" ACT WAZALENDO WAMTAMANI MHANDISI JAMES JUMBE KWA UWEZO WAKE WA KISIASA

ACT WAZALENDO WAMTAMANI MHANDISI JAMES JUMBE KWA UWEZO WAKE WA KISIASA

Na Mwandishi wetu, Misalaba Media

Uwezo wa kisiasa na ushawishi wa Mhandisi James Jumbe unaendelea kuvutia hata nje ya mipaka ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), baada ya Naibu Waziri Kivuli wa Habari, Mawasiliano na TEHAMA kupitia ACT Wazalendo, Emmanuel Ntobi, kuonesha wazi kutamani kushirikiana naye katika harakati za kuwatumikia wananchi.

Kupitia ujumbe wake wa hadharani, Ntobi amemwelezea Jumbe kama kiongozi mwenye mvuto na anayekubalika kwa wananchi wa Shinyanga Mjini, akisisitiza kuwa taifa linahitaji viongozi wa aina hiyo wenye maono na ushawishi wa kweli.

Si kawaida kwa chama cha upinzani kumvutiwa waziwazi na mwanasiasa kutoka chama tawala, lakini mchango na mwenendo wa Jumbe umeonesha tofauti kubwa na kuwafanya wapinzani waone umuhimu wa kuungana naye katika mustakabali wa kisiasa wa taifa.

Tunamkaribisha ACT – chama cha vitendo – tukapambane kwa ajili ya wananchi. Safari hii, tunahitaji ushindani wa haki bila kubughudhiwa na vyombo vya dola. Wananchi wanahitaji mtu jasiri, si maneno matupu!”amesema Ntobi

Kauli hiyo inakuja muda mfupi baada ya Jumbe kutoa salamu za shukrani kwa CCM na kueleza kuwa licha ya kutopitishwa kuwania ubunge, ameendelea kujifunza mengi, na yupo tayari kuendelea kulitumikia taifa kwa namna yoyote ile itakayowezekana.

Kwa wachambuzi wa siasa mkoani Shinyanga, kauli ya ACT Wazalendo imechukuliwa kama ishara ya wazi kuwa Jumbe ni kiongozi mwenye mvuto mpana unaovuka mipaka ya chama kimoja, huku wananchi wakisubiri kwa hamu kuona hatua yake inayofuata.


Post a Comment

Previous Post Next Post