" KATAMBI AWAITA WANANCHI WA SHINYANGA KUSIKILIZA ILANI YA CCM KWENYE MKUTANO WA DKT. NCHIMBI

KATAMBI AWAITA WANANCHI WA SHINYANGA KUSIKILIZA ILANI YA CCM KWENYE MKUTANO WA DKT. NCHIMBI

Na Mapuli Kitina Misalaba


Mgombea Ubunge wa Jimbo la Shinyanga Mjini kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) katika Uchaguzi Mkuu wa 2025, Paschal Patrobas Katambi, amewaomba wananchi wa Shinyanga kujitokeza kwa wingi kushiriki mkutano mkubwa wa kampeni utakaohusisha ujio wa Mgombea Mwenza wa Kiti cha Urais wa CCM, Dkt. Emmanuel Nchimbi, ambaye anatarajiwa kuwasili mkoani Shinyanga kesho Septemba 3, 2025.

Katambi ameyasema hayo leo Septemba 2, 2025 alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari, akibainisha kuwa mkutano huo utakuwa fursa muhimu kwa wananchi kusikiliza kwa kina sera, mafanikio na Ilani ya CCM kuelekea Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025.

Amesema wananchi wa Shinyanga wanapaswa kujitokeza kwa wingi siyo tu kumsikiliza Dkt. Nchimbi, bali pia kupata elimu ya moja kwa moja kuhusu utekelezaji wa miradi ya maendeleo iliyofanywa na Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kipindi cha miaka mitano iliyopita, pamoja na mipango mipya ya maendeleo kwa miaka mitano ijayo kupitia Ilani ya CCM 2025–2030.

“Wananchi wa Shinyanga wajitokeze kwa wingi kwenye ujio wa Mgombea Mwenza wa Kiti cha Urais, Dkt. Emmanuel Nchimbi, wasikilize sera za CCM kupitia Ilani yetu na kufahamu pia kuhusu Shinyanga Mpya ya 2025–2030,” amesema Katambi.

Katambi ameongeza kuwa katika mkutano huo viongozi wa chama na wagombea watatoa maelezo ya kina kuhusu hatua kubwa za kimaendeleo zilizofikiwa katika sekta mbalimbali za kijamii na kiuchumi, ikiwemo elimu, afya, barabara, maji na ajira, ambazo zimekuwa na mchango mkubwa katika kuinua maisha ya wananchi wa Shinyanga na Tanzania kwa ujumla.

Aidha, amesisitiza kuwa ujio wa Dkt. Nchimbi ni ishara ya kujali mkoa wa Shinyanga na ni nafasi kwa wananchi kuonyesha mshikamano wao na chama kwa kujitokeza kwa wingi ili kusikiliza, kuuliza maswali na kushiriki katika mjadala wa maendeleo ya taifa kupitia Ilani ya CCM.

Kesho Septemba 3, 2025, Dkt. Emmanuel Nchimbi anatarajiwa kuwasili rasmi mkoani Shinyanga kwa ajili ya kampeni hizo za kunadi sera na ilani ya chama hicho, kuelekea Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025. 

🥃🍶 TUMIA VINYWAJI BORA VYA EAST AFRICAN SPIRITS – BEI RAFIKI, LADHA SAFI BILA HARUFU MBAYA

Post a Comment

Previous Post Next Post