Wananchi wa Kata ya Iparamasa, Wilayani Chato mkoani Geita wamemshukuru
Mjumbe wa Mkutano Mkuu wa Taifa wa CCM, Paschal Lutandula, kwa kufanikisha
ukamilishaji wa mfumo wa maji taka katika wodi ya wazazi kwenye Kituo cha Afya
cha Iparamasa, uliokuwa umekwama kwa zaidi ya miezi sita.
Kukwama kwa mfumo huo kulisababisha wanawake kutumia choo kimoja kwa pamoja
na wanaume, hali iliyozua usumbufu na kero kubwa hasa kwa akinamama wajawazito
na waliojifungua. Hata hivyo, baada ya jitihada za Lutandula, kazi hiyo ilikamilika
ndani ya wiki moja na vyoo hivyo kukabidhiwa rasmi kwa wananchi.
Wananchi kwa furaha kubwa walimlaki Lutandula kwa bashasha, nyimbo za
shukrani na vifijo, wakieleza kuwa hatua hiyo imeondoa usumbufu mkubwa
waliokuwa wakiupata kwa muda mrefu.
Akizungumza wakati wa makabidhiano hayo, Mwenyekiti wa Bodi ya Afya ya kituo
hicho, John Buswelu, alisema:
“Wananchi, hususan akinamama wajawazito na waliojifungua, walikuwa wakipata
shida kutumia vyoo vya nje. Tulifikisha kilio chetu kwa Mjumbe wa Mkutano Mkuu
na ndani ya wiki moja alihakikisha mfumo huo unakamilika.”
Naye Mganga Mfawidhi wa Kituo hicho, Rechol
Holomi, alieleza kuwa upatikanaji wa mfumo wa maji taka ni hatua kubwa katika
kuboresha mazingira ya huduma kwa akinamama, hususan kipindi cha ujauzito na
kujifungua.
Baadhi ya wananchi pia walitoa shukrani zao kwa Lutandula na kuwataka wadau wengine wa maendeleo kuiga mfano wake wa uzalendo na kujitolea katika kutatua changamoto zinazowakabili wananchi wa kawaida.
Post a Comment