" WANAFUNZI WA DARASA LA NNE WAKUTWA WAMEFARIKI DUNIA KWENYE MAJI SHINYANGA

WANAFUNZI WA DARASA LA NNE WAKUTWA WAMEFARIKI DUNIA KWENYE MAJI SHINYANGA

Na Mapuli Misalaba, Shinyanga

Watoto wawili wa darasa la Nne shule ya msingi Maganzo Wilaya ya Kishapu wamekutwa wamefariki Dunia kwenye mto unaotiririsha maji kitongoji cha Mwembeni kijiji cha Masagala kata ya Maganzo.

Akizungumza leo na Misalaba Blog mtendaji wa kijiji cha Masagala Bwana Kalima Manyesho amesema kuwa tukio hilo limetokea Jumatano Januari 18,2023 majira ya saa kumi na mbili jion.

Ameeleza kuwa watoto hao ni wakazi wa kitongoji cha Majengo kata ya Maganzo walikutwa wamefariki Dunia baada ya kuzama kwenye mto unaotiririsha maji wakiwa wanaogelea kwa kutumia makopo ya ndoo za maji kama maboya ya kuogelea.

“Nilipigiwa simu majira ya saa kumi na mbili jioni kwamba watoto hao wamekutwa wakiwa wamezama kwenye hilo timbwi nikachukua polisi tukaenda kuwatoa tukawapeleka Hospitali tulipotoka Hospitali tukawapeleka kwa wazazi”

“Lakini kwa muda huo wa saa kumi na mbili jioni walikuwa tayari wameshatoka shule nafikiri labda hawakuwa kwenye uangalizi mzuri wa wazazi”.amesema mtendaji Manyesho

Kwa upande wake mwenyekiti wa kijiji cha Masagala Bwana Elias Jiganga Masasi amekiri kuwepo kwa tukio hilo huku akiwaomba wazazi kuwajibika ipasavyo katika suala la ulinzi wa watoto ili kuimarisha usalama wao.

“Taarifa za watoto hao nilizipokea ni kweli wamefariki jambo hili nalikemea kwa sababu wazazi huwa tunawaambia mara kwa mara na suala la watoto tulishakataa wasiogelee kwenye maji wakitoka shule wanatakiwa warudi nyumbani wakatulie hili ni wazazi tu walishindwa kuwasimamia watoto hao”.amesema mwenyekiti Masasi

Watoto waliofariki Dunia ni Hamis Ibrahim mwenye umri wa Miaka kumi (10) na Kadri Rashidi mwenye umri wa Miaka kumi (10) ambao wote walikuwa wanasoma darasa la Nne shule ya msingi Maganzo Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu Mkoani Shinyanga.

Mazishi ya Kadri Rashidi yamefanyika siku ya jana Alhamis huku mazishi ya Hamis Ibrahim yanafanyika leo Ijumaa Januari 20,2023.

Juhudi za kumpata kamanda wa jeshi la Polisi Mkoa wa Shinyanga bado hazijafanikiwa.

Post a Comment

Previous Post Next Post