" MKUU WA MKOA SHINYANGA AONGOZA MAANDAMANO YA WAFANYAKAZI KWA SIKU YA MEI MOSI

MKUU WA MKOA SHINYANGA AONGOZA MAANDAMANO YA WAFANYAKAZI KWA SIKU YA MEI MOSI

Na Mapuli Kitina Misalaba

Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mhe. Anamringi Macha ameongoza maelfu ya wafanyakazi kutoka taasisi mbalimbali katika maandamano ya amani ikiwa ni sehemu ya maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani yanayofanyika leo Mei 1, 2025.

Maandamano hayo yameanzia katika viwanja vya Zimamoto mjini Shinyanga na kuelekea uwanja wa CCM Kambarage ambako sherehe za kimkoa zinaendelea kwa shamrashamra mbalimbali zikiwemo burudani na utoaji wa zawadi kwa wafanyakazi bora.

Wafanyakazi kutoka Halmashauri zote sita za Mkoa wa Shinyanga — Manispaa ya Kahama, Manispaa ya Shinyanga, Halmashauri ya Wilaya ya Ushetu, Kishapu, Msalala pamoja na Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga — wamejitokeza kwa wingi kuonesha mshikamano wao katika kutambua mchango mkubwa wanaoutoa katika maendeleo ya jamii na taifa kwa ujumla.

Maadhimisho ya mwaka huu yamebebwa na kaulimbiu isemayo “UCHAGUZI MKUU 2025 UTULETEE VIONGOZI WANAOJALI HAKI NA MASLAHI YA WAFANYAKAZI, SOTE TUSHIRIKI”, ikiwa ni wito kwa Watanzania kushiriki kikamilifu katika mchakato wa uchaguzi kwa maslahi ya wafanyakazi.

Shughuli za maadhimisho zinaendelea katika uwanja wa CCM Kambarage kwa kushirikisha viongozi wa serikali, vyama vya wafanyakazi na wadau mbalimbali wa maendeleo kutoka ndani ya mkoa wa Shinyanga.




 

Post a Comment

Previous Post Next Post