Mtangazaji mahiri wa kituo cha matangazo cha Gold FM kilichopo Wilaya ya Kahama, mkoani Shinyanga, Steven Kanyefu (@mr.notification_) ametajwa kuwa mtangazaji bora namba moja kwa kipindi cha Januari hadi Juni mwaka huu (2025).
Kanyefu ametajwa kwenye
orodha ya heshima kupitia ripoti maalum iliyotolewa na @radiodoctor_tz,
chombo kinachojihusisha na ufuatiliaji wa vipindi vya redio na tathmini ya
ubora wa watangazaji kutoka mikoa mbalimbali nchini Tanzania.
Kwa mujibu wa taarifa
hiyo, Kanyefu ameibuka kinara kutokana na ubunifu wake,
umahiri mkubwa wa uwasilishaji wa vipindi, na zaidi uwezo wake
wa kuvutia wasikilizaji kwa sauti yake yenye mvuto na hoja zenye mashiko
anazowasilisha hewani kila siku kupitia Gold FM.
Ripoti hiyo imebainisha kuwa miongoni mwa vigezo vilivyotumika kumpa ushindi huo ni kazi bora anayofanya akiwa hewani, namna wasikilizaji wanavyomfuatilia kwa njia ya mtandao, na mchango wake mkubwa katika kushirikisha jamii kupitia vipindi vyake.
Kwa hatua hiyo, Steven Kanyefu ameendelea kuipeperusha vyema bendera ya Kahama na Mkoa wa
Shinyanga katika tasnia ya habari na utangazaji, na kuwa mfano
wa kuigwa kwa watangazaji wengine nchini.
MISALABA MEDIA inatoa pongezi kwa Kanyefu kwa heshima hiyo ya kitaifa – hakika ni ushindi unaotokana na bidii, uthubutu na mapenzi kwa kazi.
👉WAFANYAKAZI GOLD FM WANG'ARA KATIKA MAADHIMISHO YA MEI MOSI 2025
Post a Comment