" SHINYANGA: WATU 21 WAJERUHIWA KATIKA AJALI YA BARABARANI IBADAKULI, MMOJA AFARIKI DUNIA

SHINYANGA: WATU 21 WAJERUHIWA KATIKA AJALI YA BARABARANI IBADAKULI, MMOJA AFARIKI DUNIA


Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Manispaa ya Shinyanga, Dkt. Moshi Lyoba, akielezea hali za majeruhi.


Na Mapuli Kitina Misalaba

Watu 21 walipata majeraha katika ajali ya barabarani iliyohusisha mabasi mawili, LBS na Happy Nation, jana majira ya saa kumi jioni katika eneo la Ibadakuli, Manispaa ya Shinyanga kati yao mwanamke mmoja aitwaye Christina Masanja mwenye umri wa miaka 37 mkazi wa Tabora, alifariki dunia wakati akiendelea kupatiwa matibabu.

Akizungumza na Misalaba Media, Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Manispaa ya Shinyanga, Dkt. Moshi Lyoba, amesema katika Hospitali hiyo walipokea majeruhi  21, wakiwemo wanawake nane (8), wanaume kumi na watatu (13), na watoto wawili.

Dkt. Lyoba ameeleza kuwa majeruhi wengi walikuwa na mifupa iliyovunjika na vidonda sehemu mbalimbali za miili yao.

"Tuliwapatia matibabu ya haraka majeruhi hao, lakini kwa bahati mbaya, mmoja wao, mwanamke aitwaye Christina Masanja mwenye umri wa miaka 37 na mkazi wa Tabora, alifariki dunia wakati tukiendelea kumpatia matibabu kutokana na majeraha makubwa aliyopata kichwani," amesema Dkt. Lyoba.

Aidha, Dkt. Lyoba amebainisha kuwa wagonjwa wanne walihamishiwa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga, Mwawaza, kutokana na hali zao kuwa mbaya zaidi.

Miongoni mwao ni mgonjwa aliyevunjika mfupa, mwingine aliyevunjika nyonga, na mtoto mwenye umri wa miaka mitano ambaye amevunjika mkono, ambao wanahitaji matibabu maalum.

"Wagonjwa waliobaki wamelazwa wodini na hali zao zinaendelea kuimarika, lakini tunatarajia kuwapa rufaa wagonjwa watatu kwenda Hospitali ya Rufaa kwa matibabu zaidi," amesema Dkt. Moshi

Wananchi walioshuhudia ajali hiyo wamewasihi madereva kuwa makini barabarani na kuzingatia sheria za usalama ili kuepusha ajali huku wakiliomba  jeshi la polisi kitengo cha usalama barabarani kutekeleza wajibu wao ipasavyo ili kuzuia ajali.

Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Manispaa ya Shinyanga, Dkt. Moshi Lyoba, akizungumza na Misalaba Media.


Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Manispaa ya Shinyanga, Dkt. Moshi Lyoba, akizungumza na Misalaba Media.

TAZAMA HAPA PICHA ZA MABASI MAWILI YALIYOPATA AJALI MKOANI SHINYANGA



 

Post a Comment

Previous Post Next Post