" SERIKALI YATAKA VYOMBO VYA HABARI VIWE MSINGI WA HAKI NA USAWA KATIKA UCHAGUZI MKUU 2025

SERIKALI YATAKA VYOMBO VYA HABARI VIWE MSINGI WA HAKI NA USAWA KATIKA UCHAGUZI MKUU 2025

Waziri wa  Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Prof. Palamagamba Kabudi  akitoa hotuba wakati akifungua Mkutano wa Mwaka wa Vyombo vya Utangazaji Tanzania ' Annual Broadcaster's Conference'

Na Mapuli Kitina Misalaba

Serikali imesema itaendelea kushirikiana na vyombo vya habari nchini ili kuhakikisha vinafanya kazi kwa uhuru na weledi kuelekea Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025.

Kauli hiyo imetolewa leo Februari 13, 2025, na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Prof. Palamagamba Kabudi, wakati akifungua Mkutano wa Mwaka wa Vyombo vya Utangazaji Tanzania Annual Broadcasters’ Conference, unaofanyika jijini Dodoma kwa siku mbili.

"Niwaahidi kuwa wizara ninayoiongoza itawapa ushirikiano wote mnaouhitaji ili kuleta matokeo chanya katika sekta ya habari, utamaduni, sanaa na michezo," amesema Prof. Kabudi.

Waziri Kabudi amesema Serikali inayoongozwa na Dkt. Samia Suluhu Hassan inaendelea kushughulikia changamoto mbalimbali zinazoikabili sekta ya habari na kuahidi kuwa wizara yake itatoa ushirikiano unaohitajika ili kuhakikisha vyombo vya habari vinatoa mchango chanya kwa taifa.

Prof. Kabudi pia amesisitiza umuhimu wa vyombo vya habari kutoa maudhui yenye tija kwa jamii badala ya kuangazia burudani pekee, huku akiwakumbusha waandishi kuzingatia weledi na kuacha kusambaza habari za upotoshaji.

Katika mkutano huo ulioandaliwa na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), wadau wa sekta ya habari wamejadili wajibu wa vyombo vya utangazaji katika kulinda haki, usawa, na weledi wa habari kuelekea uchaguzi mkuu.

Prof. Kabudi pia amewataka watangazaji kutumia Kiswahili fasaha na sanifu badala ya kuvuruga maneno na kuharibu ufasaha wa lugha.

"Vyombo vya habari vina jukumu kubwa la kuelimisha umma, lakini tumeshuhudia mabadiliko ya matumizi ya Kiswahili yasiyo sahihi. Ni jukumu lenu kurudisha heshima ya lugha yetu,” amesema Kabudi.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa TCRA, Dkt. Jabir Bakari, amesema mkutano huo unatoa nafasi kwa wadau wa utangazaji kujadili changamoto za sekta hiyo na kubuni mbinu za kuboresha huduma za utangazaji nchini.

Naye Msemaji Mkuu wa Serikali, Grayson Msigwa, amewakumbusha waandishi wa habari kuwa na umakini mkubwa katika matumizi ya teknolojia za kisasa, hususan Akili Bandia (AI), ili kuhakikisha taarifa zinazochapishwa au kutangazwa haziwezi kupotosha umma.

Mkutano huo utaendelea hadi Februari 14, 2025, ambapo mada mbalimbali kuhusu mustakabali wa sekta ya utangazaji kuelekea Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025 zitajadiliwa.

Mkutano huo unahusisha waandaaji wa maudhui, wasambazaji wa habari mtandaoni, wauzaji wa vifaa vya utangazaji, na wadau wa sekta ya habari, huku kaulimbiu ikiwa "Wajibu wa Vyombo vya Utangazaji kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2025."Waziri wa  Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Prof. Palamagamba Kabudi  akitoa hotuba wakati akifungua Mkutano wa Mwaka wa Vyombo vya Utangazaji Tanzania ' Annual Broadcaster's Conference'

Mkurugenzi Mkuu wa TCRA, Dkt. Jabiri Bakari, akizungumza kwenye mkutano wa Mwaka wa vyombo vya utangazaji, leo Februari 13, 2025.




 


Post a Comment

Previous Post Next Post