Na Mapuli Kitina Misalaba
Katika kukabiliana na changamoto ya ajira kwa vijana, Mamlaka
ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) kupitia Chuo cha Ufundi Stadi
Shinyanga imeendelea kupanua wigo wa mafunzo ya ufundi stadi ili kuwawezesha
vijana kujiajiri na kuajiriwa katika sekta mbalimbali za uzalishaji.
Akizungumza na waandishi wa habari, Mkuu wa Chuo cha
VETA Shinyanga, Abraham Richard Mbughuni amesema Serikali ya Awamu ya Sita
inayoongozwa na Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan imeweka msisitizo mkubwa katika
elimu ya ujuzi kama nyenzo muhimu ya kukuza ajira na uchumi wa taifa.
Amesema katika hotuba yake ya Bunge ya Novemba 14,
2025, Rais alisisitiza umuhimu wa kuunganisha mafunzo ya ufundi stadi na miradi
mikakati ya kitaifa ikiwemo reli ya kisasa (SGR), bandari, uchumi wa buluu,
madini na gesi, hatua inayofungua fursa pana kwa wahitimu wa vyuo vya ufundi
stadi.
Mbughuni ameeleza kuwa VETA ni wakala wa Serikali
ulioanzishwa kwa Sheria ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi, Sura ya 82, ukiwa
na jukumu la kuratibu, kugharamia na kutoa mafunzo ya ufundi stadi nchini.
“Kwa lugha rahisi, VETA ndiyo inazalisha
watu wanaojenga Tanzania kwa vitendo. Nyumba, barabara, umeme, mashine
viwandani na hata huduma za utalii zinategemea mafundi stadi,”
amesema.
Ameongeza kuwa dira ya VETA ni kuona Tanzania yenye
mafundi stadi mahiri na wa kutosha, huku kaulimbiu ikiwa ni ‘Ufundi Stadi,
Fursa Kama Zote, Kwa Watu Wote’.
Katika kupanua fursa kwa vijana mkoani Shinyanga, chuo
hicho kimeongeza uwezo wa udahili kufuatia upanuzi wa miundombinu uliofanyika
kupitia mradi wa Benki ya Maendeleo ya Afrika (ADB).
Kabla ya upanuzi huo, chuo kilikuwa na uwezo wa
kudahili wanafunzi 400 wa kozi za muda mrefu na chini ya 1,200 wa kozi za muda
mfupi kwa mwaka. Hivi sasa, uwezo umeongezeka hadi wanafunzi 545 wa muda mrefu
na zaidi ya 3,000 wa muda mfupi kwa mwaka.
Kutokana na ubora wa mafunzo, chuo hicho hupokea pia
wanafunzi wa kozi za muda mfupi kutoka nchi za Afrika Mashariki na Kati, hatua
inayochochea ajira ndani na nje ya nchi.
Mbughuni amesema VETA Shinyanga imeendelea kuboresha
na kuanzisha kozi mpya zinazoendana na mahitaji ya soko la ajira, zikiwemo
umeme wa majumbani na viwandani, uashi, useremala, ushonaji na ubunifu wa
mavazi, uchomeleaji na uundaji vyuma, ufundi bomba, pamoja na ukataji na
ung’arishaji wa madini vito.
Aidha, chuo kimeanzisha kozi mpya za ufundi magari,
umeme wa magari na utengenezaji pamoja na ukarabati wa barabara ili kukidhi
mahitaji ya sekta ya ujenzi na miundombinu.
Katika kuhakikisha hakuna kijana anayeachwa nyuma,
VETA Shinyanga imetoa mafunzo kwa makundi maalumu wakiwemo vijana wasio na
ajira, wanawake na vikundi vya ujasiriamali.
Programu ya Wanawake na Samia ilinufaisha washiriki
368, huku mradi wa bomba la mafuta wa EACOP ukitoa mafunzo kwa washiriki 20
(wanaume 16 na wanawake 4), wote wakipatiwa ujuzi wa kuwawezesha kujiajiri au
kuajiriwa.
Chuo pia kinaendelea kushirikiana na migodi, makampuni
ya ujenzi, karakana binafsi na taasisi za umma katika utoaji wa Mafunzo kwa
Vitendo (IPT) na mfumo wa Uanagenzi Pacha (DATS), unaowawezesha wanafunzi
kupata uzoefu wa moja kwa moja mahali pa kazi.
Kupitia utaratibu wa Recognition of Prior Learning
(RPL), mafundi waliopata ujuzi nje ya mfumo rasmi hupimwa na kuthibitishiwa
uwezo wao kwa kupewa vyeti vinavyotambulika kitaifa, hatua inayowawezesha
kushiriki zabuni na kupata ajira rasmi.
Serikali kupitia VETA Makao Makuu imeendelea kuboresha
karakana, madarasa na kununua vifaa vya kisasa vya kufundishia na kujifunzia
ili kuongeza ubora wa mafunzo na idadi ya wanafunzi wanaodahiliwa.
Mbughuni amesisitiza kuwa dunia ya leo inahitaji zaidi
uwezo wa kufanya kazi kuliko vyeti pekee.
“Ujuzi ni mtaji, ujuzi ni ajira, ujuzi ni
kujitegemea na ujuzi ni heshima,” amesema.
Ametumia nafasi hiyo kuwahamasisha vijana kujitokeza
kujiunga na VETA Shinyanga ili kupata stadi zitakazowawezesha kujenga maisha
yao na kuchangia maendeleo ya taifa.
Amesema kupitia uwekezaji wa Serikali ya Awamu ya
Sita, VETA imekuwa injini ya kuzalisha ajira na kukuza uchumi shindani.
“Ninawaomba wanahabari muendelee kuwa mabalozi wa kuelimisha jamii kuhusu fursa hizi, ili kila kijana ajue kuwa mustakabali wake uko mikononi mwake. VETA Shinyanga ipo kumwezesha — VETA Shinyanga, Kazi Mkononi,”
Mkuu wa Chuo cha VETA Shinyanga, Abraham Richard
Mbughuni akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake leo Machi 2, 2026.

🥃🍶 TUMIA VINYWAJI BORA VYA KAMPUNI YA EAST AFRICAN SPIRITS – BEI RAFIKI, LADHA SAFI BILA HARUFU MBAYA
Wasiliana nasi:
📍 East African Spirits (T) Ltd
📞 +255 767 650 806 | +255 652 096 254










Post a Comment