" JESHI LA JADI SUNGUSUNGU SHINYANGA VIJIJINI LAADHIMISHA MIAKA 43 KWA KISHINDO, – WAPONGEZWA NA SERIKALI KWA KAZI YA ULINZI WA RAIA NA MALI ZAO

JESHI LA JADI SUNGUSUNGU SHINYANGA VIJIJINI LAADHIMISHA MIAKA 43 KWA KISHINDO, – WAPONGEZWA NA SERIKALI KWA KAZI YA ULINZI WA RAIA NA MALI ZAO

Na Mapuli Kitina Misalaba

Jeshi la Jadi la Sungusungu Wilaya ya Shinyanga Vijijini leo Juni 12, 2025  limeadhimisha miaka 43 tangu kuanzishwa kwake kwa sherehe iliyoambatana na ujumbe wa kuendelea kushirikiana na serikali kuhakikisha ulinzi wa watu na mali unaimarika zaidi katika vijiji.

Maadhimisho hayo yamefanyika katika Kata ya Iselamagazi yakihudhuriwa na sungusungu kutoka tarafa tatu za Iselemagazi Mashariki, Nhindo Magharibi na Itwangi, wakiongozwa na viongozi wao wa ngazi mbalimbali.

Akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga mgeni rasmi, Mtendaji wa Kata ya Iselamagazi Amos Chacha, amepongeza jeshi hilo la jadi kwa kuendelea kuwa chombo muhimu katika suala la ulinzi wa raia na mali, na kuwasisitiza wanajeshi hao wa jadi kuendelea kufanya kazi kwa kufuata sheria na kanuni za nchi.

"Nipende kuwapongeza sungusungu kwa kuandaa sherehe hii ya kuadhimisha miaka 43 ya sungusungu nawapongeza sana, kazi ya sungusungu ni kulinda mali na raia, kwenye hili suala la ulinzi tujitahidi kuzingatia sheria na kanuni za nchi, tusije tukajichukulia sheria mkononi," amesema.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Sungusungu Wilaya ya Shinyanga Vijijini, Mabeja Halawa, amesema jeshi hilo liliundwa kwa lengo mahsusi la kusimamia haki za watu na mali zao, likiwa chombo cha wananchi wenyewe kwa ajili ya usalama wao.

"Jeshi la jadi la sungusungu litaendelea kushirikiana bega kwa bega na serikali kuhakikisha ulinzi wa watu na mali zao unaimarika zaidi vijijini," amesema Halawa.

Naye Mkuu wa Kituo cha Polisi Ndindo, Blighton Rutajama, ametumia nafasi hiyo kuwataka sungusungu kuendeleza ulinzi shirikishi kwa kushirikiana kwa karibu zaidi na Jeshi la Polisi katika kudhibiti na kutokomeza vitendo vya uhalifu.

Mhasibu wa Sungusungu Wilaya hiyo Mzee Malongo Mshali akisoma historia amesema sungusungu imeanzishwa rasmi tarehe 12 Juni, 1981, chini ya usimamizi wa Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Shinyanga iliyokuwa chini ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Aidha, Mshali ameeleza kuwa mwaka 1982, hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, aliyekuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, aliridhia rasmi Jeshi la Jadi kuwa sehemu ya ulinzi katika jamii kwa lengo la kukabiliana na uhalifu na kulinda mali za wananchi.

Katika sherehe hizo, kanuni rasmi za usalama na muundo wa kamati ya ulinzi ya jadi zimesomwa na Daud Ludelengeja, akifafanua kuwa sungusungu huongozwa kwa misingi ya uwazi, ukweli, na nidhamu ya hali ya juu. Mtu anayetaka kuwa kiongozi wa sungusungu anatakiwa kuwa na sifa ya kuwa na mji, kaya, tabia njema na awe msiri na mkweli mbele ya jamii.

Muundo wa uongozi wa sungusungu unaanza na kuchagua Mtemi Mkuu, Kamanda Mkuu, Katibu Mkuu, pamoja na makamanda wa vikosi vidogo na wajumbe kutoka pande mbalimbali. Kiongozi hawezi kuondolewa isipokuwa kwa sababu za kiafya, kifo, kuhama, au kuonekana na tabia mbaya mbele ya jamii.

Katika kilele cha maadhimisho hayo, viongozi mbalimbali wamekumbusha umuhimu wa kuheshimu mila, desturi, na miongozo ya ulinzi ya jadi, huku wakisisitiza kuwa sungusungu inapaswa kuendelea kuwa chombo cha kuigwa katika ujenzi wa amani, mshikamano na maendeleo vijijini.

Mkuu wa Kituo cha Polisi Ndindo, Blighton Rutajama, akizungumza kwenye maadhimishi hayo ya Miaka 43 tangu kuanzishwa kwa jeshi la jadi Sungusungu Wilaya ya Shinyanga vijijini.

 

Post a Comment

Previous Post Next Post