" BEYA FC YASHINDA KWA PENATI YATINGA FAINALI YASUBIRI MSHINDI WA SALAWE NA MWASENGE KATIKA LIGI YA MAKAMBA LAMECK

BEYA FC YASHINDA KWA PENATI YATINGA FAINALI YASUBIRI MSHINDI WA SALAWE NA MWASENGE KATIKA LIGI YA MAKAMBA LAMECK

Na Mapuli Kitina Misalaba

Mashindano ya mpira wa miguu ya Krismas Cup, yaliyoandaliwa na Makamba Mussa Lameck, yameendelea leo katika uwanja wa Mhangu kwa nusu fainali ya kwanza kati ya Beya FC na Kano FC.

Mchezo huo umemalizika kwa ushindi wa Beya FC kupitia mikwaju ya penalti, baada ya dakika 90 za mchezo kumalizika bila kufungana.

Kwa matokeo hayo, Beya FC imekata tiketi ya kucheza fainali ya mashindano hayo. Akizungumza baada ya mechi hiyo, msimamizi wa ligi hiyo, Mwalimu Emmanuel Enock Kijida, amesema nusu fainali ya pili itapigwa kesho, ikizikutanisha Salawe FC na Mwasenge FC, na mshindi atakutana na Beya FC kwenye fainali.

“Kwa matokeo haya, Beya FC wamefuzu kuingia fainali na wanaenda kukutana na mshindi wa mechi ya kesho. Timu zilizopoteza leo na zitakazopoteza kesho zitacheza Jumatatu kumtafuta mshindi wa tatu,” amesema Mwalimu Kijida.

Aidha, ametoa wito kwa wachezaji kuhakikisha wanacheza kwa amani, nidhamu, na kuheshimu waamuzi, akisisitiza kuwa mashindano haya yanalenga kukuza vipaji na kuimarisha maendeleo ya michezo katika mkoa wa Shinyanga.

Kwa upande wake, mwenyekiti wa Sungusungu, mzee Moto Mussa Kalamji, amepongeza mwandaaji wa ligi hiyo, Makamba Mussa Lameck, kwa juhudi zake za kudumisha utamaduni wa michezo.

“Kwanza nimshukuru kijana wetu mpendwa Makamba kwa kazi kubwa aliyoifanya. Hii ni burudani muhimu kwa wananchi wetu na inakuza michezo. Ninazipongeza timu zote, hasa Beya FC, lakini niwaonye kwamba kazi bado haijaisha. Wakae mguu sawa kuelekea fainali,” amesema mzee Moto.

Fainali za Krismas Cup zinatarajiwa kufanyika Jumanne, Desemba 17, 2024, ambapo zawadi mbalimbali zitatolewa kwa washindi wa nafasi ya kwanza hadi ya tatu.

Mashindano haya yanadhaminiwa na kampuni ya MCL, inayomilikiwa na Makamba Mussa Lameck, ambayo inajihusisha na biashara ya nafaka, ikiwa ni juhudi za kuchochea maendeleo ya michezo mkoani Shinyanga.

 

Post a Comment

Previous Post Next Post