
Na Mapuli Kitina Misalaba
Wananchi wa Mkoa wa Shinyanga wenye changamoto ya magonjwa ya macho wametakiwa kujitokeza kwa wingi kupata huduma za kibingwa za matibabu ya macho zitakazoanza kutolewa rasmi kuanzia Juni 2, 2025 katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga.
Huduma hiyo mpya
inalenga kupunguza msongamano wa wagonjwa wanaosafiri umbali mrefu kufuata
matibabu ya macho katika hospitali kubwa kama Bugando Mwanza au Muhimbili Dar
es Salaam.
Akizungumza na
waandishi wa habari, Mganga Mfawidhi wa Hospitali hiyo Dkt. Luzila John amesema
huduma hiyo ya macho ni ya kibingwa na itakuwa ikitolewa mara mbili kwa wiki
katika hospitali hiyo, ikiwa ni pamoja na upasuaji wa macho, uchunguzi wa kina
wa macho, matibabu ya mtoto wa jicho, presha ya macho, aleji pamoja na uoni
hafifu.
Amesema kuwa huduma
hiyo itazinduliwa rasmi Juni 2, na siku hiyo itaambatana na kuanza kwa kambi
maalum ya huduma za macho kwa wananchi ambayo itaendelea hadi Juni 6, kabla ya
huduma hizo kuendelea kutolewa kwa utaratibu wa kawaida kila wiki.
Ameeleza kuwa sababu
kubwa ya kuanzishwa kwa huduma hizo ni ongezeko la mahitaji ya huduma ya macho
katika mkoa wa Shinyanga, ambapo awali kulikuwa na kituo kimoja tu kilichokuwa
kikitoa huduma hiyo kwa kiwango kidogo.
Aidha, Dkt. Luzila
amesema hospitali hiyo tayari imewekeza zaidi ya shilingi milioni 79 kwa ajili
ya ununuzi wa vifaa tiba vya kisasa vinavyotumika katika matibabu ya macho, na
kwamba tayari wameshamaliza kumsomesha daktari bingwa wa macho ambaye sasa yupo
tayari kuhudumia wananchi.
Baadhi ya wakazi wa
Shinyanga wamepongeza kuanzishwa kwa huduma hizo wakisema kuwa hatua hiyo ni ya
muhimu sana kwa sababu itapunguza gharama walizokuwa wakitumia kusafiri hadi
Mwanza au Dar es Salaam kutafuta huduma za macho.
Hospitali ya Rufaa ya
Mkoa wa Shinyanga inatarajia kuwa kituo muhimu cha huduma bora kwa wagonjwa wa
macho kutoka wilaya zote za mkoa huo na maeneo jirani, huku ikisisitiza kuwa
huduma hizo ni endelevu, kwa kutumia wataalamu waliobobea na vifaa tiba vya
kisasa.
Post a Comment