" KAMATI YA SIASA CCM WILAYA YA SHINYANGA MJINI YAKAGUA MIRADI, YAFICHUA CHANGAMOTO KADHAA NA KUTOA MAELEKEZO

KAMATI YA SIASA CCM WILAYA YA SHINYANGA MJINI YAKAGUA MIRADI, YAFICHUA CHANGAMOTO KADHAA NA KUTOA MAELEKEZO

Na Mapuli Kitina Misalaba

Kamati ya Siasa ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Shinyanga Mjini imefanya ziara ya kukagua miradi mbalimbali ya maendeleo katika wilaya hiyo, ikisisitiza umuhimu wa miradi hiyo kukamilika kwa wakati ili wananchi waweze kunufaika na huduma zinazotarajiwa.

Ziara hiyo imefanyika leo Machi 10, 2026 ikiongozwa na Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Shinyanga Mjini, Mhe. Anord Makombe, ambapo kamati hiyo imetembelea miradi kadhaa ikiwemo ujenzi wa standi mpya ya mabasi ya mkoa, ujenzi wa soko kuu la Shinyanga pamoja na mradi wa uboreshaji wa barabara ya kuelekea Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga.

Katika ziara hiyo, kamati ya siasa ilianza kwa kutembelea Shule ya Msingi Bugayambelele ambako Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan imetoa shilingi milioni 25 kwa ajili ya ujenzi wa chumba kimoja cha darasa ili kupunguza changamoto ya upungufu wa madarasa shuleni hapo.

Baada ya hapo kamati hiyo ilitembelea mradi wa ujenzi wa standi mpya ya mabasi ya Mkoa wa Shinyanga unaoendelea katika Kata ya Kizumbi na kwamba wakati wa ukaguzi wa mradi huo, kamati hiyo ilibaini kuwepo kwa changamoto mbalimbali ikiwemo malalamiko kutoka kwa baadhi ya wananchi wanaofanya vibarua katika mradi huo.

Baadhi ya wafanyakazi hao walisema wanalipwa ujira mdogo ambao hauendani na viwango vinavyotakiwa kisheria, huku wakidai pia kucheleweshewa malipo yao kwa takribani mwezi mmoja ambapo walisema licha ya kufanya kazi kwa bidii ili kujipatia kipato, bado malipo yao yanachelewa na kiasi wanachopewa hakiridhishi.

Akizungumza baada ya kusikiliza malalamiko hayo, Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Shinyanga Mjini, Mhe. Anord Makombe amesema kamati hiyo imezipokea changamoto hizo na kuahidi kuzifuatilia ili kuhakikisha haki za wafanyakazi zinazingatiwa kwa mujibu wa sheria.

Katika hatua nyingine, kamati hiyo imetembelea mradi wa ujenzi wa Soko Kuu la Mkoa wa Shinyanga ambapo wafanyabiashara wameendelea kueleza kilio chao cha kutaka mradi huo ukamilike haraka ili waweze kurejea kufanya biashara zao.

Mwenyekiti wa soko hilo amesema wakati wafanyabiashara wanahamishwa kutoka eneo la soko walielezwa kuwa ujenzi ungechukua miezi sita pekee kwani mafundi wangefanya kazi mchana na usiku, lakini hadi sasa ni takribani miaka minne imepita bila mradi kukamilika.

Kwa upande wake, Diwani wa Kata ya Mjini, Mhe. Salum Kitumbo amewaomba wafanyabiashara kuwa na subira huku akiwahakikishia kuwa hatua mbalimbali zimeanza kuchukuliwa kwa kushirikiana na wataalam ili kuhakikisha ujenzi wa soko hilo unakamilika kwa ubora na kwa wakati.

Naye Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Shinyanga Mjini, Mhe. Makombe amesema amepokea changamoto hizo na kuahidi kuwa chama kitaendelea kufuatilia ili kuona mradi huo unakamilika na wananchi wanaanza kunufaika nao.

Katika ziara hiyo, kamati ya siasa pia imekagua mradi wa uboreshaji wa barabara ya kutoka Nguzonane kuelekea Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Shinyanga inayojengwa kwa kiwango cha lami. Hata hivyo kamati hiyo haikuridhishwa na mwenendo wa mradi huo.

Wananchi pamoja na madiwani wa Kata ya Ndani Mhe. Zamda Shaban na Diwani wa Kata ya Masekelo Mhe. Piter Koliba wamesema viongozi mbalimbali wa serikali wamewahi kutembelea mradi huo na kutoa maelekezo, akiwemo Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Shinyanga Mjini Mhe. Paschal Patrobas Katambi, Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga Wakili Julius Mtatiro, Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mhe. Mboni Mhita pamoja na Katibu wa NEC Itikadi, Uenezi na Mafunzo wa CCM, Kenan Kihongosi.

Hata hivyo wamesema pamoja na maelekezo hayo, mkandarasi hajachukua hatua madhubuti na mradi huo umesimama kwa zaidi ya wiki moja bila kazi kuendelea kufanyika.

Kwa mujibu wa viongozi hao, mradi huo una mkataba wa miezi 15 lakini hadi sasa baada ya miezi saba kupita umefikia takribani asilimia 14 tu ya utekelezaji hali inayoonyesha kusuasua kwa ujenzi huo huku wakisisitiza hatua zaidi zichukuliwe ikiwemo kumwondoa mkandarasi endapo ataendelea kuchelewesha mradi huo.

Akizungumzia suala hilo, Mwenyekiti Makombe amesema kamati hiyo imepokea malalamiko hayo na itaendelea kufuatilia ili kubaini changamoto zilizopo na kuhakikisha hatua stahiki zinachukuliwa.

Aidha, kamati hiyo imetembelea Shule ya Sekondari ya Wasichana Shinyanga Girls ambapo imekagua ujenzi wa bweni pamoja na miundombinu mingine ya shule hiyo na kwamba viongozi wa kamati hiyo wametumia fursa hiyo kuishauri serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali kuweka uzio kuzunguka shule hiyo kwa ajili ya kuimarisha usalama wa wanafunzi.

Katika hatua nyingine, kamati hiyo imetembelea Soko la Mitumbani lililopo Kata ya Ngokolona ambapo imesikiliza changamoto zinazowakabili wafanyabiashara wa soko hilo.

Wafanyabiashara wameeleza kuwa baadhi ya miundombinu ya soko hilo siyo rafiki, hususan kipindi cha mvua ambapo maeneo mengi hujaa maji na kufanya mazingira ya biashara kuwa magumu.

Ziara hiyo ya Kamati ya Siasa ya CCM Wilaya ya Shinyanga Mjini ni endelevu na inalenga kufuatilia utekelezaji wa miradi ya maendeleo pamoja na ilani ya chama hicho kwa lengo la kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora zinazokusudiwa na serikali.

Kamati ya Siasa ya CCM Wilaya ya Shinyanga Mjini ikikagua maendeleo ya ujenzi wa standi mpya ya mabasi ya Mkoa wa Shinyanga inayojengwa katika Kata ya Kizumbi.

Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Shinyanga Mjini, Mhe. Anord Makombe, akizungumza.

 

  • Wasiliana nasi:
    📍 East African Spirits (T) Ltd
    📞 +255 767 650 806 | +255 652 096 254

Post a Comment

Previous Post Next Post