" UMOJA WA WANAUME MKOA WA SHINYANGA WATAKA WANAUME WASHIRIKI KIKAMILIFU KATIKA MALEZI YA WATOTO

UMOJA WA WANAUME MKOA WA SHINYANGA WATAKA WANAUME WASHIRIKI KIKAMILIFU KATIKA MALEZI YA WATOTO


Na Mapuli Kitina Misalaba

Umoja wa Wanaume Mkoa wa Shinyanga umetumia mdahalo wa kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Familia kutoa wito kwa wanaume kushiriki kikamilifu katika malezi na makuzi ya watoto ili kujenga familia bora na taifa imara.

Akizungumza katika mdahalo huo uliofanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Manispaa ya Shinyanga, Katibu wa Umoja huo, Mzee Nsolo Stephen, amesema bado kuna changamoto kubwa ya wanaume wengi kujiondoa kwenye majukumu ya msingi ya malezi na kuacha mzigo huo kwa wanawake pekee.

“Kuna haja kubwa ya mabadiliko ya mtazamo katika jamii. Wanaume hawapaswi kuonekana kama wahudumu wa mahitaji ya kifedha tu, bali washiriki wa moja kwa moja katika malezi ya watoto wao,” amesema Mzee Nsolo.

Kwa upande wake, Katibu Msaidizi wa Umoja huo, Simeo Makoba, amesisitiza kuwa jukumu la malezi ni la pamoja na linahitaji ushirikiano kati ya baba na mama ili mtoto akue katika mazingira yenye upendo, maadili na uelewa.

“Ukosefu wa ushiriki wa baba katika malezi umesababisha mmomonyoko wa maadili kwa baadhi ya watoto. Tunapaswa kurejesha misingi ya familia zenye mshikamano,” amesema Makoba.

Umoja huo umetoa wito kwa jamii kuondoa dhana potofu kuwa malezi ni kazi ya wanawake pekee na badala yake kujenga utamaduni wa kushirikiana kuanzia ngazi ya familia.

LEO NI SIKU YA FAMILIA DUNIANI ambapo Mkoa wa Shinyanga umeadhimisha kwa kufanya mdahalo wa kujadili masuala ya malezi na ustawi wa mtoto kauli mbiu inasema‘Mtoto ni Malezi: Msingi wa Familia Bora Taifa Imara’.Katibu wa Umoja wa Wanaume Mkoa wa Shinyanga, Mzee Nsolo Stephen.Katibu Msaidizi wa Umoja wa Wanaume Mkoa wa Shinyanga, Simeo Makoba.



Post a Comment

Previous Post Next Post