" USHIRIKIANO WA CHUO CHA MADINI SHINYANGA NA BRIGHT INSTITUTE KUFUNGUA FURSA ZA AJIRA

USHIRIKIANO WA CHUO CHA MADINI SHINYANGA NA BRIGHT INSTITUTE KUFUNGUA FURSA ZA AJIRA

Na Mapuli Kitina Misalaba

Chuo cha Madini Shinyanga (Earth Sciences Institute of Shinyanga) kimepokea ugeni kutoka THE BRIGHT INSTITUTE, taasisi ya utafiti na uzalishaji wa betri kupitia madini muhimu ya kimkakati iliyo chini ya Chuo Kikuu cha North Carolina nchini Marekani, kwa lengo la kujadili na kuona uwezekano wa kuanzisha ushirikiano wa maendeleo ya teknolojia, utafiti na mafunzo kuhusu madini muhimu ya kimkakati (Critical Minerals).

Ugeni huo umepokelewa na uongozi wa chuo ukiongozwa na Mkuu wa Chuo pamoja na Mkurugenzi wa Chuo, ambapo pande hizo zilifanya mazungumzo yaliyolenga kuimarisha ushirikiano utakaowezesha Tanzania kunufaika zaidi na rasilimali zake za madini muhimu ya kimkakati.

Mkuu wa Chuo cha madini Shinyanga, Karebo Peter amesema ushirikiano huo ni hatua muhimu katika kuiwezesha Tanzania kujenga uwezo wa kitaalamu katika sekta ya madini muhimu ya kimkakati, ambayo yanahitajika duniani kwa ajili ya utengenezaji wa betri zinazotumika kwenye magari ya umeme, mifumo ya nishati ya jua, simu, saa pamoja na vifaa mbalimbali vinavyotumia betri.

Amesema kupitia ushirikiano huo, chuo kinatarajia kuongeza uwezo wa kufundisha na kufanya tafiti za kisasa zitakazowezesha kuzalisha wataalamu wenye ujuzi wa kushiriki katika mnyororo mzima wa thamani wa madini hayo, kuanzia utafiti, uchimbaji, uchakataji hadi utengenezaji wa bidhaa zenye thamani kubwa.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Chuo hicho Prof. Athanas Macheyeki amesema ushirikiano huo unatarajiwa kuleta manufaa makubwa kwa taifa kwa kusaidia kuanzishwa kwa maabara za kisasa za mafunzo na utafiti, pamoja na kuvutia wawekezaji wa viwanda vya kutengeneza betri nchini.

Ameeleza kuwa hatua hiyo itaongeza thamani ya madini yanayopatikana kwa wingi nchini Tanzania, kuongeza ajira kwa vijana na kuchochea ukuaji wa uchumi kupitia sekta ya madini.

Naye Mkurugenzi wa taasisi ya The Bright institute Prof. Hemali Rathnayake amesema taasisi hiyo imevutiwa na fursa zilizopo Tanzania katika madini muhimu ya kimkakati na inaona umuhimu wa kushirikiana na taasisi za elimu na utafiti ili kujenga kizazi cha wataalamu kitakachoweza kuongoza maendeleo ya teknolojia hiyo barani Afrika.

Amebainisha kuwa ushirikiano kati ya taasisi za elimu, serikali na sekta binafsi ni msingi muhimu katika kuhakikisha rasilimali za madini zinawanufaisha wananchi kupitia uongezaji thamani na maendeleo ya teknolojia.

Baadhi ya Wanafunzi wa Chuo cha Madini Shinyanga wameeleza kufurahishwa na ujio wa wageni hao, wakisema umewapa matumaini ya kupata maarifa mapya, mafunzo ya kisasa, pamoja na fursa za kufanya tafiti na kushiriki katika miradi ya kimataifa itakayowaongezea ushindani katika soko la ajira.

 Prof. Hemali ameeleza kuwa pamoja na kutembelea Chuo cha Madini Shinyanga, pia imefanya ziara katika taasisi mbalimbali zinazohusika na sekta ya madini nchini, zikiwemo Taasisi ya Utafiti wa Jiolojia Tanzania (GST), Wizara ya Madini na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, ikiwa ni sehemu ya kutafuta ushirikiano wa pamoja katika maendeleo ya teknolojia ya madini muhimu ya kimkakati.

Baadhi ya madini muhimu ya kimkakati yanayopatikana nchini Tanzania na yenye umuhimu mkubwa katika teknolojia ya kisasa ni pamoja na Lithium, Cobalt, Graphite, Nickel, Rare Earth Elements (REEs), Tantalum, Niobium na Manganese, ambayo yanatumika katika utengenezaji wa betri za magari ya umeme, vifaa vya kielektroniki na mifumo ya nishati safi.

Wakati huo huo, uongozi wa Chuo cha Madini Shinyanga umewakaribisha vijana na wahitimu wa elimu ya sekondari na vyuo mbalimbali kujiunga na chuo hicho ili kupata taaluma zinazohitajika katika sekta ya madini na teknolojia za kisasa.

Uongozi huo umeeleza kuwa chuo kinaendelea kuboresha mazingira ya kujifunzia, maabara na ushirikiano wa kimataifa ili kuwaandaa wataalamu watakaoshiriki kikamilifu katika maendeleo ya sekta ya madini nchini na duniani.





Post a Comment

Previous Post Next Post