Jeshi la Polisi Mkoa wa Shinyanga linawashikilia watu
wawili kwa tuhuma za kuhusika na mauaji ya mwanamke aliyefahamika kwa jina la Hollo
Ruchanganya, mwenye umri wa miaka 60 mkazi wa Kijiji cha Bunambiyu Wilaya ya
Kishapu, huku uchunguzi wa tukio hilo ukiendelea.
Akizungumza na vyombo vya habari, Kamanda wa jeshi la Polisi
Mkoa wa Shinyanga kamishna msaidizi mwandamizi wa Polisi Janeth Magomi, amesema
kuwa tukio hilo linahusishwa na imani za kishirikina, ambapo bado baadhi ya
watu wanaendelea kujihusisha na vitendo hivyo hatarishi.
Amesema tukio hilo lilianzia nyumbani kwa marehemu
baada ya mgeni asiyejulikana kufika majira ya usiku wakati familia ikiandaa
chakula cha jioni, na kujitambulisha kuwa anatoka Kijiji cha Sanga, Mwamashimba
Wilaya ya Kwimba.
Kwa mujibu wa Kamanda Magomi, mgeni huyo aliomba
apelekwe kwa mganga wa jadi anayejulikana kwa jina la Ng’wana Masanja, ambaye
ni ndugu wa marehemu, na baada ya mazungumzo, marehemu aliondoka naye kwa lengo
la kumpeleka.
“Hata hivyo, tangu aondoke na mgeni huyo
hakurejea nyumbani, na baadaye mwili wake ulikutwa majira ya asubuhi na ndugu
yake aliyekuwa akielekea shambani,” amesema Magomi.
Ameongeza kuwa Jeshi la Polisi linaendelea kumsaka mtu
aliyekuwa na marehemu kabla ya kifo chake ili aweze kukamatwa na kufikishwa
mbele ya sheria, huku likisisitiza kuwa halitavumilia vitendo vya mauaji
vinavyochochewa na imani potofu za kishirikina.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kijiji cha Bunambiyu,
Boniphace Zengo, amesema alipokea taarifa za tukio hilo majira ya saa moja
asubuhi na kufika eneo la tukio, ambapo alishirikiana na wananchi pamoja na
familia ya marehemu kupata taarifa za awali.
Amesema familia ilieleza kuwa mgeni huyo alifika
majira ya saa tatu usiku akitafuta waganga wa mapacha na kuelekezwa kwa mtu
anayejulikana kama Ng’wana Masanja, ndipo marehemu alipoamua kuongozana naye
baada ya kumaliza kula chakula.
Hata hivyo, marehemu hakurejea nyumbani na kwamba
alikutwa akiwa ameuawa kisha mwili wake kutupwa katika shamba la mahindi jirani
na makazi yake katika kijiji cha Bunambiyu, wilayani Kishapu mkoani Shinyanga.
🥃🍶 TUMIA VINYWAJI BORA VYA KAMPUNI YA EAST AFRICAN SPIRITS – BEI RAFIKI, LADHA SAFI BILA HARUFU MBAYA
Wasiliana nasi:
📍 East African Spirits (T) Ltd
📞 +255 767 650 806 | +255 652 096 254

Post a Comment