwenendo wa mtoto huanzia nyumbani, hivyo aina ya malezi anayopata ndiyo huamua namna atakavyoonekana mbele ya jamii.

Katika mada yake, alifundisha aina nne za malezi zinazopatikana katika familia.

1. Malezi ya Kimabavu

Afisa Elizabeth alieleza kuwa haya ni malezi ambayo mzazi hutumia mamlaka makubwa bila kumpa mtoto nafasi ya kujieleza.

Katika malezi haya:

  • Mtoto hana uhuru wa kutoa maoni yake.
  • Maamuzi yote hufanywa na mzazi.
  • Hisia na mahitaji ya mtoto hayapewi nafasi.

Alionya kuwa athari za malezi haya ni pamoja na:

  • Kumjengea mtoto hofu.
  • Kupunguza uwezo wa kujiamini.
  • Kushindwa kufanya maamuzi akiwa mtu mzima.
  • Kuongeza uwezekano wa mtoto kukua akiwa mkali au mkatili kwa wengine.

2. Malezi ya Kidemokrasia

Haya ndiyo malezi aliyoyapendekeza zaidi.

Alieleza kuwa katika malezi haya, wazazi na watoto huishi kwa kufuata taratibu na sheria za familia zinazowapa wote nafasi ya kusikilizana.

Katika malezi haya:

  • Mtoto husikilizwa.
  • Anapata nafasi ya kueleza hisia na mawazo yake.
  • Nidhamu hutolewa kwa upendo na maelekezo.
  • Familia hujenga mawasiliano mazuri.

Alisisitiza kuwa malezi haya humjengea mtoto kujiamini, kuwajibika na kuwa raia mwema mwenye maadili.

3. Malezi Huru

Afisa Ustawi alieleza kuwa katika malezi haya mzazi humwachia mtoto kufanya karibu kila kitu anachotaka bila kuweka mipaka wala kufuatilia mwenendo wake.

Alionya kuwa uhuru uliopitiliza unaweza kusababisha mtoto:

  • Kukosa nidhamu.
  • Kushindwa kuheshimu mamlaka.
  • Kujiingiza katika makundi mabaya na tabia hatarishi.

4. Malezi Ulia

Aidha, alizungumzia malezi ya uzembe au kupuuza wajibu wa mzazi, ambapo mtoto hukosa uangalizi, mwongozo na muda wa wazazi wake.

Katika mazingira haya mtoto hukua bila kupata upendo, ushauri na ulinzi wa kutosha, jambo linaloweza kumfanya atafute faraja sehemu zisizo salama na kuathiri maendeleo yake ya kimwili, kiakili na kihisia.

Akihitimisha mada yake alisema:

"Mzazi, jitafakari leo. Wewe unaangukia katika kundi gani la malezi? Tukibadili malezi yetu leo, tutabadilisha maisha ya watoto wetu kesho."

Mdahalo Wajadili Umuhimu wa Mtoto Katika Familia

Baada ya mada hiyo kulifanyika mdahalo uliobeba ujumbe wa:

"Mtoto ni msingi wa familia bora na taifa imara."

Washiriki walijadili namna wazazi, viongozi wa dini, serikali na jamii kwa ujumla wanavyoweza kushirikiana kuhakikisha watoto wanapata malezi bora, elimu, ulinzi na mazingira salama ya kukua.

Risala Yasomwa Mbele ya Mgeni Rasmi

Katika maadhimisho hayo pia ilisomwa risala iliyoandaliwa na Kanisa lenye Kituo cha Huduma ya Maendeleo ya Mtoto kwa kushirikiana na Shirika la Compassion.

Risala hiyo iliainisha mafanikio yaliyopatikana kupitia huduma za maendeleo ya mtoto pamoja na mapendekezo mbalimbali kwa serikali na wadau kuhusu kuimarisha ulinzi wa mtoto, kupambana na mimba za utotoni, kuboresha elimu na kuendelea kuwekeza katika malezi bora ya watoto.

Mgeni Rasmi Asisitiza Urafiki Kati ya Wazazi na Watoto

Akijibu risala hiyo, Mgeni Rasmi ambaye ni Afisa Maendeleo aliwapongeza waandaaji kwa kuandaa maadhimisho hayo yenye manufaa kwa jamii.

Katika hotuba yake aliwataka wazazi kujenga urafiki na watoto wao badala ya kuwafanya waishi kwa hofu.

"Mtoto awe rafiki yako. Asiogope kukueleza changamoto zake. Akikuamini, atakushirikisha mambo yake mapema kabla hayajawa makubwa."

Aidha, alionya kuhusu matumizi holela ya simu kwa watoto, akisema wazazi wanapaswa kusimamia matumizi ya teknolojia badala ya kuwaachia watoto simu bila uangalizi.

Pia alisisitiza kuwa jukumu la malezi ni la wazazi wote na jamii kwa ujumla, hivyo halipaswi kuachiwa wasaidizi wa nyumbani pekee.

Akilihitimisha hotuba yake, aliwashukuru Shirika la Compassion kwa kazi kubwa wanayoifanya katika kuwalea watoto na kuahidi kuwa serikali imepokea mapendekezo yote yaliyomo kwenye risala na itaendelea kuyafanyia kazi kwa kushirikiana na wadau mbalimbali.

Vilevile aliwapongeza viongozi wa dini, wazazi, walezi na kamati ya maandalizi kwa kufanikisha maadhimisho hayo.

Shukrani

Kwa niaba ya Klasta ya Shinyanga, Mwenyekiti wa Klasta, Isac Mbise, alitoa shukrani kwa viongozi wa serikali, viongozi wa dini, Shirika la Compassion, wazazi, walezi, watoto na wageni wote waliojitokeza kushiriki katika maadhimisho hayo.

Alisema ushiriki mkubwa wa wadau unaonesha dhamira ya pamoja ya kujenga kizazi chenye maadili na mustakabali mzuri wa Taifa.

Hitimisho

Maadhimisho ya Siku ya Familia na Mtoto wa Afrika yameacha ujumbe mzito kwa jamii kwamba malezi bora huanzia nyumbani. Familia ndiyo msingi wa kumjenga mtoto mwenye maadili, anayejitambua na anayechangia maendeleo ya taifa.

Kauli mbiu ya mwaka huu imeendelea kuwa mwito kwa kila mzazi na mlezi kutekeleza wajibu wake kwa upendo, busara na uwajibikaji, kwa kutambua kuwa:

"Mtoto ni Mlezi, Msingi wa Familia Bora kwa Taifa Imara."

 



 SHY TALENT FILMS - CONTENT YA MWISHO DRAMA

🥃🍶 TUMIA VINYWAJI BORA VYA KAMPUNI YA EAST AFRICAN SPIRITS – BEI RAFIKI, LADHA SAFI BILA HARUFU MBAYA

  • Wasiliana nasi:
    📍 East African Spirits (T) Ltd
    📞 +255 767 650 806 | +255 652 096 254

Post a Comment

Previous Post Next Post