" NYUNDO FC YAIONDOA NZOZA FC KWA PENATI, MAWEMIRU FC NA MAHEMBE FC KUKIPIGA KESHO

NYUNDO FC YAIONDOA NZOZA FC KWA PENATI, MAWEMIRU FC NA MAHEMBE FC KUKIPIGA KESHO

Na Mapuli Kitina Misalaba

Timu ya NYUNDO FC imefanikiwa kutinga hatua inayofuata ya mashindano ya NIACHEKONA CUP 2026 baada ya kuiondoa NZOZA FC kwa mikwaju ya penati kufuatia mchezo wa leo Jumapili Mei 31, 2026 ambapo umemalizika bila kufungana ndani ya dakika 90 za kawaida.

Mchezo huo uliochezwa katika uwanja wa Mwabenda kata ya Solwa, Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga ulikuwa na ushindani mkubwa huku timu zote zikitengeneza nafasi mbalimbali za kufunga lakini zikiwa hazikufanikiwa kuzitumia ipasavyo.

Baada ya dakika 90 kumalizika kwa sare ya 0-0, sheria za mashindano zilihitaji mshindi kupatikana kwa mikwaju ya penati ambapo NYUNDO FC ilionesha utulivu mkubwa na kufanikiwa kushinda kwa penati 5-3.

Katika hatua hiyo, NZOZA FC ilikosa penati moja muhimu iliyowagharimu nafasi ya kuendelea na mashindano hayo, huku NYUNDO FC ikitumia vizuri nafasi zake zote na kufuzu hatua inayofuata.

Kutokana na ushindi huo, NYUNDO FC sasa itasubiri mshindi wa mchezo wa kesho ili kujua mpinzani wake katika hatua inayofuata ya mashindano hayo yanayoendelea kuvutia timu na mashabiki kutoka ndani na nje ya Mkoa wa Shinyanga.

Akizungumza baada ya mchezo huo, Makamu Mwenyekiti wa NIACHEKONA CUP, Bwana Samwel Stephen ametangaza ratiba ya mchezo wa kesho ambapo MAWEMIRU FC itamenyana na MAHEMBE FC katika pambano linalotarajiwa kuwa na ushindani mkubwa.

Ameendelea kuwahimiza wananchi, wadau wa michezo pamoja na mashabiki wa soka kujitokeza kwa wingi katika uwanja wa Mwabenda ili kuendelea kushuhudia vipaji vya vijana pamoja na burudani ya soka inayotolewa kupitia mashindano hayo.

Mashindano ya NIACHEKONA CUP 2026 yameandaliwa na Paul Daud Augustino (MC NIACHEKONA) kwa ufadhili wa Shirika la Lushu Foundation kwa lengo la kuibua vipaji vya vijana, kuimarisha amani na kukuza michezo katika jamii.

Kwa huduma za ushereheshaji wa matukio mbalimbali, matangazo na burudani, MC NIACHEKONA anapatikana kupitia namba 0757 267 738.

Kikosi cha Nzoza FC.

Post a Comment

Previous Post Next Post