" HALMASHAURI YA WILAYA YA SHINYANGA YAKABIDHI MIKOPO YA ASILIMIA KUMI KWA AWAMU YA PILI YENYE THAMANI YA ZAIDI YA MILIONI 500

HALMASHAURI YA WILAYA YA SHINYANGA YAKABIDHI MIKOPO YA ASILIMIA KUMI KWA AWAMU YA PILI YENYE THAMANI YA ZAIDI YA MILIONI 500

Na Mapuli Kitina Misalaba

 Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga, Wakili Julius Mtatiro, amevionya vikali vikundi vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu walionufaika na mikopo kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga, akisisitiza kuwa serikali haitasita kuchukua hatua kali, ikiwemo kifungo cha jela, kwa wale watakaoamua kugeuza matumizi ya fedha hizo kinyume na makubaliano ya awali.

Akizungumza leo Mei 27, 2025, wakati wa hafla ya uzinduzi wa utoaji wa mikopo ya awamu ya pili kwa vikundi vilivyokidhi vigezo, Mtatiro amesema serikali imejitoa kwa dhati kuwainua wananchi kiuchumi kupitia mikopo hiyo isiyo na riba, hivyo ni wajibu wa wanavikundi kuhakikisha fedha hizo zinatumika kama ilivyokusudiwa.

“Tunapotoa fedha hizi, tunatarajia zielekezwe katika malengo yaliyowasilishwa kwenye maombi ya mkopo. Kama kuna mtu ndani ya kikundi atataka kutumia fedha kwa shughuli binafsi au tofauti na walivyokubaliana, serikali itamchukulia hatua kali ikiwemo kumfikisha mahakamani na kumfungia jela,” amesema Mtatiro kwa msisitizo.

Aidha, amewataka wanavikundi kushirikiana kwa karibu katika utekelezaji wa miradi yao na hasa katika matumizi ya fedha, huku akitoa pongezi kwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga, Dkt. Kalekwa, watumishi wa halmashauri hiyo, Mwenyekiti wa Halmashauri na baraza la madiwani kwa kusimamia vyema mapato ya ndani hali iliyosababisha halmashauri hiyo kuvuka malengo ya makusanyo kwa zaidi ya asilimia 100.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga, Dkt. Kalekwa Kasanga, amevitaka vikundi hivyo kuwa na juhudi katika biashara na miradi yao ili kuhakikisha wanaongeza tija na kupata faida, huku akisisitiza umuhimu wa nidhamu ya kifedha.

“Mkumbuke fedha hizi si za msaada, ni mkopo. Mnapaswa kuzirudisha kwa wakati ili kuwezesha wengine kupata fursa hii. Kama kuna mtu atataka kuingilia au kutumia fedha zenu kinyume na utaratibu, taarifa zitolewe kwa viongozi ili hatua zichukuliwe,” amesema Dkt. Kalekwa.

Naye Mbunge wa Jimbo la Solwa, Mhe. Ahmed Ally, amepongeza jitihada za Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutoa fedha za maendeleo, akisema kuwa hatua hiyo imeleta mwanga mpya wa maendeleo kwa wananchi wa jimbo lake.

Mbunge huyo amevihimiza vikundi kurejesha mikopo kwa wakati ili kuendelea kunufaika katika awamu zijazo, huku akiwasihi wananchi kuendelea kumwamini na kumuunga mkono Rais Samia katika kila hatua.

“Nawaomba wananchi tuendelee kumuunga mkono Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa kumpigia kura nyingi ifikapo wakati wa uchaguzi, ili aendelee na kazi nzuri ya kuwaletea maendeleo. Pia ni muhimu jimbo hili liendelee kuwa na mbunge wa CCM ili tushirikiane vizuri katika kusukuma gurudumu la maendeleo,” amesema Ahmed.

Akiwasilisha taarifa ya mikopo hiyo, Mkuu wa Divisheni ya Maendeleo ya Jamii wa Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga, Joseph Ntomela amesema mikopo hiyo inatolewa kwa mujibu wa agizo la serikali na kufuatia maboresho ya taratibu za usimamizi wa mikopo isiyo na riba kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu.

Katika awamu ya kwanza, Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga ilitoa mikopo yenye jumla ya Tsh 152,500,000 kwa vikundi 15 vilivyokidhi vigezo: ambapo Vikundi vya wanawake: 8 – Tsh 81,500,000 huku Vikundi vya vijana: 7 – Tsh 71,000,000

Katika awamu ya pili (Januari – Machi 2025), vikundi 94 vilisajiliwa, vikiwa na jumla ya maombi ya mkopo yenye thamani ya Tsh 2,452,468,300. Baada ya uhakiki, vikundi 56 pekee ndivyo vilivyokidhi vigezo na kupatiwa mikopo yenye jumla ya Tsh 537,800,000:

Vikundi vya wanawake: 32 – Tsh 310,100,000, Vikundi vya vijana: 20 – Tsh 209,400,000 na Vikundi vya watu wenye ulemavu: 4 – Tsh 18,300,000

Baada ya kupokea hundi zao, wanavikundi wanapewa mafunzo maalum yatakayowasaidia katika utekelezaji wa miradi yao. Mafunzo haya yanajumuisha mada zifuatazo:

Utunzaji wa kumbukumbu na uwekaji wa akiba, Usimamizi wa miradi ya kilimo na mifugo, Ujasiriamali na masoko, Uendeshaji wa vikundi, Uzalendo katika usimamizi wa mali, Taratibu za kurejesha mkopo, Mipango ya maendeleo, Sheria na kanuni za mikopo, Wajibu na haki za wanakikundi na Utatuzi wa migogoro ya kikundi

Miongoni mwa vigezo vya msingi ili kikundi kuwa na safia ya kupata mkopo ni: Wanakikundi wawe raia wa Tanzania, Umri wa vijana kati ya miaka 18 hadi 45, Kikundi kiwe kimesajiliwa katika mfumo wa serikali, Kikundi kiwe na akaunti ya benki, Kisiwe na wanachama wenye ajira rasmi ambapo kwa watu wenye ulemavu, kuwe na walau wanakikundi wawili

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga Mhe. Ngassa Mboje umemshukuru Rais Dkt. Samia kwa kuwezesha upatikanaji wa mikopo hiyo isiyo na riba, na kutoa wito kwa wanavikundi kutumia vyema mikopo hiyo, kurejesha kwa wakati, na kujiletea maendeleo endelevu kwa faida ya jamii na taifa kwa ujumla.Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga, Wakili Julius Mtatiro, akizungumza leo Mei 27, 2025, wakati wa hafla ya uzinduzi wa utoaji wa mikopo ya awamu ya pili kwa vikundi vilivyokidhi vigezo katika Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga.Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga, Wakili Julius Mtatiro, akizungumza leo Mei 27, 2025, wakati wa hafla ya uzinduzi wa utoaji wa mikopo ya awamu ya pili kwa vikundi vilivyokidhi vigezo katika Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga.

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga Mhe. Ngassa Mboje akizungumza leo Mei 27, 2025, wakati wa hafla ya uzinduzi wa utoaji wa mikopo ya awamu ya pili kwa vikundi vilivyokidhi vigezo katika Halmashauri hiyo.


Post a Comment

Previous Post Next Post