" SERIKALI NA SHIRIKA LA CSEMA WAKUTANISHA TAASISI MBALIMBALI KUJADILI UTOAJI WA HAKI KWA WAHANGA WA UKATILI

SERIKALI NA SHIRIKA LA CSEMA WAKUTANISHA TAASISI MBALIMBALI KUJADILI UTOAJI WA HAKI KWA WAHANGA WA UKATILI

Na Mapuli Kitina Misalaba

Serikali mkoani Shinyanga kwa kushirikiana na Shirika la CSEMA chini ya ufadhili wa UNFPA imewakutanisha wajumbe wa kamati ya kusukuma mashauri ngazi ya Mahakama kutoka ngazi ya Mkoa na Wilaya zote za Shinyanga, kwa lengo la kujadili utekelezaji wa huduma za uendeshaji mashauri ya ukatili wa kijinsia na ukatili dhidi ya watoto.

Akizungumza wakati wa semina hiyo, Afisa Ustawi wa Jamii kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Lydia Kwesigabo, amesema kuwa semina hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa Mradi wa Haki Yangu, Chaguo Langu, ambao unalenga kuimarisha mpango mkakati wa kitaifa wa kutokomeza ukatili wa kijinsia kwa wanawake na watoto (MTAKUWWA) pamoja na mpango mkakati wa Mkoa wa Shinyanga wa kutokomeza ukatili huo.

“Kupitia semina hii tumekutanisha wadau kutoka sekta mbalimbali ili kujadili changamoto zinazojitokeza katika mashauri ya ukatili wa kijinsia na kutafuta njia za kuyasogeza mbele hadi kufikia hatua ya haki. Pia tunajengeana uwezo na kuongeza uelewa wa pamoja kwa wataalam wote wanaoshughulika na mashauri haya,” amesema Lydia.

Ameongeza kuwa Mradi wa Haki Yangu, Chaguo Langu unatekelezwa kwa ushirikiano kati ya serikali, UNFPA, CSEMA, na mashirika mengine ya kiraia, ambapo kupitia mikutano kama hiyo, wadau wanabaini changamoto, kupanga mikakati, na kuimarisha uratibu wa pamoja katika mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia.

Kwa upande wake, Mratibu wa Mradi wa Haki Yangu, Chaguo Langu kutoka Ofisi ya Kanda ya Shinyanga Bi. Jane Haule, amesema sekta ya Mahakama ina nafasi muhimu katika kusukuma mbele mashauri ya ukatili wa kijinsia na kuhakikisha haki inapatikana kwa wahanga, hasa wanawake na watoto wenye ulemavu.

“Mahakama ni mhimili muhimu sana wa haki. Ushirikiano kati ya taasisi hizi ni hatua kubwa katika kuhakikisha kesi za ukatili zinapewa kipaumbele na wahanga wanapata haki zao kwa wakati,” amesema Jane.

Semina hiyo imehusisha taasisi mbalimbali zikiwemo:

Mahakama za Mkoa na Wilaya (Shinyanga, Kishapu na Kahama), Ofisi ya Mashtaka, Ofisi ya Mganga Mkuu wa Mkoa na Wilaya, Idara ya Ustawi wa Jamii Mkoa na Wilaya, Jeshi la Polisi (RCO, OC CID – Kahama na Kishapu, pamoja na Dawati la Jinsia), TAKUKURU, Uhamiaji, Magereza, Ofisi ya Maendeleo ya Jamii, Probation Officer

Semina hiyo ya siku mbili inalenga kutathmini changamoto na mafanikio katika uendeshaji wa mashauri ya ukatili wa kijinsia na dhidi ya watoto, sambamba na kuandaa mpango kazi wa pamoja utakao saidia kuboresha uratibu wa taasisi hizo.

Baadhi ya washiriki wamepongeza CSEMA kwa uratibu mzuri wa semina hiyo na kuahidi kutekeleza kwa vitendo maazimio yote yatakayofikiwa, ili kuhakikisha upatikanaji wa haki kwa wahanga wa ukatili wa kijinsia mkoani Shinyanga.

Mratibu wa Mradi wa Haki Yangu, Chaguo Langu kutoka Ofisi ya Kanda ya Shinyanga Bi. Jane Haule, akielezea umuhimu wa sekta ya Mahakama hasa katika kusukuma mashtaka kuwa sehemu ya kuunga jitihada za upatikanaji wa haki kwa kesi za masuala ya unyanyasaji wa kijinsia hususan zinazohusu wanawake na Watoto wenye ulemavu.





 

Post a Comment

Previous Post Next Post