" Video: KATAMBI ATOA ONYO KWA VIONGOZI WANAOKULA FEDHA ZA WANANCHI

Video: KATAMBI ATOA ONYO KWA VIONGOZI WANAOKULA FEDHA ZA WANANCHI


Na Mapuli Kitina Misalaba

Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Paschal Patrobas Katambi, amewataka watumishi wa serikali na viongozi wa ngazi mbalimbali kutekeleza majukumu yao kwa weledi, uadilifu na kwa kuzingatia sheria ili kulinda usalama na haki za wananchi.

Katambi ametoa maelekezo hayo leo wakati wa ziara yake katika Manispaa ya Shinyanga, ambapo pamoja na mambo mengine amefanya mkutano wa hadhara katika Uwanja wa Zimamoto Nguzonane mjini Shinyanga.

Amesema nchi ilitaka kuingia kwenye majaribu yaliyosababishwa na watu wachache waliotaka kuhatarisha usalama wa taifa, akisisitiza kuwa usalama wa taifa unahusisha haki ya wananchi kuishi kwa amani, kuwa huru katika kufanya shughuli zao, kulindwa mali zao pamoja na kupata haki zao za kiuchumi na kijamii.

Ameeleza kuwa ni wajibu wa serikali kuhakikisha wananchi wanapata huduma za afya, miundombinu bora na haki ya kuchagua viongozi wao kwa mujibu wa sheria, akibainisha kuwa masuala hayo pia ni sehemu ya msingi wa usalama wa taifa.

“Hapa duniani ili tuweze kuishi tunawajibu wa kufuata sheria kwa kuzitekeleza na kuzitii. Ndiyo maana sisi viongozi tumepewa jukumu la kusimamia haki za wananchi, uhai wa wananchi, usalama wa wananchi na mali za wananchi, tukizembea katika kusimamia hayo hakuna mtu ataweza kuishi kirahisi,” amesema Katambi.

Aidha, amewapongeza wananchi wa Jimbo la Shinyanga Mjini kwa kuendelea kuwa kielelezo cha kufuata taratibu na sheria, huku akiahidi kuwa serikali itaendelea kuwahudumia kwa nguvu zote chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan.

Katambi ametoa wito kwa wananchi kuendelea kutoa ushirikiano kwa vyombo vya ulinzi na usalama, akisisitiza kuwa viongozi wote wanapaswa kuwahudumia wananchi kwa uaminifu na haki.

Amesema endapo kiongozi yeyote atabainika kula fedha za wananchi, hatua kali za kisheria zitachukuliwa dhidi yake bila kusita.

“Ukipewa uongozi katika serikali hii ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania hakikisha unatimiza wajibu wako ukijua cheo ni dhamana. Tusinyenyue mabega, tusitunishe matumbo, tufanye kazi kwa niaba ya Rais. Hatutaki viongozi wenye maadili mabaya ambao wanakula rushwa na kuwanyima wananchi haki zao za msingi,” amesisitiza.

 

  • Wasiliana nasi:
    📍 East African Spirits (T) Ltd
    📞 +255 767 650 806 | +255 652 096 254

Post a Comment

Previous Post Next Post