Na Mapuli Kitina Misalaba
Wadau mbalimbali mkoani Shinyanga wametakiwa kuendelea
kuimarisha ushirikiano katika kuzuia na kupambana na usafirishaji haramu wa
binadamu pamoja na kuhamasisha uhamiaji salama, ili kulinda haki za wanawake,
watoto, vijana na makundi mengine yaliyo katika mazingira hatarishi.
Wito huo umetolewa na Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa
Shinyanga, Rafael Msela, wakati akifunga semina ya kimkoa kuhusu Usafirishaji
Haramu wa Binadamu (TIP) na Uhamiaji Salama iliyowakutanisha wawakilishi wa
taasisi za serikali, vyombo vya ulinzi na usalama, mahakama, ofisi ya mashtaka,
uhamiaji, ustawi wa jamii, maendeleo ya jamii, asasi za kiraia, viongozi wa
dini pamoja na vyombo vya habari.
Akizungumza katika hafla ya kufunga semina hiyo, Msela
amewashukuru waandaaji ambao ni Shirika la Community of Volunteers for the
World (CVM), CHODAWU na Sekretarieti ya Kupambana na Usafirishaji Haramu wa
Watu (ATS) chini ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kwa kuandaa mafunzo hayo
yaliyolenga kuongeza uelewa kuhusu usafirishaji haramu wa binadamu na uhamiaji
salama.
Amesema mada zilizowasilishwa zimewajengea washiriki
uwezo wa kutambua mbinu zinazotumiwa na wahalifu, namna ya kuwabaini waathirika
pamoja na hatua zinazopaswa kuchukuliwa katika kuzuia, kulinda na kushughulikia
matukio ya usafirishaji haramu wa binadamu.
Msela alisema usafirishaji haramu wa binadamu si
tatizo la taasisi moja, bali ni changamoto inayohitaji ushirikiano wa sekta
zote kwa kuwa waathirika wake wakubwa ni watoto, wasichana, wanawake na vijana
wanaodanganywa kwa ahadi za ajira au maisha bora na baadaye kuingia katika
mazingira ya unyonyaji, ukatili na kunyimwa haki zao za msingi.
Ameeleza kuwa katika Mkoa wa Shinyanga bado zipo
changamoto zinazohusiana na ajira za watoto katika sekta zisizo rasmi pamoja na
hatari zinazotokana na uhamiaji usio salama, hivyo elimu inayotolewa kupitia
semina hiyo inapaswa kuwafikia wananchi wengi zaidi.
Amewataka washiriki kuhakikisha maarifa waliyopata
hayaishii ndani ya ukumbi wa mafunzo bali yanatumika katika maeneo yao ya kazi
na kwenye jamii kwa kutoa elimu kuhusu viashiria vya usafirishaji haramu wa
binadamu, kutambua mapema waathirika na kuchukua hatua za haraka pale viashiria
vinapoonekana.
Aidha, ametoa wito kwa Serikali, vyombo vya ulinzi na
usalama, mahakama, ofisi ya mashtaka, asasi za kiraia, taasisi za dini, vyombo
vya habari pamoja na washirika wa maendeleo kuendelea kuimarisha ushirikiano
kwa kubadilishana taarifa kwa wakati, kuimarisha mifumo ya rufaa kwa waathirika
na kutekeleza wajibu wa kila mdau katika mapambano dhidi ya uhalifu huo.
Msela pia ameeleza kufurahishwa na kuimarishwa kwa Kikosi
Kazi cha Kupambana na Usafirishaji Haramu wa Binadamu (TIP Working Group),
akisema kitakuwa jukwaa muhimu la kuratibu utekelezaji wa maazimio yaliyofikiwa
wakati wa semina hiyo.
Akitoa mada kuhusu uhamiaji salama, Mrakibu wa
Uhamiaji Mkoa wa Shinyanga, Issa Kisiroti, amesema bado wapo baadhi ya wananchi
wanaokata hati za kusafiria (paspoti) kwa kufuata taratibu zote za kisheria,
lakini wanapofika mipakani huamua kutumia njia zisizo rasmi maarufu kama njia
za panya, jambo ambalo ni kosa la kisheria.
Amefafanua kuwa sheria za uhamiaji zinamtaka kila
mwenye paspoti kutumia vituo rasmi vya mipakani anapoingia au kutoka nchini, na
anayekiuka utaratibu huo anaweza kuchukuliwa hatua za kisheria kama
anavyofanyiwa mtu anayejihusisha na biashara ya magendo.
Kisiroti amesema Idara ya Uhamiaji imeendelea kutoa
elimu kwa wananchi kupitia kampeni ya "Mjue Jirani Yako", inayolenga
kuwahamasisha wananchi kuwafahamu watu wanaoishi katika maeneo yao na kutoa
taarifa kwa mamlaka wanapobaini wageni au watu wanaowatilia shaka ili hatua za
kisheria zichukuliwe mapema.
Aidha, ameonya kuwa baadhi ya watumishi wasiokuwa
waadilifu wamekuwa wakishirikiana na wasafirishaji haramu wa binadamu kwa
kupokea rushwa na kuwasaidia kuvuka mipaka kinyume cha sheria, akisisitiza kuwa
vitendo hivyo ni makosa yanayochukuliwa hatua kali za kisheria.
Ameongeza kuwa Tanzania imekuwa ikipokea wahamiaji
haramu kutoka nchi jirani ikiwemo Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Burundi na
Rwanda, lakini elimu inayoendelea kutolewa imechangia kupungua kwa matukio hayo
kutokana na wananchi kuelewa umuhimu wa kutumia nyaraka halali za kusafiria,
ikiwemo hati za muda mfupi.
Naye mwezeshaji kutoka Wizara ya Mambo ya Ndani ya
Nchi, Providence Simbila, alisema kusafiri si kosa, bali kosa ni kutumia
udanganyifu, vitisho au mbinu nyingine haramu kumsafirisha mtu kwa lengo la
kumtumikisha au kumnyonya.
Amesema sheria ya Kupambana na Usafirishaji Haramu wa
Binadamu inaweka adhabu kwa wahusika, ikiwemo kifungo cha kuanzia miaka mitatu
au adhabu nyingine kwa mujibu wa sheria.
Kwa upande wake, mwezeshaji kutoka Shirika la CVM, Mwajuma
Ally, amesema kupitia mradi wa EmPoWedeD II, shirika hilo linaendelea
kuwawezesha wasichana wanaofanya kazi za majumbani kutambua haki zao za msingi,
kupata mikataba ya ajira na kuboresha mazingira yao ya kazi.
Amesema wasichana wengi wanaofanya kazi za majumbani
bado wanakabiliwa na mishahara midogo, ukosefu wa mikataba ya kazi na
kutofahamu haki zao kama wafanyakazi, jambo linalowaweka katika hatari ya
kunyonywa na kudhurumiwa.
Mwajuma amesema mradi huo utatekelezwa kwa kipindi cha
miaka mitatu kuanzia mwaka 2026, ukiwa na shughuli mbalimbali zinazolenga
kuzuia usafirishaji haramu wa binadamu na kuhakikisha wafanyakazi wa majumbani
wanalindwa kwa kuzingatia sheria za kazi na haki za binadamu.
Ameongeza kuwa kupitia mradi huo, wafanyakazi wa
majumbani wanawezeshwa kupata elimu kuhusu haki zao, mafunzo ya ujuzi kupitia
VETA, ajira zenye staha pamoja na elimu ya uhamiaji salama ili kupunguza
uwezekano wa kudhurumiwa na kuingia kwenye mazingira ya usafirishaji haramu wa
binadamu.
Semina hiyo ni sehemu ya juhudi za Serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali za kuendelea kujenga uwezo wa taasisi na jamii katika kuzuia, kutambua na kupambana na usafirishaji haramu wa binadamu.
Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga, Rafael Msela, akizungumza wakati wa kufunga semina ya kimkoa kuhusu Usafirishaji Haramu wa Binadamu (TIP) na Uhamiaji Salama leo Julai 8, 2026 mjini Shinyanga.
Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga, Rafael Msela, akizungumza wakati wa kufunga semina ya kimkoa kuhusu Usafirishaji Haramu wa Binadamu (TIP) na Uhamiaji Salama leo Julai 8, 2026 mjini Shinyanga.
Mwezeshaji kutoka Shirika la CVM, Mwajuma Ally, akiwasilisha mada kuhusu ulinzi wa wafanyakazi wa majumbani, haki za wafanyakazi na juhudi za kuzuia usafirishaji haramu wa binadamu kupitia mradi wa EmPoWedeD II.
Mwezeshaji kutoka Shirika la CVM, Mwajuma Ally, akiwasilisha mada kuhusu ulinzi wa wafanyakazi wa majumbani, haki za wafanyakazi na juhudi za kuzuia usafirishaji haramu wa binadamu kupitia mradi wa EmPoWedeD II.
Mrakibu wa Uhamiaji Mkoa wa Shinyanga, Issa Kisiroti, akitoa elimu kuhusu umuhimu wa kutumia njia halali za kusafiri na kuzingatia sheria za uhamiaji.
Mrakibu wa Uhamiaji Mkoa wa Shinyanga, Issa Kisiroti, akitoa elimu kuhusu umuhimu wa kutumia njia halali za kusafiri na kuzingatia sheria za uhamiaji.
imewakutanisha wadau mbalimbali mkoani Shinyanga kujadili mikakati ya kuzuia uhalifu huo na kuimarisha ulinzi wa makundi yaliyo katika mazingira hatarishi.
imewakutanisha wadau mbalimbali mkoani Shinyanga kujadili mikakati ya kuzuia uhalifu huo na kuimarisha ulinzi wa makundi yaliyo katika mazingira hatarishi.
SHY TALENT FILMS - CONTENT YA MWISHO DRAMA
🥃🍶 TUMIA VINYWAJI BORA VYA KAMPUNI YA EAST AFRICAN SPIRITS – BEI RAFIKI, LADHA SAFI BILA HARUFU MBAYA
Wasiliana nasi:
📍 East African Spirits (T) Ltd
📞 +255 767 650 806 | +255 652 096 254





























Post a Comment