Na Mapuli Misalaba, Shinyanga
Mzee Nalinga Najulwa mwenye umri wa Miaka 103
anayeishi mtaa wa Dome kata ya Ndembezi Manispaa ya Shinyanga amesema Tanzania inapofikisha
Miaka 61 ya uhuru suala la maadili liwe ajenda ili kuendelea kuwa na Taifa
lenye kizazi chenye uadilifu.
Ameyasema hayo wakati akizungumza na Misalaba Blog
ambapo amesema licha ya mabadiliko mbalimbali yanayojitokeza suala la maadili
limeendelea kusahaulika hali inayochangia kuwa na kizazi kinachorithi
mmomonyoko wa maadili.
Mzee Najulwa ameiomba jamii kuheshimu maadili ya
kitanzania badala ya kufuata tamaduni za mataifa ya Magharibi ambazo baadhi
yake zinamafundisho yanayosababisha madhara ikiwemo vitendo vya ukatili katika
jamii.
Amewataka viongozi wa dini kutumia nafasi yao kutoa
mafundisho kwa waumini wao waweza kuwa na hofu ya Mungu ili kuondokana na
vitendo viovu.
“Hii
inasababishwa na baadhi ya watu kuwa na tamaa katika Dunia hii nawaomba sana
viongozi wa Dini na kwenye misikiti wanatakiwa wafanye bidii sana kuwaelimisha
watu ili wawe karibu na uchaji wa Mungu maana wameshayaacha mambo ambayo Mungu
ameagiza wanajifanya wao wenyewe”.amesema Mzee Nalinga
Najulwa
Mzee Najulwa ametumia nafasi hiyo kuiomba serikali
kuwa na utamaduni wa kuielezea historia ya uhuru wa Tanganyika kwa njia
mbalimbali ikiwemo mikutano ya hadhara ili kuwawezesha kuwa na kumbukumbu nzuri
juu ya Nchi yao.
“Viongozi
wa serikali wakazane kuwaelimisha watu na wawe na utaratibu wa kufanya mikutano
ya kuwaelezea wapate elimu hiyo ya kumbukumbu kuwakumbusha mambo yalivyokuwa
tangu Mwanzo lakini pia Rais anatakiwa awe karibu na watu kwa ajili ya
kuwaelezea jinsi utawala unavyoendeleo”.amesema Mzee Nalinga
Aidha Mzee Nalinga Najulwa amempongeza Rais wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuungana na
viongozi wengine marais wa awamu zilizopita kuendeleza umoja katika Taifa la
Tanzania.
Leo Disemba 9, 2022 ni siku ya Kumbukumbu ya Maadhimisho ya Miaka 61 ya uhuru wa Tanganyika ambayo huadhimishwa kila Mwaka ifikapo Mwezi na tarehe kama ya leo.
Mzee Nalinga Najulwa mwenye umri wa Miaka 103 anayeishi mtaa wa Dome kata ya Ndembezi Manispaa ya Shinyanga
akizungumza na Misalaba Blog
Post a Comment